Friday, June 13, 2014

SHIRIKA LA NYUMBA LA TAIFA (NHC) LILIPOTIA SAINI UJENZI WA NYUMBA 14 KWA MANISPAA YA BOSOKELO, TUKIO LILILOFANYIKA DODOMA, JUNI 10, 2014

 
 Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpya Busokelo, Meckson Moses Mwakipunga(katikati) akibadilishana mkataba na Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Saidi Mderu (kushoto) baada ya kuusaini katika hafla iliyofanyika Hoteli ya New Dodoma.Kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Bwana Felix Maagi. Mawaziri walishuhudia tukio hilo.
 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, (Kazi Maalum) ambaye pia ni Mbunge Rungwe Mashariki, Profesa Mark Mwandosya (wa pili kulia) akisalimiana na Mbunge wa Jimbo la Rungwe Magharibi, Mhe Profesa David Mwakyusa.  
 Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mkoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) pia Mbunge wa Siha, Mhe. Aggrey Mwanri akipongeza baada ya kuongea ktk hafla hiyo.  
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Bwana Felix Maagi akitoa yake machache katika hafla hiyo.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpya Busokelo, Meckson Moses Mwakipunga akiongea baada ya kusaini mkataba katika hafla iliyofanyika Hoteli ya New Dodoma.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Bwana Felix Maagi (kulia), Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpya Busokelo, Meckson Moses Mwakipunga(kushoto) na Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Saidi Mderu wakisaini mkataba wa ujenzi wa nyumba 14 za bei nafuu kwa shilingi milioni 500 katika hafla iliyofanyika Hoteli ya New Dodoma jana. Wanaoshuhudia (kulia) ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, (Kazi Maalum), Profesa Mark Mwandosya na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mkoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Aggrey Mwanri.

Baadhi ya Wabunge wa Mkoa wa Mbeya wakiongozwa na Katibu wa Wabunge wa Mkoa huo Dkt Mary Mwanjelwa (kulia) wakishuhudia hafla ya utiaji saini wa mkataba huo.

Kama tunavyofahamu mahitaji ya nyumba bora nchini, hususan Wilaya mpya kama hii ni makubwa sana kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watu hususan watumishi wa umma wanaokuja kutumikia Taifa katika Wilaya hizi.

Mradi huu unatarajiwa kuanza Julai 2014, na unategemewa kukamilika Agosti 2015 ikiwa ni muda wa takribani mwaka. Mradi huu una nyumba za gharama nafuu 14 tu zitakazouzwa kwa Halmashauri ya wilaya ya Busokelo, zikiwa ni nyumba za vyumba vitatu vya kulala, sebule, jiko la kisasa na maegesho ya magari ya ziada.

Mradi huu utagharimu kiasi cha shilingi 1,112,109,880 ikiwa ni wastani wa shilingi milioni 79  kwa kila nyumba.

Ujenzi wa nyumba unahitaji ardhi ya kutosha. Hivi sasa tumeshakuwa na ardhi ya akiba yenye ukubwa wa ekari 1,372.1 katika maeneo mbalimbali nchini ambayo Shirika limelipia ardhi hiyo kwa gharama ya shilingi bilioni 34.3.

Mradi wa ujenzi wa nyumba za gharama nafuu ulibuniwa na Shirika kwa lengo la kuwapatia makazi bora wakazi walioko katika Halmashauri za Miji na Wilaya, hususan Wilaya mpya. Hivi sasa ipo miradi mbalimbali ya ujenzi wa nyumba za gharama nafuu inayotekelezwa na Shirika katika miji mbalimbali hapa nchini.
Katika mwaka huu wa fedha, Shirika limeanza utekelezaji wa ujenzi wa nyumba 578 za gharama nafuu katika maeneo 15 nchini, zenye jumla ya gharama ya shilingi bilioni 24. Nyumba hizo zinajengwa katika Wilaya za Manyoni, Mkinga, Mvomero, Kongwa, Uyui, Manyara na Monduli. Maeneo mengine zinakojengwa nyumba hizo ni pamoja na Mkuzo, Mlole, Mtanda, Mrara, Bombambili, Unyankumi, na Ilembo, Isikizya.

Lengo ni kuhakikisha kuwa zaidi ya nyumba 5000 za gharama nafuu zinajengwa katika Halmashauri mbalimbali za Wilaya. Hii itarejesha dhamira njema aliyokuwa nayo Baba wa Taifa ya kulianzisha Shirika hili ili liwezeshe watu wa kipato cha chini na kati kuwa na nyumba bora.
Ili kutimiza azma hiyo, tunaziomba Halmashauri zote za Miji na Wilaya kulipatia Shirika ardhi yenye masharti nafuu ya kuwawezesha kujenga nyumba za gharama nafuu. Halmashauri zikifanya hivyo zitafanya nyumba zinazojengwa kuwa nafuu, na pia zitapata kodi ya majengo kutokana na nyumba hizo. Aidha, ujenzi wa nyumba utapendezesha mandhari ya Halmashauri hizo na kutoa ajira kwa watanzania.

No comments: