Tuesday, October 14, 2008

Mwisho wa kumtaja Mkuchika leo

LEO itakuwa mwisho kwa jina la Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Kapteni George Mkuchika, kutajwa katika vyombo vya habari baada ya Wahariri kuamua kutoandika au kutangaza habari zake katika vyombo vya habari.

Wahariri wa vyombo vya habari nchini, wameamua kwa pamoja kususia kuandika habari zote zinazomuhusu waziri huyo kupinga hatua yake ya kulifungia gazeti la MwanaHalisi kutochapishwa kwa miezi mitatu..

Kauli hiyo ya pamoja, ilitolewa jana na Jukwaa la Wahariri nchini, katika mkutano wao uliofanyika katika Hoteli ya New Africa jijini Dar es Salaam na kutoa maamuzi yao juu ya kufungiwa kwa gazeti hilo bila ya kupewa muda wa kutosha kujitetea kuhusiana na walichokiandika.

Pamoja na uamuzi wa kutoandika habari za waziri huyo, pia wahariri hao wameamua, kufungua kesi ya kupinga kufungiwa kwa gazeti hilo, na kufanya maandamano siku ya Ijumaa kwa lengo la kuelezea kero zao na kuziandikia barua nchi wafadhili kuelezea jinsi Tanzania inavyoanza kuingilia uhuru wa vyombo vya habari.
Na Festo Polea

No comments: