Saturday, July 05, 2025

WANANCHI 216 WAKABIDHIWA HATI MILIKI WILAYANI MASWA










Ofisi ya Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Simiyu, leo imeendesha zoezi la kugawa jumla ya hati miliki 216 kwa wananchi wa Wilaya ya Maswa. Tukio hilo limekuwa sehemu ya mkakati endelevu wa Serikali katika kuhakikisha kila mwananchi anamiliki ardhi kisheria, kwa usalama na kwa manufaa ya sasa na baadaye.

Zoezi hilo pia linaendelea kuwa chachu ya kuhamasisha umiliki halali wa ardhi, sambamba na kuimarisha usimamizi wa rasilimali hiyo muhimu kwa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla. Wananchi waliopokea hati hizo wameelezea furaha yao na kueleza kuwa sasa wana uhakika wa kuwekeza kwa uhuru na kuondokana na migogoro ya ardhi.

RC MTANDA ATAKA ELIMU YA KUTOSHA KUHUSU MFUMO WA e-ARDHI




Mkuu wa mkoa wa Mwanza Said Mtanda amewataka wataalamu wa sekta ya ardhi kutoa elimu ya kutosha kuhusu matumizi ya mfumo wa  e-Ardhi Kwa kutumia njia mbalimbali kama vile kuandaa mabonanza au matamasha.

"Tuifanye kazi kama ibada Kwa kuhakikisha tunawahi na kufanya kwa weledi na ufanisi wakati Wote".amesema.

Mkuu huyo wa mkoa wa Mwanza ametoa kauli hiyo tarehe 3 Juni 2025 katika kikao cha watumishi wote wa sekta ya ardhi kutathmini hali ya utekelezaji majukumu ya sekta Kwa mwaka 2024/25 na kujipanga namna Bora na yenye ufanisi zaidi ya kutekeleza majukum ya mwaka 2025/26.

Aidha, amewataka wataalam wa sekta ya ardhi katika mkoa huo kuwa wabunifu katika Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi ili kuongeza kasi ya ufanisi wa sekta.

Pia amewataka wataaalam hao kuacha kuzalisha migogoro mipya ya ardhi na kuhakikisha migogoro iliyopo inashughulikiwa.

"Tuendelee utaratibu wa Kliniki za Ardhi kwenye Wilaya na ngazi ya mkoa, tuongeze kasi ya ukusanyaji maduhuli Kwa kuwafuatilia wadaiwa wa Kodi ya Pango la ardhi Kila mara na kuwachukulia hatua stahiki za kisheria" amesema.

Kwa upande wake Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Mwanza Wilson Luge amesema, ofisi yake katika kipindi cha mwaka mmoja wa 2024/2025 imesajili jumla ya Hatimilki za kimila (CCRO) 1,642  sawa na 8.2%.

Kwa mujibu wa Luge, jumla ya Hatimilki 4,665 sawa 10% zimetolewa huku viwanja 9,607  sawa na 33.79 vikiwa vimepimwa na michoro Tp 176 sawa na 176% imeandaliwa.

Akigeukia ulipaji kodi ya pango la ardhi katika mkoa wake,  Bw. Luge alisema, ofisi yake imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni  8.5 sawa na 42% .

Friday, July 04, 2025

WAZIRI RIDHIWANI KIKWETE AVUTIWA NA KAZI ZA BODI YA ITHIBATI YA WAANDISHI WA HABARI (JAB) KATIKA MAONESHO YA SABASABA




Dar es Salaam, Julai 04, 2025 — Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu, Mhe. Ridhiwani Kikwete, leo ametembelea banda la Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) lililopo katika Kijiji cha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kwenye Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Nyerere.

Katika ziara hiyo, Mhe. Ridhiwani alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Bodi hiyo ikiwa ni pamoja na usajili na utoaji wa ithibati kwa waandishi wa habari nchini, elimu kuhusu maadili ya uandishi wa habari, pamoja na mikakati ya kuboresha taaluma hiyo kwa manufaa ya umma.

Akipokea maelezo kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa JAB, Mhe. Waziri alielezwa kuwa Bodi hiyo imeendelea kupokea maombi ya ithibati kutoka kwa waandishi mbalimbali wa habari kote nchini, huku ikisisitiza umuhimu wa uandishi wa habari wenye weledi, uadilifu na uwajibikaji.

Mhe. Ridhiwani Kikwete alipongeza kazi kubwa inayofanywa na JAB katika kuhakikisha uandishi wa habari nchini unaendeshwa kitaaluma, huku akihimiza waandishi wa habari – hususan vijana – kujitokeza kwa wingi kupata ithibati ili kutambulika rasmi na kufanya kazi kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizowekwa.

"Naipongeza JAB kwa kazi nzuri. Nawasihi waandishi wa habari, hasa vijana, kuchangamkia fursa ya kupata ithibati. Hii inaleta heshima kwa taaluma yenu, lakini pia ni hatua muhimu ya kujenga uwajibikaji na weledi katika kazi zenu za kila siku," alisema Mhe. Ridhiwani.

Aidha, Mhe. Waziri alitumia fursa hiyo kuzungumza na baadhi ya waandishi waliokuwepo katika banda hilo, ambapo alieleza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki kwa waandishi wa habari na kuimarisha ushirikiano baina ya wadau wa sekta ya habari na taasisi za serikali.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi hiyo alimshukuru Mhe. Ridhiwani kwa kutembelea banda lao na kuonesha kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Bodi katika kusimamia taaluma ya habari. Alisema ujio wa Waziri ni kichocheo kikubwa kwa Bodi kuendelea na jitihada zake za kuimarisha weledi na maadili ya uandishi nchini.

Matukio mbalimbali yaliambatana na maonesho ya vitabu vya mwongozo wa Ithibati, nyaraka za kisheria, pamoja na video fupi zinazoonesha kazi za JAB na miongozo ya utoaji ithibati kwa waandishi wa habari.

TANZANIA YAENDELEA KUTANGAZA NA KUKUZA KISWAHILI NA UTAMADUNI WAKE KIMATAIFA






Na mwandishi wetu, Osaka, Japan

Lugha ya kiswahili na utamaduni wa mtanzania vimeendelea kuwa kivutio kikubwa kwa wageni mbalimbali wa kimataifa waliotembelea banda la Tanzania katika Wiki ya utamaduni na Kiswahili inayoendelea kwenye maonesho ya biashara ya dunia (Expo 2025) yanayofanyika Osaka.

Viongozi waandamizi wa mataifa mbalimbali, wametembelea banda hilo ikiwemo Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi la Japani, Bw. Koichiro Gemba, Mfalme wa Lesotho, Mhe. Letsie III na Mhe. Prudence Sebahizi, Waziri wa Biashara na Viwanda wa Rwanda. 

Viongozi hao wameonesha kuvutiwa kwa kiasi kikubwa na lugha ya Kiswahili na Utamaduni kupata nafasi katika Maonesho hayo ya Dunia yenye hadhi kubwa. 

Akizungumza wakati alipotembelea banda hilo Mhe. Sebahizi alieleza kufurahishwa na namna lugha ya Kiswahili ilivyopewa nafasi katika maonesho hayo ya dunia na kudai Kiswahili kinaweza kuwa nyenzo muhimu katika kuwaunganisha Waafrika katika juhudi zao za kujiletea maendeleo ya kiuchumi na kijamii. 

Akizungumza na maofisa wa taasisi za Tanzania zinazoshiriki katika maonesho hayo, ikiwemo Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) na Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), Mhe. Sebahizi amesema kuwa lugha ya kiswahili inakidhi kwa matumizi miongoni mwa Waafrika

Viongozi hao pia walipata fursa ya kujionea vivutio vya kitamaduni kama vile mavazi ya jadi, sanaa za mikono, bidhaa za kipekee kama kahawa ya Kilimanjaro, Madini ya Tanzanite, viungo vya asili vya Zanzibar na machapisho mbalimbali ya Kiswahili huku Kamusi Kuu ya Kiswahili kutoka BAKITA ikiwavutia wengi.

Ushiriki huu wa Tanzania katika maonesho hayo ambayo kwa upande wa Tanzania yanaratibiwa na TanTrade, ni sehemu ya juhudi endelevu za kuitangaza lugha ya Kiswahili kama urithi wa Afrika na dunia, sambamba na utamaduni wake tajiri, ili kuimarisha uhusiano ya kimataifa na kuvutia wawekezaji, watalii na washirika wa maendeleo kupitia nguvu ya lugha na utambulisho wa kitaifa.

Kilele cha wiki hii ya Utamaduni na Kiswahili katika maonesho hayo kitafanyika tarehe 7 mwezi wa 7, ambapo kwa kawaida huwa ni Maadhimisho ya Siku Kiswahili Duniani (MASIKIDU), ambapo kutakuwa na utoaji wa vyeti na tuzo mbalimbali kwa wadau walioshiriki kwa hali na mali kukikuza, kukieneza, na kukiendeleza Kiswahili nchini Japani.

𝗪𝗔𝗡𝗔𝗡𝗖𝗛𝗜 𝗪𝗔𝗙𝗨𝗥𝗔𝗛𝗜𝗦𝗛𝗪𝗔 𝗡𝗔 𝗨𝗣𝗔𝗧𝗜𝗞𝗔𝗡𝗔𝗝𝗜 𝗪𝗔 𝗠𝗕𝗘𝗚𝗨 𝗕𝗢𝗥𝗔 𝗭𝗔 𝗠𝗜𝗧𝗜









Dar es Salaam. Wananchi wameeleza kufurahishwa na juhudi za Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika kuhakikisha upatikanaji wa mbegu bora za miti na elimu ya uhifadhi, katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.

Ikiwa leo ni siku ya saba ya maonesho hayo, mamia ya wananchi wameendelea kutembelea banda la Wizara ya Maliasili na Utalii, hususan katika eneo la TFS, ili kupata mafunzo kuhusu uhifadhi wa misitu na ufugaji wa nyuki.

Baadhi ya wananchi wamesema kuwa wamevutiwa na namna TFS inavyowaelimisha kuhusu upandaji wa miti bora kulingana na aina ya udongo na hali ya hewa ya maeneo mbalimbali nchini

“Nimejionea miche mizuri kabisa na nimenunua mbegu na miche. Hii si mara ya kwanza kununua hapa. Kwa kweli TFS wanafanya kazi nzuri katika kuhakikisha wananchi wanapata mbegu bora za miti na elimu ya kupanda miti inayofaa kwa maeneo tofauti,” alisema Ndg. Tabu Ramadhan, mmoja wa wananchi waliotembelea banda hilo.

Naye Ndg. Geofrey Mati alieleza kuwa mafunzo aliyoyapata yameongeza uelewa wake kuhusu upandaji miti.

“Nimepewa elimu nzuri sana ya upandaji miti katika eneo ninaloishi. Wamenieleza kuwa si kila mti unapandwa popote; inategemea na udongo na hali ya hewa ya eneo husika. Hapo awali sikuwa nafahamu, lakini sasa nimepata uelewa mkubwa sana,” alisema Mati.

Mbali na elimu ya miche na mbegu bora, wananchi pia wamepata fursa ya kujionea shughuli za ufugaji nyuki, zikiwemo maandalizi ya manzuki, uvunaji na uchakataji wa mazao ya nyuki.

Aidha, TFS imewahimiza wananchi kuendelea kutembelea banda lao katika maonesho hayo ili kupata elimu zaidi juu ya uhifadhi wa misitu, ufugaji wa nyuki, pamoja na kupata ofa maalumu za kutembelea vivutio vya utalii wa ikolojia vinavyosimamiwa na wakala huo.

Maonesho ya Sabasaba 2025 yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13, yakishirikisha washiriki kutoka ndani na nje ya nchi. 

@treeseedstz

WANANCHI 216 WAKABIDHIWA HATI MILIKI WILAYANI MASWA

Ofisi ya Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Simiyu, leo imeendesha zoezi la kugawa jumla ya hati miliki 216 kwa wananchi wa Wilaya ya Maswa....