Thursday, July 27, 2017

MH. PAUL MAKONDA AGAWA KOMPYUTA KATIKA HALMASHAURI ZA JIJI LA DAR ES SALAAM


Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Mh. Paul Mkaonda akipanga kompyuta mara baada ya kupokea kuoka Kampuni ya TAMOBA Company Ltd ya jijini Dar es salaam.

Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Mh. Paul Makonda akiangalia kompyuta mara baada ya kupokea kopmyuta hizo zilizotolewa na Kampuni ya TAMOBA Company Ltd ya jijini Dar es salaam.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,Mh.Paul Makonda leo amekabidhi kompyuta za kisasa 50 zenye thamani ya zaidi ya Shilingi Milioni 170 kwa Manispaa tano za Mkoa wa Dar es salaam pamoja na Watu wa Jiji na Mkoa kwa ajili ya kurahisisha utoaji wa vibali vya ujenzi.

Katika mgawanyo huo kila Manispaa imepatiwa kompyuta nane (8) huku Ofisi ya Jiji wakipatiwa kompyuta tano (5) na Ofisi ya Mkoa wakipatiwa kompyuta tano (5) ikiwa ni ufadhili wa kampuni ya ulinzi ya TAMOBA Company Ltd iliyomuunga Mkono RC Makonda kutokana na kuhamasika na utendaji kazi wake mzuri.

Makonda amesema Kompyuta hizo zitawekewa Mfumo wa kisasa ujulikanao kama Dar Ardhi E.System utakaoziunganisha idara zote zinazohusika na utoaji wa vibali vya ujenzi (One stop Center) ili kurahisisha Mwananchi kupata kibali cha ujenzi ndani ya muda mfupi, ambapo mwananchi atakuwa na uwezo wa kutuma maombi ya kibali cha ujenzi kwa kutumia simu ya mkononi mwake au Computer hata akiwa nyumbani na akapewa majibu yake kwa haraka.

“Kazi yangu kubwa ni kupunguza mateso,malalamiko na kero za Wananchi dhidi ya maswala ya Ardhi, na namna mbili za kupunguza ni pamoja na kuwawezesha watendaji kuwa na nyenzo na vifaa vitakavyorahisisha kufanya kazi zao kisasa zaidi kuendana na kasi ya Rais wetu Dr.John Magufuli, na pili ni kusimamia uwajibikaji kwamba kila mmoja anatekeleza majukumu yake ili Mwananchi wa Mkoa wa Dar es salaam asipate adha na mateso aliyokuwa akiyapata kwenye Sekta ya Ardhi.

Umuhimu wa kutoa vibali vya ujenzi ni jambo lisilopingika hasa katika mji huu unaokuwa kwa kasi barani Afrika” Alisema Makonda. Aidha kompyuta hizo zitawekewa Mfumo maalumu utakao kuwa ukikusanya Maoni na mapendekezo ya wananchi ambapo wananchi watakuwa na fursa ya kutuma maoni yao na kero mbalimbali zinazowakabili kwenye sekta ya Ardhi.

“Tumeishi sana kwenye mfumo wa makaratasi na mafaili, na wakati mwingine kumekuwa na changamoto ya kupotea kwa mafaili na mwananchi kupata adha ya kutoelewa nini afanye maana ataanza upya kutuma maombi, lakini si hivyo tu bali pia inafanya kazi kuwa ngumu, na mfumo huu wa kizamani unaonekana ni chanzo cha rushwa hasa pale mwananchi anapokuwa akisumbuliwa na mtumishi.

Naamini kompyuta hizi zinaenda kukata mzizi wa fitina,Wananchi kulundikana ofisini ni kero kubwa, wananchi kusumbuka kupata huduma ni kero kubwa”,alisema Makonda.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa kampuni ya TAMOBA Bwana Joseph Kimisha amesema kuwa kampuni yao itaendelea kushirikiana na ofisi ya mkoa wa Dar es salaam katika masuala mbalimbali ili kuhakikisha wanatatua kero mbalimbali zinazowakabili wananchi.

Katika Makabidhiano hayo pia makamu Mwenyekiti wa Bodi ya kampuni ya TAMOBA Bwana Otieno Igogo ameahidi kuwa watatoa jumla ya Printer 12 kwa ajili ya kusaidia utendaji kwa manispaa za jiji la Dar es salaam ambapo kila manispaa itapata Printer mbili na idara ya ardhi Mkoa kupata printer mbili pia.

No comments: