Sunday, August 01, 2010

Rais aongoza kura za maoni CCM



Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Jakaya Mrisho Kikwete ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, leo, Jumapili, Agosti Mosi, 2010, alikuwa miongoni mwa maelfu kwa maelfu ya wanachama wa CCM nchi nzima ambao wamepiga kura ya maoni ndani ya chama hicho.
Kikwete, akifuatana na Mama Salma Kikwete, amepiga kura yake ya maoni katika kijiji cha kwao cha Msoga, Wilaya ya Bagamoyo, Mkoa wa Pwani ambako ameandikishwa kama mpiga kura.
Kura ya maoni ya CCM inalenga kuchagua nani wana-CCM wanaamini anafaa kuwa mgombea nafasi ya ubunge na udiwani katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu kupitia chama hicho katika majimbo na kata mbali mbali nchini.
Mheshimiwa Kikwete amewasili kwenye Kituo cha Kupigia Kura cha Ofisi ya CCM ya tawi la Kijiji cha Msoga majira ya saa nane mchana na kujiunga na wapiga kura wengine kwa ajili ya zoezi hilo muhimu kwa Chama cha Mapinduzi.
Mara baada ya kupiga kura yake, Rais Kikwete amerejea Dar es Salaam.

No comments: