Friday, March 03, 2017

Puma Energy yazindua kampeni ya Usalama barabarani


Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Naibu Kamishna wa Polisi Mohamed Mpinga (Kulia) akikabidhi picha yenye mahudhui ya usalama barabarani iliyochorwa na mwanafunzi wa shule ya Msingi Bunge ya jijini Dar es Salaam, Veronica Innocent (wa kwanza kushoto) kwa mwalimu wake Bi Amina Kayeke wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa kampeni maalumu ya Usalama barabarani kwa wanafunzi wa shule za msingi inayoendeshwa na kampuni ya Puma Energy .Mwanafunzi huyo aliibuka mshindi wa kwanza kitaifa kwenye shindano la kuchora picha zenye maudhui ya usalama barabarani katika kampeni hiyo kwa mwaka jana. Wanaoshuhudia ni pamoja na Meneja Mkuu wa kampuni hiyo hapa nchini Bw Philippe Corsaletti (wa pili kulia ) na Naibu Mkurugenzi wa taasisi inayoshughulikia masuala ya usalama barabarani ya Amend, Bw Tom Bishop.
Meneja Mkuu wa kampuni ya Puma Energy hapa nchini Bw Philippe Corsaletti (kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na na mwanafunzi wa shule ya Msingi Bunge ya jijini Dar es Salaam, Veronica Innocent alieibuka mshindi wa kwanza kitaifa kwenye shindano la kuchora picha zenye maudhui ya usalama barabarani katika kampeni ya Usalama barabarani inayoendeshwa na kampuni hiyo.
Meneja Mkuu wa kampuni ya Puma Energy hapa nchini Bw Philippe Corsaletti akizungumza kwenye hafla hiyo. 
Mwalimu Amina Kayeke kutoka shule ya Msingi Bunge ya jijini Dar akizungumza kuhusu changamoto wanazozikabili wanafunzi wake katika masuala ya usalama barabarani. Pembeni ni mwanafunzi wa shule hiyo, Veronica Innocent alieibuka mshindi wa kwanza kitaifa kwenye shindano la kuchora picha zenye maudhui ya usalama barabarani katika kampeni ya Usalama barabarani inayoendeshwa na kampuni ya Puma Energy.
Veronica Innocent alieibuka mshindi wa kwanza kitaifa kwenye shindano la kuchora picha zenye maudhui ya usalama barabarani katika kampeni ya Usalama barabarani inayoendeshwa na kampuni ya Puma Energy akizungumza mbele Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Naibu Kamishna wa Polisi Mohamed Mpinga, Uongozi wa Puma Energy, maofisa wa serikali pamoja na walimu kutoka shule mbalimbali za jijini Dar es Salaam waliohudhuria warsha hiyo.
Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Naibu Kamishna wa Polisi Mohamed Mpinga akizungumza kwenye ufunguzi wa kampeni hiyo. Kwa mujibu wa Kamanda tangu kuanzishwa kwake kampeni hiyo imeweza kupunguza vifo vitokananvyo na ajali barabarani kwa asilimia 50 katika shule ambazo kampeni hiyo imeweza kufika
Makabidhiano ya picha yakiendelea. 

Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Naibu Kamishna wa Polisi Mohamed Mpinga (Katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Uongozi wa Puma Energy, taasisi inayoshughulikia masuala ya usalama barabarani ya Amend, maofisa wa serikali pamoja na walimu kutoka shule mbalimbali za jijini Dar es Salaam waliohudhuria warsha hiyo. 

KAMPUNI ya Puma Energy Tanzania leo wamezindua kampeni maalumu ya Usalama barabarani kwa wanafunzi wa shule za msingi, ikiwa ni mkakati wa kampuni hiyo kueneza elimu hiyo muhimu kuanzia ngazi ya chini. 

Ikiwa ni muendelezo tu tangu ianzishwe rasmi mwaka 2013, hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo imefanyika jijini Dar es Salaam na kuhudhuliwa na Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Naibu Kamishna wa Polisi Mohamed Mpinga, maofisa wa serikali pamoja na walimu. 

Utolewaji wa elimu kwa wanafunzi kuhusu usalama barabarani pamoja na matumizi ya sanaa hususani mashindano ya kuchora dhana tofauti zinazohusiana na mada kuu ya usalama barabarani vilitajwa kuwa ni ni miongoni mwa agenda muhimu katika kampeni hiyo. 

“Lengo la kuhusisha wanafunzi katika kampeni hii ni kutokana na imani tuliyonayo kwamba elimu kuhusu usalama barabarani inatakiwa kujengwa miongoni mwetu tangu tukiwa katika umri mdogo kabisa. Kwa kufanya hivyo tutakua tukiwa na elimu ya kutosha kuhusu suala hili,’’ alibainisha Meneja Mkuu wa kampuni hiyo hapa nchini Bw Philippe Corsaletti. 

Kwa mujibu wa Bw Corsaletti tangu kuanzishwa kwa kampeni hiyo mwaka 2013, jumla ya shule 33 zenye jumla ya wanafunzi 39,000 wamefundishwa mafunzo hayo hapa nchini huku ripoti ya ukaguzi kuhusu elimu hiyo ikionyesha kupungua kwa ajali maeneo ya shule hizo. 

Akiizungumzia kampeni hiyo, Naibu Mkurugenzi wa taasisi inayoshughulikia masuala ya usalama barabarani ya Amend, Bw Tom Bishop alisema kampeni ya mwaka huu itahusisha shule 10 za Dar es Salaam na 3 za mkoa wa Kilimanjaro. 

Alizitaja shule hizo kuwa ni pamoja na shule za msingi Diamond na Olympio zilizopo wilaya ya Ilala, Mkwawa na Kigogo zilizopo wilaya ya Kinondoni, Buza na Amani zilizopo wilaya ya Temeke, Mbezi na Amani zilizopo wilaya ya Ubungo pamoja na Kibugumo na Kibada zilizopo wilaya ya Kigamboni. 

Kupitia kampeni hiyo, kampuni ya Puma imepanga kuendesha mafunzo hayo pamoja na kuchora tena michoro ya ukutani kuhusu usalama barabarani kwa shule 12 ambazo tayari zimekwisha pitia mafunzo hayo, kuweka miundombinu ya usalama barabarani kwa shule za msingi Ungindoni, pamoja na kuchora michoro kwenye kuta za shule za msingi Oysterbay, Mburahati na Bryson ili kutoa elimu hiyo kwa madereva. 

“Kwa upande wa shule za mkoa wa Kilimanjaro tutazitambua baadae baada ya kumaliza hizi za mkoa wa Dar es Salaam.Lengo letu ni kuzifikia shule zote hapa nchini,’’ aliongeza Bw Bishop. 

Akizungumza kwenye uzinduzi huo, Kamanda Mpinga alisema tangu kuanzishwa kwake imeweza kupunguza vifo vitokananvyo na ajali barabarani kwa asilimia 50 katika shule ambazo kampeni hiyo imeweza kufika. 

“ Ndio maana natoa wito kwa wadau wengi zaidi wajitokeze kuunga mkono kampeni za namna hii kwasababu inahitajika kufika nchi nzima ili haya mafanikio tunayoyaona kwenye kampeni hii yaakisi nchi nzima,’’ alisema. 

Naye, Afisa Elimu Vifaa, Takwimu Wilaya ya Kinondoni Bi Martha Kayombo alitoa wito kwa walimu nchini kuhakikisha kwamba wanasimamia suala la usalama barabarani popote watakapokuwepo hususani maeneo ya barabarani ili kuwasaidia watoto wadogo.

No comments: