Wednesday, November 07, 2012

Kambi ya Taifa ya Kikapu yazinduliwa leo


: kutoka kushoto ni Roberto Quirzo- Afisa wa mambo ya umma ubalozi wa Marekani, Kocha Sconiers, Mkurugenzi msaidi wa michezo Yasoda na Makamu wa Rais wa TBF Magesa.
Mgeni rasmi , kocha na viongozi wa TBF wakiwa pamoja na wachezaji waliochaguliwa na Kocha Sconiers kuunda timu ya Taiafa ya Tanzania ya Kikapu.-
--
Tuna furaha kuwatangazia kuwa kambi ya timu ya Taifa ya kikapu (wanawake na wanaume) imezinduliwa leo asubuhi katika viwanja vya Don Bosco.
Mgeni rasmi katika uzinduzi huo alikuwa ni ndugu Roberto Quiroz Afisa wa mambo ya umma wa Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania.
Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Mkurugenzi Msaidizi wa  michezo toka wizara ya habari, utamaduni, vijana  na michezo ndugu Juliana Yasoda.
Kambi hiyo inaendeshwa na Kocha wetu wa timu ya Taifa ya Kikapu Jocuis Sconiers amabye ni Kocha Msaidizi wa Kocha Mkuu Albert Sokaitis.

Kocha Mkuu Sokaitis atakuja nchini baadae kuungana na Sconiers ili kuendeleza mafunzo haya katika mpango  wa maendeleo ya kikapu wa miaka 4, ambao tutakuwa tunaufanyia tathimini kila baada ya miaka 2. Kocha Sconiers alifika nchini ijumaa ya 2/11/2012 na siku iliyofuata alienda Tanga kwenye fainali za Kombe la Taifa na alichagua wachezaji wa timu ya Taifa kwa kushirikiana na makocha wazalendo.
Sehemu ya utekelezaji wa mpango huo utahusisha kufundisha timu ya Taifa, kuendesha mafunzo kwa vijana wetu wote wa umri mbali mbali (chini ya miaka 12, chini ya miaka 16 na chini ya miaka 18), kuongeza uwezo wa kuifundi kwa shirikisho la kikapu Tanzania, kuendesha mafunzo kwa walimu wetu wazalendo, kutambua na kuibua vipaji vilivyopo na kuviendeleza kwa kuwapatia mafunzo zaidi ya kikapu na nafasi za masomo katika vyuo vikuu mbali mbali huko Marekani. Mipango mingine iliyopo ni uendelezaji wa miundombinu ya mchezo wa kikapu nchini.

Malengo yetu kwa sasa ni kufanya vizuri katika mashindano yajayo ya kutafuta bingwa wa timu za Taifa za kanda ya tano ya FIBA Afrika yatakayofanyika hapa Dar Es Salaam mwezi January 2013 na baadae kupata nafasi ya kushiriki kutafuta bingwa wa Afrika (Afrobasket), lengo la mbele ni kushiriki mashindano ya Olimpiki ya 2016 yatakayofanyika huko Rio, Brazili.
Awamu hii ya kwanza ya mpango wa mafunzo unadhaminiwa na watu wa Marekani kupitia ubalozi wao hapa Tanzania, tunawashukuru sana watu wa Marekani.
Kwa niaba ya TBF nachukua fursa hii kuwapongeza watu wa Marekani kwa kumchagua tena Rais Barack Obama, ambaye ni mpenzi mkubwa na ni mchezaji wa mchezo wa kikapu.
Ili tuweze kufanikiwa tunaomba wadau wote wa michezo na wa maendeleo ikiwemo Serikali, taasisi za umma na binfasi, mtuunge mkono kwa hali na mali kufanikisha mpango huu wa mafunzo kwa timu ya Taifa na kwa makocha wetu wazalendo kwa faida ya vijana wetu na Taifa letu.
Mungu Ibariki Tanzania
PHARES MAGESA
MAKAMU WA RAIS-TBF

No comments: