Friday, October 24, 2008

Shirikisho Afrika




UAMUZI wa wakuu wa nchi 26 za Afrika kuunganisha soko la pamoja katika nchi hizo, umeondoa ndoto ya kuanzisha shirikisho la kisiasa la Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hatua hiyo inatokana na mpango wa wakuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na Jumuiya ya Soko la Pamoja kwa Nchi za Kusini na Mashariki mwa Afrika (Comesa), kuanzisha mchakato huo ambao utameza mambo ya jumuiya hizo.

Shirikisho la Afrika Mashariki linahusisha nchi za Tanzania, Uganda, Kenya, Burundi na Rwanda na tayari nchi hizo zilishapiga hatua kubwa kuelekea kuwa kitu kimoja, huku mabilioni ya fedha yakiwa yametumika katika mchakato huo, ambao pia ulihusisha kutafuta maoni kwa wananchi.

Baadhi ya taasisi za Shirikisho la Afrika Mashariki zilishaanza kufanya kazi, ikiwemo sekretarieti inayoratibu shughuli zote za shirikisho hilo, bunge, mahakama huku mamilioni mengine yakitumika kujenga ofisi za makao makuu mjini Arusha, lakini uamuzi uliofanywa juzi unaweza kuwa mwanzo za kuzorota kwa harakati hizo.

Akijibu swali kutoka gazeti hili kuhusu uamuzi huo wakuu wa nchi 26 uliofanywa nchini Uganda, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernad Membe alisema ni dhahiri hapo baadaye kama mchakato utakwenda kama ulivyo, shirikisho hilo halitakuwepo.

No comments: