Saturday, July 15, 2017

RC MAKONDA APOKEA KOMPYUTA 50 ZENYE THAMANI YA SHILINGI MILLION 85 KUTOKA KAMPUNI YA TAMOBA



Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,Paul Makonda ( kushoto) akikabidhiwa Computer 50 zenye thamani ya shilingi Million 85 na Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Joseph Kimisha kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya TAMOBA Balozi Mstaafu Francis Mndolwa.

Baadhi ya Kompyuta hizo.Picha na Emmanuel Massaka,Globu ya jamii.


Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,Paul Makonda (wakwanza kulia) akizungumza leo jijini Dar es Salaam katika hafla ya kukabidhiwa Computer 50 zenye thamani ya shilingi Million 85 na kampuni ya ulinzi ya TAMOBA kama namna ya kuunga mkono utendaji kazi mzuri

Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya TAMOBA Balozi Mstaafu Francis Mndolwa kizungumza mchache katika hafla hiyo leo jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mh.Paul Makonda amepokea Kompyuta 50 zenye thamani ya shilingi Million 85 kutoka kwa kampuni ya ulinzi ya TAMOBA,ikiwa kama namna ya kuunga mkono utendaji kazi mzuri unaofanywa na Ofisi hiyo. 

Upatikanaji wa Computer hizo umekuja ikiwa ni sehemu ya shauku na utafutaji wa RC Makonda kwa ajili ya kuongeza tija na ufanisi katika kuwahudumia wananchi wa Dar es Salaam, ambapo itakumbukwa hivi karibuni Mh.Makonda alifanya mkutano na Watumishi wa sekta ya Ardhi wa Manispaa zote na moja ya kero kubwa iliyo bainishwa kuwasumbua wananchi ni namna ya kupata kibali cha ujenzi jambo lililomkera RC Makonda. 

Kucheleweshwa kwa huduma ya namna hii kwa wananchi huchochea utoaji Rushwa na ujenzi holela bila vibali unaosababisha Serikali kupoteza kodi ya viwanja na kodi zingine zinazohusiana na ardhi. 

Aidha amesema kuwa wananchi wamekuwa wakipata kero mbalimbali ikiwemo ile ya kupewa kibali na manispaa kisha wakaja watu wa zima moto wakakuzuia kuendelea kwa ujenzi sababu hawana taarifa, huku wakati mwingine ukimalizana na watu Zimamoto wanakuja watu wa OSHA nao wanakuzuia usiendelee na ujenzi. 

Hivyo basi badala ya hivi vitengo husika nane kuwa sehemu moja (one stop center) badala yake vimetawanyika na kuwa kero na usumbufu kwa wananchi hasa wanaotaka kufuata taratibu. 

kutokana na sababu zote hizo,Makonda ameamua kutengeneza mfumo mpya utakaomwezesha mwananchi kutokwenda kupanga foleni Manispaa yoyote ile, anapotaka kibali cha ujenzi badala yake anaweza kutuma kwa njia ya mtandao na vitengo vyote vinane vikapokea taarifa hizo kwa wakati mmoja na kumfanya kila mwenye kitengo chake kuwajibika kwa wakati pasipokuwa na kisingizio cha kupoteza taarifa za wateja, urasimu na hata lugha mbaya kwa wananchi wanaotaka huduma ya Serikali. 

Aidha mfumo huo utamwezesha Mkuu wa Mkoa kuona nani anakwamisha utendaji ili hatua za haraka zichukuliwe na mwananchi apate huduma ya haraka. 

Mfumo huu pia utamwezesha mwananchi kutuma kero inayohusu huduma ya ardhi popote alipo na ikapatiwa ufumbuzi pasipo yeye kuhangaika. 

Mkuu wa Mkoa ameahidi pia kuwapatia Pikipiki 50 watendaji wa idara ya ardhi ili waweze kufanya safari za haraka kwenda kwenye migogoro ya ardhi pale inapoibuka kabla ya madhara makubwa kutokea. 

“Nataka ifike mahali Mwananchi yoyote Yule bila kujali kipato chake akiomba kibali cha ujenzi apatiwe ndani ya mwezi mmoja,haiwezekani mtu anatuma maombi ya kupata kibali cha ujenzi anazungushwa na hatimae anakata tamaa na mwisho wa siku anajenga bila kibali na kusababisha ujenzi holela.*aliongea Makonda. 

Kwa hiyo ndio maana nikaona twende kwenye mfumo wa kupata kibali cha ujenzi ndani ya muda mfupi na serikali kupata mapato. Nikimaanisha ndani ya mwezi mmoja unatosha kupitia taarifa na kupitia maombi yao ili kamati ya mipango miji ifanye kazi yake ndani ya wakati.” alisisitiza Makonda. 

Sanjari na hayo Mkuu wa Mkoa ameushukuru uongozi wa kampuni ya TAMOBA kwa kutimiza ndoto aliyonayo na kueleza kuwa sasa ni wakati wa wataalamu kukamilisha mfumo ili wananchi waanze kupata huduma ya kisasa na aina yake. 

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya TAMOBA Balozi Mstaafu Francis Mndolwa amesema kuwa wameamua kutoa zawadi hizo kwa mkuu wa mkoa ili kusaidia kuboresha shughuli mbalimbali za maendeleo kwa wakazi wa jiji la Dar es salaam huku akionyesha kushangazwa na watanzania wanaoingiza chuki na ubinafsi katika kazi nzuri anayoifanya Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Naye Mkurugenzi wa kampuni hiyo Bwana Joseph Kimisha amesema kuwa kampuni yao inafarijika na namna ofisi ya mkuu wa mkoa inavyoshughulikia kero za wananchi kwa ufanisi na kueleza kuwa wataendelea kushirikiana na ofisi hiyo bega kwa bega

No comments: