Tuesday, July 25, 2017

TANZANIA NA KENYA ZAMALIZA TOFAUTI ZAO ZA KIBIASHARA

Tume hiyo itaongozwa na Mawaziri wa mambo ya Nje wa Tanzania na Kenya na kujumuisha mawaziri wanaohusika na masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Biashara, Fedha, Mambo ya Ndani ya Nchi, Kilimo, Uchukuzi na Utalii wa nchi hizo. 
 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania Balozi Dkt. Augustine Mahiga (kulia) akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu mazungumzo ya pamoja kuhusu mahusiano ya kibiashara kati ya Serikali ya Tanzania na Kenya mapema hii leo jijini Dar es Salaam, katikati ni Mkurugenzi, Idara ya Ushirikiano wa Kikanda toka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Balozi Innocent Shiyo na kushoto ni Kaimu Balozi wa Kenya nchini Tanzania Peter Sang.
 Mkurugenzi, Idara ya Ushirikiano wa Kikanda toka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Balozi Innocent Shiyo akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu mazungumzo ya pamoja kuhusu mahusiano ya kibiashara kati ya Serikali ya Tanzania na Kenya mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kulia ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania Balozi Dkt. Augustine Mahiga.
Baadhi ya waandishi wa habari wakimfuatilia Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania Balozi Dkt. Augustine Mahiga (hayupo pichani) wakati akitoa ufafanuzi kuhusu mazungumzo ya pamoja kuhusu mahusiano ya kibiashara kati ya Serikali ya Tanzania na Kenya mapema hii leo jijini Dar es Salaam. Picha na Eliphace Marwa -Maelezo.

Na: Paschal Dotto - MAELEZO.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Kenya zimefanya mazungumzo ya pamoja na kutatua  vikwazo vilivyokuwa vikiikabili  sekta ya biashara baina ya nchi hizo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Jijini Dar es Salaam Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Augustine Mahiga ametoa taarifa juu ya kumalizika kwa tofauti za kibiashara baina ya nchi hizo. 

 “Bidhaa za Tanzania zilizowekewa vikwazo na nchi ya Kenya ni unga wa ngano pamoja na  gesi ya kupikia (LPG). Aidha juhudi, za Serikali ya Tanzania kuona vikwazo hivyo vinaondolewa na Serikali ya Kenya kwa wakati hazikuzaa matunda, hivyo Serikali ya Tanzania nayo iliweka vikwazo kwa bidhaa za maziwa na sigara kutoka Kenya kuingia katika soko la Tanzania,” amefafanua Dkt. Mahiga.

Amesema kuwa kutokana na mahusiano mazuri ya udugu yaliyopo kati ya Tanzania na Kenya na  kwa kujali manufaa mapana ya Jumuiya ya Afrika Mashariki viongozi wakuu wa nchi hizo mbili, Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Uhuru Kenyatta na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli walikubaliana kuzungumza na kutoa vikwazo vya biashara hizo. 

Aidha, Dkt. Mahiga amesema, nchi hizo zimekubaliana kuunda Tume ya pamoja ambayo itakuwa na jukumu la kuepusha tofauti za kibiashara kati ya Tanzania na Kenya pamoja na kutolea ufumbuzi changamoto za kibiashara kati ya nchi hizo mbili pindi zinapojitokeza.

No comments: