Friday, January 31, 2014

UBALOZI WA CHINA NCHINI WASAIDIA WAHANGA WA MAFURIKO WA MOROGORO

Mkurugenzi  wa Idara ya  Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Luteni Jenerali Sylivester Rioba akipokea msaada huo kwa niaba ya serikali kutoka kwa  Balozi wa Mhe. Lu Youqin.
……………………………………………………………………………………………………..
Na Eliphace Marwa-Maelezo
Ubalozi wa China nchini Tanzania kwa kushirikiana na makampuni ya watu wa China nchini   wametoa msaada wa vitu mbalimbali kwa waathirika wa mafuriko mkoani Morogoro toka kwa  Mhe. Lu Youqing ,vyenye thamani ya sh. milioni 30.
Msaada huo  umetolewa  na  Balozi wa China nchini Tanzania Mhe.Lu Youqing na ulikabidhiwa kwaMkurugenzi  wa Idara ya  Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Luteni Jenerali Sylivester Rioba akipokea msaada huo kwa niaba ya serikali amesema kuwa anaishukuru Serikali ya China kwani imekuwa mstari wa mbele  pale Tanzania inapopata maafa mbalimbali.
Aidha Luteni Jenerali Rioba aliongeza kuwa  mafuriko hayo ya aina yake hayajawi kutokea yalianzia milima ya Kilosa na Mvomero na kupelekea kufurika kwa mto Mkundi.
“Mheshimiwa Balozi mvua hizi zilikuwa kubwa  ambazo hazijawahi kutokea wilayani Mvomero na kupelekea kuharibu daraja la Dumila ambalo ndiyo  kiunganishi cha Mkoa wa Morogoro na Dodoma,” alisema Luteni Jenerali Rioba.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Mhe.Antony Mtaka akiongea kwa niaba ya  Mkuu wa Mkoa wa Morogoro  amesema kuwa mamia ya nyumba ikijumuisha madarasa, majengo ya mahakama ya mwanzo, mashamba na barabara zimeharibiwa vibaya na mafuriko hayo.
“Kwa niaba ya Serikali napenda kushukuru Serikali ya China  kupitia Mhe. Balozi Lu kwa msaada huu na ningependa kuahidi kuwa msaada huu utawafikia walengwa kama ilivyokusudiwa, ”alisema Mhe. Mtaka.
Kwa upande wake Balozi wa china ametoa pole kwa waathirika wa mafuriko na kusema kuwa watu wa Jamhuri ya China wako pamoja nao katika kipindi hiki kigumu.
“China na Tanzania ni marafiki wa muda mrefu hivyo kampuni ya ujenzi ya CCECC ilichukua hatua za haraka katika kushiriki ujenzi wa daraja hilo kwa kushirikiana bega kwa bega  na ndugu zao Watanzania kwa kufanya kazi usiku na mchana na kumaliza ujenzi huo kwa muda wa siku mbili,” alisema Balozi Youqing.
Ubalozi wa China kwa kushirikiana na makampuni ya China nchini umetoa vitu mbalimbali ikiwemo Chakula, mashuka, madawa na maturubahi ikiwa ni sehemu ya mchango wao kwa waathirika hao wa mafuriko mkoani Morogoro.

No comments: