Thursday, July 24, 2025

*KAMISHNA KUJI AKAGUA ENEO LA KOGATENDE SERENGETI ASISITIZA MAAFISA NA ASKARI UHIFADHI KUENDELEA KUSIMAMIA SHERIA ZA HIFADHI ILI KUIMARISHA SHUGHULI ZA UTALII












Na. Philipo Hassan - Serengeti

Kamishna wa Uhifadhi, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) CPA Musa Nassoro Kuji, leo Julai 24, 2025 amefanya ukaguzi katika eneo la vivuko vya nyumbu (Kogatende) ndani ya Hifadhi ya Taifa Serengeti. Katika ukaguzi huo alielekeza Maafisa na Askari Uhifadhi kusimamia sheria ipasavyo, taratibu na miongozo mbalimbali ya Hifadhi za Taifa ili kuboresha shughuli za utalii endelevu usioharibu mazingira.

Ziara ya Kamishna Kuji ni muendelezo wa ziara zake za kikazi kukagua shughuli za maendeleo na utekelezaji wa miongozo mbalimbali iliyowekwa na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kuwa na uhifadhi endelevu ambao ndio kiini cha utalii tunaoushuhudia leo ukilipatia Shirika na Taifa mapato na fedha za kigeni ambazo zimeendelea kuchagiza katika uchumi wa Taifa letu.

Akizungumza katika ziara hiyo Kamishna Kuji alitoa maagizo kwa Maafisa na Askari Uhifadhi wanaosimamia shughuli za utalii katika Hifadhi ya Taifa Serengeti kuendelea kusimamia sheria, kanuni na taratibu zilizotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kuboresha huduma bora kwa watalii na kuwakumbusha kuzifuata ili kuondoa mkanganyiko wa mara kwa kwa mara. 

Aidha, Kamishna Kuji alisema, “Endeleeni kuchukua tahadhari na kuendelea kusimamia taratibu na sheria za hifadhi zilizowekwa kwa ajili ya kudhibiti vitengo vya uvunjifu wa sheria na miongozo ya hifadhi iliyowekwa. Kuweni imara kudhibiti matendo yanayokiuka taratibu zote za kiuhifadhi zinazofanywa na waongoza utalii wasio na weledi kama vile kushusha watalii kwenye  magari maeneo yasiyoruhusiwa ambayo ni hatari kwa watalii na waongoza watalii pia”.

Vilevile, CPA Kuji aliongeza, Simamieni na kuthibiti magari yanayotumia njia zisizo halali na rasmi  “Offroading”, kutupa taka hifadhini, mwendokasi na tabia ya kulisha wanyamapori, kwa wale watakaokengeuka na kutotii sheria na taratibu hizo, sheria ichukue mkondo wake”.  

Naye, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Stephano Msumi ambaye ni Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Serengeti akitoa taarifa ya tukio lililotokea Julai 21, 2025 ambapo picha jongefu na mnato zilionekana katika mitandao ya kijamii zikionesha watalii wakiwa wameshuka kutoka kwenye magari

katika eneo la Kogatende kivuko namba nne wameshajulikana na taratibu za adhabu zinaendelea kuchukuliwa kwa kufuata miongozo na hatutamuonea mtu wala kumfumbia mtu macho.

“ Hata hivyo, Afande Kamishna, kama hifadhi hii mama na yenye watalii wengi tumeshachukua hatua kali za kisheria kutokana na tukio hilo ambapo kampuni zote zilizohusika kuvunja sheria na taratibu kwa kushusha watalii kutoka kwenye magari yao katika maeneo ambayo hayaruhusiwi tayari zimeanza kuchukuliwa”, alisema Mhifadhi Msumi.

Kamishna Msumi aliongeza kuwa “Ni jukumu la kila mmoja wetu kwa maana ya TANAPA, waongoza watalii, madereva pamoja na wadau wote wa utalii kuhakikisha kuwa tunafuata sheria, taratibu na miongozo iliyowekwa tuwapo hifadhini ili kuendelea kutunza maliasili zetu ambazo ni chanzo cha kuleta watalii kutoka maeneo mbalimbali duniani.  Na watalii hao hukuza uchumi wa watanzania pamoja na kuchangia kuongeza pato la Taifa.

Katika kuhitimisha ziara yake Kamishna Kuji ametoa maelekezo kwa uongozi wa Kanda ya Magharibi na Hifadhi ya Taifa Serengeti kuongeza nguvu katika kuimarisha shughuli za ulinzi na usalama katika eneo la Nyatwali Wilayani Bunda ambalo Shirika limekabidhiwa kwa ajili ya kulijumuisha kuwa sehemu ya Hifadhi ya Taifa Serengeti kwa manufaa ya shughuli za uhifadhi na utalii hapa nchini. ‎

RC CHALAMILA ASIKITISHWA NA HUDUMA MBOVU YA MABASI YAENDAYO HARAKA-DART












-Asema Serikali sikivu ya Rais Dkt Samia Suluhu imesikia kilio hicho mwarobaini tayari umepatikana.

Mku wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Albert Chalamila amefanya ziara katika Kituo cha mabasi yaendayo haraka DART kilichopo Kimara mwisho Wilaya ya Ubungo na kuitaka mamlaka inayosimamia mabasi yaendayo haraka UDART kuboresha huduma zao ili kumaliza adha wanayopitia wananchi wanaotumia usafiri huo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo RC Chalamila amesema hajaridhishwa na huduma hiyo ya usafiri wa mabasi yaendayo haraka kutokana na uchache wa mabasi jambo ambalo limekua likichangia huduma mbovu na kuwasababishia watumiaji wa usafiri huo adha kubwa  kinyume na dhamira ya Rais Dkt Samia ya kutaka kuboresha huduma yq usafiri katika Jiji hilo,hivyo ameitaka UDART kuboreha huduma.

Aidha RC Chalamila ametembelea upanuzi wa barabara ya Ubungo Kimara unaosimamiwa na TANROAD ambapo ameitaka mamlaka hiyo kumsimamia mkandarasi amalize ujenzi huo kwa wakati pia ameshauri uwepo wa huduma za vyoo kwenye maeneo ya vituo vikubwa ikiwemo kimara.

Kwa upande wake Menaja upangaji ratiba na udhibiti kutoka UDART Daniel Madilu amesema tayari wameshafanya tathmini ya changamoto ya usafiri huo na kwamba tayari wameagiza mabasi miamoja kutoka China yatakayoingia nchini mwezi wa tisa mwaka huu

Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa Mhe Albert Chalamila ametembelea mamlaka ya kusimamia ujenzi wa barabara za mwendokasi DART iliyopo Ubungo maji jijini humo na kueleza mikakati ya Serikali chini ya Rais Dokta Samia kumaliza changamoto ya usafiri wa mwendokasi ambapo kwa mradi wa kimara wamepata mwekezaji mpya anaitwa Trans Dar wakati kwa barabara ya Mbagala wamepata mwekezaji anaitwa Mophat wanaotarajia kuingiza magari yao hivi karibuni

Vilevile Kwa upande wa Mtendaji Mkuu wa DART  Dkt Othman Kiamia ameahidi kushughulikia changamoto zilizopo kwa sasa ili kuondoa kero kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kusimamia uingizaji mabasi yakutosha na yenye ubora kukidhi uhitaji wa huduma hiyo ya usafiri wa mwendokasi

UCHIMBAJI NA UCHAKATAJI WA GYPSUM ITIGI WACHANGAMSHA UCHUMI, WAWEKEZAJI WATAKIWA KUJITOKEZA




Itigi, Singida – Julai 24, 2025

Uchimbaji na uchakataji wa madini ya gypsum katika Wilaya ya Itigi, mkoani Singida, umeendelea kuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi kwa wakazi wa eneo hilo, hususan vijana na wanawake, huku Serikali ikihamasisha wawekezaji kuja kuwekeza zaidi katika sekta hiyo.

Akizungumza wakati wa mafunzo kwa wachimbaji wadogo wa madini, Mkaguzi wa Madini Ujenzi na Viwandani Itigi, kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Charles Fumbuka, amesema shughuli za uchimbaji wa  gypsum zinafanyika kwa usalama na kuwanufaisha wananchi kwa kuongeza ajira na kipato.

“ Wachimbaji wameitikia wito wa Serikali wa kuongeza thamani madini yao hapo hapo mgodini badala ya kusafirisha madini ghafi. Gypsum sasa inatengeneza mikanda ya gypsum kwa ajili ya ujenzi wa nyumba pamoja na bidhaa  mbalimbali ambazo huuzwa ndani na nje ya Nchi,” amesema Fumbuka.

Aidha, amesema masoko ya bidhaa zinazotokana na gypsum yanapatikana ndani ya mkoa na yanaendelea kuimarika kadri mahitaji ya viwandani yanavyoongezeka.

Kwa upande wake, Mjiolojia kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Geofrey Mutagwa, amesema mkoa wa Singida una utajiri mkubwa wa madini na fursa lukuki kwa wawekezaji, hasa kwenye viwanda vya saruji na bidhaa za ujenzi.

“Singida ni mkoa wenye rasilimali nyingi. Tuna gypsum ya kutosha, nguvu kazi ya kutosha, na wananchi wenye ushirikiano mkubwa. Tunawakaribisha wawekezaji kuja kuwekeza, hasa kwenye viwanda vya kuchakata na kuongeza thamani ya madini yetu,” amesema Mutagwa.

Naye mchimbaji wa madini ya gypsum, Sadiki Kidira, amesema kuwa iwapo mazingira ya uchimbaji na uchakataji yataendelea kuboreshwa, Tanzania haitaendelea kuagiza gypsum kutoka nje ya nchi.

“Itigi tunaweza kabisa kuzalisha madini ya gypsum ya kutosha kwa matumizi ya ndani na hata kuuza nje. Vijana watanufaika zaidi na itapunguza changamoto za ajira na hata uvunjifu wa amani,” amesisitiza Kidira.

Mchimbaji mwingine mdogo, Moza Hilari, ameeleza namna alivyonufaika na uchimbaji huo, akisema ameweza kumsomesha mtoto wake na kujikimu kimaisha.

“Ninaishukuru Serikali kwa kutuamini na kutupa nafasi ya kushiriki kwenye Sekta ya Madini. Sasa tunaweza kujitegemea na kushiriki kikamilifu kwenye uchumi wa taifa,” amesema Moza.

Kwa ujumla, uchimbaji na uchakataji wa madini ya gypsum Itigi si tu umeleta ajira, bali pia umefungua milango ya maendeleo endelevu kwa wananchi wa Singida – na sasa ni fursa kwa wawekezaji kuchangamkia madini haya yenye thamani.

TANZANIA YAIKARIBISHA KOREA KUSINI KUSHIRIKI MIRADI MIKUBWA YA MIUNDOMBINU










Dar es Salaam, Tanzania – Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kuvutia uwekezaji wa kimataifa kupitia semina ya kimkakati iliyowakutanisha viongozi waandamizi wa serikali na wawekezaji kutoka Korea Kusini.

Semina hiyo maalum ilifanyika Julai 24, 2025 katika Hoteli ya Hyatt Regency Kilimanjaro jijini Dar es Salaam, ikiandaliwa na Taasisi ya Fedha ya Korea kwa ajili ya Ujenzi (K-Finco) kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Deogratius Ndejembi, aliwahimiza wawekezaji wa Korea kushiriki kikamilifu katika miradi ya kimkakati ya maendeleo ya ardhi, nyumba na miundombinu nchini Tanzania.

“Tunajenga taifa kwa msingi wa haki katika umiliki wa ardhi, usawa wa kijamii na ukuaji wa miji yenye mpangilio. Tunahitaji ushirikiano wenu ili kufanikisha haya,” alisema Mhe. Ndejembi.

Alisisitiza kuwa Tanzania ni nchi salama na yenye mazingira rafiki kwa uwekezaji, huku serikali ikiendelea kuboresha sera, mifumo ya kidijitali na utekelezaji wa miradi ya kimkakati kwa uwazi na ufanisi mkubwa.

Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Mhe. Togolani Mavura, aliwataka wawekezaji kuangazia fursa nyingi zilizopo nchini Tanzania katika sekta za reli, bandari, barabara, viwanja vya ndege na ujenzi wa nyumba za gharama nafuu.

“Serikali ya Tanzania, chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeweka miundombinu kama msingi wa kukuza uchumi wa viwanda. Nawaalika mshirikiane nasi kutimiza dira hii ya maendeleo,” aliongeza.

Alifafanua kuwa tayari kampuni za Korea kama Suncan Tandu na Kangar zimeonesha mfano wa ushirikiano chanya, huku taasisi na viongozi wa Korea akiwemo Madam Coll, wakionesha utayari mkubwa kusaidia kampuni hizo kuwekeza na kustawi katika soko la Tanzania.

Awali, Balozi wa Korea nchini Tanzania, Mhe. Eunju Ahn, alifungua rasmi semina hiyo kwa kusisitiza dhamira ya Serikali ya Korea kuendeleza ushirikiano wa muda mrefu na Tanzania, hasa katika sekta ya ujenzi na miundombinu. Aliahidi kuwa Korea itaendelea kuhamasisha kampuni zake kuangalia fursa mbalimbali za uwekezaji zinazopatikana nchini.

Semina hiyo ilihudhuriwa na viongozi na wadau mbalimbali wakiwemo Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Ulega, Waziri wa Miundombinu, Mhe. Naa Obeida, Rais wa K-Finco, Dr. Lee, Makamu wa Rais wa Thompson C&T, Mr. Chi, pamoja na wawakilishi wa kampuni za Korea, taasisi za kifedha na maafisa waandamizi wa Serikali ya Tanzania.

Semina hiyo ina lengo la kubadilishana uzoefu kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Korea katika sekta ya ujenzi na miundombinu. Ilifanyika sambamba na semina hiyo, na kuhudhuriwa na wataalam wa sekta ya ujenzi kutoka pande zote mbili.

Kwa ujumla, semina hii imefungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya Tanzania na Korea Kusini, na kuimarisha msingi wa maendeleo ya pamoja katika sekta ya miundombinu, makazi na uwekezaji endelevu.

#InvestInTanzania #KoreaNaTanzania #NdejembiKazini #MavuraDiplomacy #MiundombinuBora #MakaziEndelelevu #UshirikianoWaKimataifa

WAZIRI MKUU AHITIMISHA ZIARA YA BELARUS










*Aalika wenye viwanda, makampuni, wafanyabiashara kuwekeza nchini

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amehitimisha ziara yake ya kikazi ya siku mbili nchini Belarus na ametumia ziara hiyo kuwaalika wenye viwanda, makampuni na wafanyabiashara waje kuwekeza nchini.

Waziri Mkuu aliwaeleza wakuu wa taasisi aliokutana nao baadhi ya maeneo ya kimkakati kwenye uwekezaji ambayo ni elimu ya juu, afya, kilimo, TEHAMA, uendelezaji viwanda, madini na kukuza utalii. Alisema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kukuza uchumi wa Tanzania kwa kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Kwa kuzingatia azma ya Rais Samia, Waziri Mkuu amewahakikishia wenye viwanda na wamiliki wa kampuni zinazotaka kuwekeza nchini, utayari wa Serikali ya Tanzania kushirikiana nazo kwa kuzipatia misaada stahiki zitakapokuja kuwekeza nchini. Amewasihi wenye viwanda vya matreka na mitambo ya kilimo wafungue matawi nchini Tanzania ikiwemo na vituo vya kuhudumuia matrekta (mechanization centres) ili huduma za matrekta ziweze kuwa karibu na wakulima.

Vilevile, jana jioni (Jumatano, Julai 23, 2025) Waziri Mkuu alitembelea kiwanda cha kutengeneza mitambo inayotumika kuchimba madini na magari ya migodini; na pia alitembelea kiwanda cha kutengeneza vifaa vya uokoaji na kuzima moto na kusisitiza umuhimu wa kushirikiana na viwanda hivyo ili kuondoa tatizo la uhaba wa vifaa hivyo nchini.

Kampuni na taasisi alizotembelea Waziri Mkuu ni pamoja na kampuni ya kuzalisha na kusambaza dawa na vifaa tiba ya Belmedepreparaty (Republican Unitary Production Enterprises); Kiwanda cha kuzalisha matrekta na mitambo ya kilimo (Minsk Tractor Plant – OJSC); Chuo Kikuu cha Kilimo cha Belarus (BSATU), Kiwanda cha kuzalisha na kusambaza vifaa vya kielektoniki (BelOMO); kiwanda cha uzalishaji na usambazaji wa mitambo na magari makubwa ya kwenye migodi (BELAZ JSC) na kampuni ya kutengeneza na kusambaza vifaa vya uokoaji na zimamoto (POZHSNAB LLC).

Aidha, katika ziara hiyo Waziri Mkuu Majaliwa alikutana na mwenyeji wake, Bw. Alexander Turchin ambapo kwa pamoja walishuhudia utiaji saini wa hati tatu za makubaliano zilizohusu mashauriano ya kisiasa na makubaliano ya kuendeleza sekta za kilimo na elimu.

Vilevile, walishuhudia utiaji saini wa mkataba baina ya Chama cha Wafabiashara, Viwanda na Kilimo ya Tanzania (TCCIA) na Chama cha Wafabiashara wa Belarus unaolenga kukuza ushirikiano wa kibiashara baina ya nchi hizo mbili.

Waziri Mkuu Majaliwa pia alikutana na Wawakilishi wa Muungano wa Kampuni za Belarus zinazofanya biashara na mataifa ya Afrika (AFTRADE); na aliweka shada la maua kwenye mnara wa kumbukumbu ya mashujaa.

Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu aliambatana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Kazi, Uchumi na Uwekezaji wa SMZ, Bw. Shariff Ali Sharriff, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika wa Afrika Mashariki, Cosato Chumi, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Khatibu Kazungu, Naibu Katibu Mkuu Kilimo, Dkt. Stephen Nindi na Balozi wa Tanzania nchini Urusi na Belarus, Balozi Fredrick Kibuta na watendaji wengine wa Serikali.

WAZIRI MKUU AMALIZA ZIARA BELARUS, ANADI FURSA ZA UWEKEZAJI











Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa ametumia ziara yake nchini Belarus kunadi fursa za uwekezaji katika maeneo manne ya kipaumbele ya Serikali ya awamu ya sita ambayo ni kilimo, afya, madini na ulinzi & usalama.

Mhe. Waziri Mkuu katika siku mbili za ziara yake,  tarehe 22 na 23 Julai 2025 ametembelea kampuni kubwa nane zenye nguvu ya mitaji jijini Minsk na kuzihakikishia utayari wa Serikali ya Tanzania kushirikiana nazo kwa kuzipatia kila aina ya msaada zitakapokuja Tanzania kuwekeza.

Kwenye eneo la kilimo, Mhe. Waziri Mkuu alikutana na viongozi wa kampuni ya AFTRADE ambayo tayari ipo nchini na kuwasisitiza kuongeza kasi katika kuendeleza kilimo hususan kuwa na programu za kuwasaidia wakulima wadogo mitaji, utafiti na mafunzo ili kilimo  kiweze kuwa na tija, kizalishe ajira na kuongeza usalama wa chakula nchini.

Katika eneo hilo la kilimo, Waziri mkuu pia alitembelea chuo cha kilimo cha Belarus na viwanda vya matrekta na  kuvishawishi viwanda hivyo kufungua matawi nchini Tanzania. 

Kuhusu chuo cha kilimo ambacho mafunzo yake huyafanya kwa vitendo zaidi,  Waziri Mkuu aliomba Watanzania wapatiwe fursa za masomo katika chuo hicho ili waweze kuendeleza sekta ya kilimo nchini, watakapomaliza masomo yao.

Kuhusu Afya, Mhe. Waziri Mkuu alitembelea kampuni ya kuzalisha na kusambaza dawa na vifaa tiba ya Belmedepreparaty ambayo ni moja ya kampuni kubwa nchini Belarus. Kampuni hiyo inayozalisha bidhaa tofauti tofauti zaidi ya 1700 na kuuza ndani na nje ya nchi katika mataifa zaidi ya 24, iliridhia maombi ya Mhe. Waziri Mkuu na kuahidi kufanya ziara nchini Tanzania kuangalia fursa za uwekezaji.

Mhe. Waziri Mkuu alisema Belmedepreparaty ni kampuni sahihi kuja kuwekeza nchini kutokana na kutumia teknolojia ya kisasa ya kuzalisha bidhaa zenye ubora na viwango vya kimataifa.

Kwa upande wa sekta ya madini, Waziri Mkuu alitembelea kiwanda cha kutengeneza mitambo inayotumika kuchimba madini migodini na kukishawishi kiwanda hicho kuja kuwekeza nchini Tanzania. 

Kuhusu suala la Ulinzi na Usalama, Mhe. Waziri Mkuu alitembelea kiwanda cha kutengeneza vifaa vya ukoaji na kuzima moto na kusisitiza umuhimu wa kushirikiana na kiwanda hicho ili kuondoa tatizo la uhaba wa vifaa hivyo nchini.

Waziri Mkuu amemaliza ziara yake na aliondoka Julai 24, 2025 kurejea nyumbani.

*KAMISHNA KUJI AKAGUA ENEO LA KOGATENDE SERENGETI ASISITIZA MAAFISA NA ASKARI UHIFADHI KUENDELEA KUSIMAMIA SHERIA ZA HIFADHI ILI KUIMARISHA SHUGHULI ZA UTALII

Na. Philipo Hassan - Serengeti Kamishna wa Uhifadhi, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) CPA Musa Nassoro Kuji, leo Julai 24, 2025...