Wednesday, July 08, 2009

Mtoto wa Michael Jackson aliza wengi


Mwili wa mfalme wa muziki wa Pop Michael Jackson ukiwa kwenye jeneza lenye kuta za dhahabu uliagwa na maelfu ya washabiki wake waliohudhuria kwenye ukumbi wa Staples Center wakati mamilioni ya washabiki wake wengi duniani walifuatilia tukio hilo kwenye luninga na internet. Picha za hafla ya kuuaga mwili wa Michael Jackson mwisho wa habari hii.
Akiongea kwa mara ya kwanza mbele ya halaiki ya watu, mtoto wa kike wa Michael Jackson , Paris, mwenye umri wa miaka 11 aliwaliza watu wengi pale alipopewa nafasi ya kuongea.

"Tangia nilipozaliwa, baba amekuwa ni baba bora ambaye hana mfano, ningependa kusema kwamba nampenda sana" alisema Paris na kuanza kuangua kilio huku akikumbatiwa na shangazi yake Janet Jackson.

Awali akiongea katika hafla hiyo ya kuuaga mwili wa Michael Jackson, mchungaji Al Sharpton aliwaambia watoto watatu wa Michael Jackson kuwa wasijali habari mbaya zinazosambazwa juu ya baba yao.

"Nataka watoto watatu wa Michael Jackson wajue kwamba baba yao alikuwa si mtu wa ajabu kama anavyoandikwa" alisema Sharpton na kuongeza "Vitu vya ajabu ni vile ambavyo baba yenu ilimbidi avikabili".

Safari ya Michael Jackson ilianzia kwenye nyumba ya kuhifadhia maiti ya Forest Lawn ambapo familia yake na ndugu zake walikusanyika kwa maombi na kulichukua jeneza lake tayari kwa safari ya kuelekea kwenye ukumbi wa Staples Center ambako watu 20,000 walikuwa wakisubiri.

Baada ya hapo jeneza la dhahabu la Michael Jackson lilipandishwa kwenye gari la kifahari huku helikopta 20 za waandishi wa habari zikifuatilia tukio kutoka angani.

Msafara wa magari mengi ya kifahari ulianza kuelekea kwenye ukumbi wa Staples Center ambako familia , marafiki na watu maarufu walijumuika na washabiki wa Michael Jackson ambao walibahatika kushinda bahati nasibu ya tiketi za kuhudhuria hafla hiyo.

No comments: