BENKI
 ya NMB kwa kushirikiana na Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), 
wamezindua mashirikiano ya kimkakati na ya Kidijitali ya Ununuzi na 
Uuzaji wa Hisa za Kampuni mbalimbali zilizoorodheshwa DSE ambapo kupitia
 aplikesheni ya NMB mkononi unaeza kuipata huduma ya uuzaji na ununuzi 
wa hisa ya DSE.
Mashirikiano
 haya ni matokeo ya ubunifu na ushirikiano wa muda mrefu kati ya NMB na 
DSE, uliounganisha rasmi mifumo miwili ya suluhishi za kidijitali za NMB
 Mkononi ya Benki ya NMB na Hisa Kiganjani ya Soko la Hisa Dar es 
Salaam.
Akizungumza
 wakati wa uzinduzi huo uliofanyika leo jijini Dar es Salaam, Afisa 
Mtendaji Mkuu wa NMB, Bi Ruth Zaipuna, alisema wanajivunia mashirikiano 
mema na DSE, yaliyozaa huduma hiyo inayowapa Watanzania na Wawekezaji 
wengine njia rahisi, salama na za kisasa za kushiriki uwekezaji.
“Huduma
 hii ya Ununuzi na Uuzaji wa Hisa kupitia NMB Mkononi, ni matokeo ya 
Ubunifu na Ushirikiano baina ya NMB na DSE, uliounganisha mifumo ya NMB 
Mkononi na Hisa Kiganjani, bunifu na kazi kubwa iliyowezeshwa kwa juhudi
 za wataalamu wa TEHAMA kutoka pande zote mbili.
“Kupitia
 huduma hii tunayozindua leo, wateja wa NMB sasa wataweza kujisajili, 
kununua, kuuza hisa na kufanya malipo kupitia akaunti za NMB, kupata 
taarifa ya thamani ya uwekezaji wao, kuona bei za hisa zilizoorodheshwa 
DSE na kujua mwenendo wa Soko la Hisa la Dar es Salaam.
 “Hili
 ni jukwaa linaloenda kuleta mapinduzi ya kweli katika ushiriki wa 
Watanzania kwenye Sekta ya Fedha, hususani Masoko ya Mitaji na Dhamana, 
lakini pia ni kielezo na uthibitisho wa dhamira ya dhati ya NMB 
kuwezesha ushirikishwaji wa kifedha kwa njia ya teknolojia,” alibainisha
 Bi. Zaipuna.
Akizindua
 huduma hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, 
Profesa Kitila Mkumbo, alizipongeza NMB na DSE kwa ubunifu wa kiwango 
cha juu, unaoenda kuisadia Serikali ya Tanzania chini ya Rais Dk. Samia 
Suluhu Hassan katika maeneo makuu manne muhimu kiuchumi.
Aliyataja
 maeneo hayo aliyosema yamo katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo, kuwa ni
 pamoja na Kuimarisha Upatikanaji wa Huduma kwa Wananchi, Kusaidia 
Kubadili Mitazamo ya Wananchi, Kuelimish Jamii Juu ya Uwekezaji na 
Kuchagiza Ushirikiano kwa Taasisi za Ndani.
“Hili
 linalofanyika hapa ni tukio zuri na la maana sana, pongezi kwa NMB na 
DSE kwa huduma hii, kwetu sisi kama Serikali, hili ni jambo kubwa, 
muhimu na la maana sana linaloenda kutusaidia katika maeneo makuu manne 
ambayo ni muhimu kwa ustawi na ukuaji wa kiuchumi.
“Moja,
 huduma hii inaenda kuimarisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi, 
Serikali na Chama Tawala tunayo Mpango wa Maendeleo wa Taifa, ambao 
unataka ifikapo mwaka 2030, huduma zote za Kiserikali zimfikie mwananchi
 popote alipo, hili mnalozindua leo, mmetutangulia sana.
“Pili,
 mnaenda kusaidia kubadili mitazamo ya wananchi walio wengi. DSE ni 
kongwe, ilipoanza ilikuwa ngumu kumwambia Mtanzania anunue Hisa, sasa 
hii huduma inaenda kubadili mitazamo ya Watanzania juu ya Hisa, kwamba 
Utajiri sio tu kuwa na magari, majumba na viwanda, bali hata Hisa ni 
Utajiri pia.
“Pia
 katika eneo la tatu, huduma hii itakuza uelewa katika suala zima la 
uwekezaji. Kwa kweli huduma hii inaenda kuchochea uwekezaji miongoni mwa
 Watanzania. Inaenda kubadili mitazamo hasi juu ya uwekezaji kwamba sio 
kwa ajili ya wageni tu, bali hata wazawa wanapaswa na wanaweza kuwekeza.
“Ili
 uchumi ukue, watu wanahitaji kuwekeza na hatua ya kwanza ni uwekaji 
akiba, ili akiba izae, ndio linapokuja suala na ununuzi wa hisa, ambao 
unafaida kubwa. Eneo la nne ni ushirikiano mliokuja nao NMB na DSE. Ni 
taasisi za ndani zenye mafanikio na mnapokuja na aina hii ya 
ushirikiano, mnachagiza wengine,” alibainisha Profesa Kitila.
Naye
 Afisa Mtendaji Mkuu wa DSE, Peter Nalitolela, alisema wao wanajisikia 
fahari sio tu kwa kuwa sehemu ya mashirikiano ya muda mrefu na NMB, bali
 ufanikishaji wa uzinduzi wa huduma bora ya kidijitali inayoenda kutanua
 wigo wa ushiriki wa Watanzania katika masuala mazima ya uwekezaji kwa 
njia ya hisa.
“NMB
 ni taasii inayoaminika, kinara wa ushirikiashaji jamii katika Huduma 
Jumuishi za Kifedha kwa Watanzania wa kadfa zote, ushirikiano huu na 
huduma hii ni uthibitisho kuwa taasisi hizi mbili zina dhamira ya dhati 
ya kukuza maslahi na ustawi wa wananchi.
“Wito
 wetu kwa umma hasa vijana, wawekeze sio kwa sababu wana pesa nyingi, 
bali kwa sababu wanahitaji kuwa na kesho iliyo bora na sisi kwa upande 
wetu, tunapambana kuondoa dhana hasi kuwa uwekezaji ni lazima uwe na 
mabilioni ya fedha, bali kwa kiasi chochote unaweza kuanza nacho 
uwekezaji,” alisema Nalitolela.
Kwa
 upande wake, Mkurugenzi wa Utafiti, Sera na Mipango wa Soko la Mitaji 
na Dhamana (CMSA), CPA Alfred Mkombo, akimwakilisha Afisa Mtendaji Mkuu 
wa CMSA, Nicodemus Mkama, aliitaja huduma hiyo kuwa ni hatua muhimu 
katika Sekta ya Fedha, hasa Soko la Mitaji na Dhamana nchini.
“Sisi
 CMSA tukiwa wasimamizi wa mitaji, tuna jukumu la kusimamia huduma zote 
za Masoko ya Mitaji, tunapongeza jitihada hizi za NMB na DSE kwa sababu 
ubunifu wao unaenda kutanua wigo wa Masoko ya Mitaji kuyafikia makundi 
yaliyoachwa nyuma katika hili.
“Hudum
 hii inayozinduliwa leo inaenda kuwa chachu ya wananchi wote kushiriki 
katika fursa za uwekezaji mijini na vijijini, hasa ukizingatia kuwa NMB 
Mkononi ina mtandao mpana unaojumuiosha wateja zaidi ya milioni 7 wa 
kada tofauti kote nchini.
“Tunazipongeza
 Bodi za NMB na DSE kwa ushirikiano huu unaozinda huduma hii iliyokidhi 
mahitaji na matakwa ya kikanuni ya CMSA,” alisisitiza Mkombo mbele ya 
waalikwa wa hafla hiyo iliyohudhuriwa pia na Msajili wa Baraza la Soko 
la Mitaji na Dhamana, Martin Kolikoli.



No comments:
Post a Comment