Monday, May 11, 2009

Waathirika wa mabomu wanyeshewa


ZAIDI ya kaya 300 kati ya 800 ambazo nyumba zao zilibomolewa wakati wa ajali ya milipuko ya mabomu kwenye kambi ya Mbagala ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Aprili 29, bado hazijapata mahema na hivyo kunyeshewa na mvua zinazoendelea jijini Dar es salaam.

Hali ya wananchi walioathiriwa na mabomu imekuwa si nzuri kutokana na misaada mbalimbali inayotolewa kusaidia wananchi hao ikipatikana kwa shida, ikiwa ni pamoja na chakula na mahema, ambayo inadaiwa yanatolewa pungufu kutokana na kutojua idadi halisi ya watu waliokuwa wakiishi kwenye nyumba mmoja.

Wakizungumza na Mwananchi jana eneo la maafa hayo, baadhi ya wananchi walisema hali zao kiafya sasa ziko mashakani kutokana na kuwa kwenye mazingira yanayoweza kusababisha waugue kirahisi.

“Awali tulikuwa na maisha mazuri, lakini leo hii tunaishi maisha ya shida na yenye hatari ya kukumbwa na maradhi,” alisema Suleyman Hamisi, mmoja wa wakazi wa Mbagala.

“Hii nyumba sio ya kwetu sisi ni wapangaji tu. Mwenye nyumba haishi hapa, lakini tumeamua kuingia gharama ya kuitengeneza ili tupate mahali pa kuishi, kwa sababu tangu siku ya kwanza tunanyeshewa mvua hapa nje na tuna watoto wadogo.” Imeandikwa na Jakson Odoyo.

No comments: