Saturday, July 01, 2017

UWT YAPULIZA KIPYENGA CHA KUCHUKUA FOMU KUOMBA UONGOZI, YAMUUNGA MKONO JPM KUHUSU MIMBA SHULENI

NA BASHIR NKOROMO, DAR.

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania (UWT) Amina Makilagi leo ametangaza rasmi tarehe ya Wanachama wa Jumuia hiyo kuanza kuchukua fomu kwa ajili ya kuomba ridhaa ya kugombea nafasi mbalimbali za uongozi tangu ngazi ya Kata hadi Taifa, na kusema fomu zinatolewa bure, huku akionya kuwa atakayejaribu kutumia rushwa kuomba nafasi yoyote atakatwa.

Pia ametumia ameaema UWT inaunga mkono tamko la Mwenyekiti wa CCM, Rais Dk. Magufuli alilolitoa hvi kribuni kwamba, ni marufuku kwa msichana atakayepata ujauzito akiwa shuleni katika mfumo rasmi kurudi masomoni katika mfumo huo rasmi.

Makilangi amesema, UWT inaunga mkono tamko hilo kwa sababu ndiyo maelekezo yaliyomo katika Ilaniya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020, na pia ndiyo Sera ya Serikali katika kusimamia utoaji elimu katika mfumo rasmi hapa nchini.

"Tafiti mbalimbali za Jumuia na Taasisi nyingine hapa nchini na za Kimataifa likiwemo Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataida (UNICEF), Mwanafunzi mjamzito au aliyejifungua ni vigumu kuendelea na masomo katika mfumo ambao umeandaliwa kulingana na Saikolojia ya akili ya mtoto asiye na majukumu ya malezi na ndiyo maana upomfumo uliopendekezwa na sera na ilani ya CCM kwamba anayekatiza masomo katika mfumo rasmi anaweza kuendelea katika mfumo usio rasmi, Mifumo isyo rasmi kwa ajili ya wanafunzi wa aina hiyo na wengine waliokosa masomo katika mfumo wa kawaida ni  kama MEMKWA na QT" , alisema Makilagi.

Alisema UWT inatambua na kuheshimu mapendekezo  ya tafiti hizo kuhusu watoto na pia inakubaliana na sera ya Serikali na Ilani ya CCM kuweka utaratibu bora na wenye manufaa  zaidi wa kuwazuia wajawazito na wazazi  kuendelea na masomo katika mfumo rasmi na badala yake kutengeneza mfumo mbadala wa kupata elimu kwa kuwa kufanya hivyo kumaimarisha nidhamu, na uwezo wa kitaaluma wa watoto.

"Pia UWT inawapongeza Wabunge kwa kupitisha sheria kali kwa wale watakaobainika kusababisha upatikanaji wamimba  kwa wanafunzi, kutetea na kufanikisha ndo za utotoni.  Sheria ya maraekebisho ya sheria mbalimbali namba 2 ya mwaka 2016 ilyofanyiwa marekebisho ya sheria ya elimu ya Sura 353 inaweka wazi dhamira ya Serikali ya kumlinda mtoto wa kike na kutoa onyo kali kwa wale wenye tabia za kuwarubuni na kuwasababishaia mimba zisizotarajiwa  na za utotoni",

"pamoja nakuunga mkono kauli ya Mheshimiwa Rais, pia UWT inawashauri na kuwaomba Wazazi , Walezi na Jamii kwa ujumla, kuwalinda watoto wa kike na kutoa elimu ya kutosha kuhusu masuala ya jinsia, athari za mimba za utotoni na athari za maambukizi ya magonjwa ya zinaa ukiwemo Ukimwi", alisema Makilagi.

UWT imetoa mwito kwa wasichana waliopo shuleni kujizatiti kwenye masomo na kujiepusha na vishawishi kwa kuwa dira ya Tanzania ni kuwa na Taifa lenye uwiano na fursa sawa baina ya wanaume na wanawake hivyo mwito ni kwamba wasichana wajitahidi zaidi ili kulifikia lengo la kuwa washiriki katika ujenzi wa Taifa.

UFUATAYO NI TAARIFA KAMILI KUHUSU UCHAGUZI WA KATIKA UWT





TAARIFA KWA WANACHAMA WA UWT/CCM KUPITIA VYOMBO VYA HABARI – TAREHE 30/06/2017

Mwaka 2017 ni mwaka wa Uchaguzi wa Viongozi ndani Chama Cha Mapinduzi na Jumuiya zake ambazo ni Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT), UVCCM na WAZAZI kuanzia ngazi ya Tawi hadi Taifa.

UCHAGUZI WA MATAWI
Kwa upande wa UWT Uchaguzi wa Viongozi ngazi ya Matawi, Matawi yaliyofanya Uchaguzi ni 19,927 sawa na 87% na Matawi ambayo bado kufanya Uchaguzi ni 3,118 sawa na 13%.

UCHAGUZI NGAZI YA KATA/WADI
Tarehe 04/06/2017 hadi tarehe 11/06/2017 tulitoa na kupokea fomu za wanachama walioomba kuteuliwa kuwa Viongozi wa UWT ngazi ya Kata/Wadi. Hatua inayoendelea hivi sasa ni mchakato wa vikao kwa mujibu wa Katiba ya UWT. Uchaguzi wa Kata/Wadi utafanyika kati ya tarehe 25/07/2017 hadi tarehe 28/07/2017.

UCHAGUZI NGAZI YA JIMBO
Tarehe 29/06/2017 hadi tarehe 04/07/2017 kutoa na kupokea fomu na Uchaguzi wa Viongozi wa UWT ngazi ya Jimbo unatarajiwa kufanyika kati ya tarehe 25 – 26/08/2017.


UCHAGUZI WA VIONGOZI WA WILAYA, MKOA NA TAIFA
Tarehe 02/07/2017 hadi 10/07/2017 tutaanza kutoa na kupokea fomu za wanachama wanaoomba kuteuliwa kugombea Uongozi wa Wilaya, Mkoa na Taifa.


Utaratibu wa Fomu
Fomu za kugombea Uongozi wa UWT wa Wilaya, Mkoa na Taifa zinapatikana katika Ofisi za UWT Wilaya zote na Mikoa.

Nafasi ya Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti
Fomu za kuomba kuteuliwa kugombea nafasi ya Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti UWT, zitatolewa katika Vituo vitatu.

1.       Ofisi ya UWT Makao Makuu Dodoma;
2.       Ofisi Ndogo ya UWT Dar es Salaam;
3.       Afisi Kuu ya UWT Zanzibar;

Nafasi zingine za Kitaifa

1.     Nafasi tano (5) za Halmashauri Kuu ya Taifa, nafasi tatu (3) Bara na nafasi mbili (2) Zanzibar.

2.     Nafasi kumi (10) za Baraza Kuu la UWT, nafasi tano (5) Bara nafasi tano (5) Zanzibar.

3.     Nafasi ya Uwakilishi wa UWT kwenda Jumuiya ya Vijana nafasi moja (1) na nafasi moja ya Mjumbe mmoja kuiwakilisha UWT Wazazi.

4.     Fomu za kugombea nafasi hizo zitapatikana katika Ofisi ya UWT Wilaya na Mikoa yote Tanzania Bara na Zanzibar.

5.     MIKUTANO MIKUU YA WILAYA, MIKOA NA TAIFA

(1)       Mikutano Mikuu ya UWT ngazi ya Wilaya itafanyika tarehe kati ya tarehe 21 – 22/09/2017.

(2)        Mikutano Mikuu ya UWT ngazi ya Mikoa itafanyika tarehe kati ya tarehe 25 – 26/10/2017.

(3)       Mkutano Mkuu wa UWT ngazi ya Taifa utafanyika tarehe 01 – 03/11/2017.


GHARAMA ZA FOMU
Fomu zote za kugombea Uongozi wa Tawi hadi Taifa zitatolewa bila malipo yoyote.

WITO KWA WANACHAMA
Nitumie nafasi hii kupitia Vyombo vya Habari kuhamasisha wanachama wote wa UWT/CCM wanawake kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi mbalimbali ndani ya UWT kuanzia ngazi ya Wilaya, Mkoa na Taifa ifikapo tarehe 02 – 10/07/2017.


ANGALIZO KWA WATENDAJI/VIONGOZI NA WANACHAMA
Mipango ya kutafuta fedha kwa ajili ya gharama za Mikutano ya Wilaya, Mikoa na Taifa iendelee bila kuhusisha uchukuaji wa fomu na kugombea Uongozi ndani ya UWT.

KUZINGATIA KANUNI YA UCHAGUZI
Aidha, ninasisitiza umuhimu wa kuzingatia Katiba na Kanuni ya Uchaguzi wa UWT na Kanuni ya Uchaguzi ya Maadili ya Viongozi wa CCM, lengo ni kuhakikisha Uchaguzi kwa ngazi zote unakuwa Huru na Haki kwa wanachama wote wa UWT/CCM.


RUSHWA
Uchaguzi wa 2017 tunahitaji kupata Viongozi wasiotoa Rushwa  kwa wanachama na wajumbe wasiopokea wala kutoa Rushwa. Lengo ni kupata Viongozi waadilifu na wachapa kazi na wenye moyo wa kufanya kazi za UWT bila kutanguliza maslahi yao binafsi.

KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI

 Imetolewa na:
Ndugu Amina Nassor Makillagi (MNEC, MB)
KATIBU MKUU WA UWT
  30/06/2017

No comments: