Tuesday, November 27, 2012

*SHARO MILIONEA AFARIKI KWA AJALI YA GARI MUHEZA


 
Gari alilopata nalo ajali marehemu Sharo Milionea.
Kamanda wa Polisi mkoani Tanga, Constatine Masawe, amethibitisha kutokea kwa ajali iliyosababisha kifo cha Msanii,  Sharo Milionea, aliyepata ajali usiku wa kuamkia leo mida ya saa mbili usiku katika kijiji cha Lusanga, Muheza mkoani Tanga. 
*********************
MSANII mahiri wa filamu na muziki wa Bongo Flava nchini, Hussein Mkiety almaarufu, Sharo Milionea, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo majira ya saa mbili jana usiku, kwa ajali ya gari katikati ya Kijiji cha Lusanga na Maguzoni Songa, Wilaya ya Muheza mkoani Tanga.

Kwa mujibu wa kamanda wa polisi wa mkoa wa Tanga, Constatine Masawe,Sharo alikuwa peke yake garini wakati ajali hiyo ikitokea na mwili wake umehifadhiwa katika hospitali Teule ya Muheza. 



Kamanda Masawe alisema Milionea, akiwa anaendesha gari namba T478 BVR Toyota Harrier akitokea Dar es Salaam kwenda Muheza alipofika eneo hilo gari lake liliacha njia na kupinduka mara kadhaa na kusababisha kifo chake. 


Hii ni ajali ya pili kati ya alizowahi kupata msanii huyo, Sharo kwa mwaka huu baada ya Januari 5 kunusurika katika ajali ya basi alilokuwa amepanda la Taqwa likitokea Burundi kuelekea Dar es Salaam kupinduka katika eneo la Mikese, Morogoro saa mbili na nusu asubuhi.
Sharo ambaye alikuwa amekaa kwenye siti ya mbele kabisa alipoteza simu tu katika ajali hiyo ambayo ilijeruhi abiria wengine vibaya.

Kifo cha Sharo kinafuatia vifo vya wasanii wengine wawili wa filamu nchini ndani ya wiki moja, Mlopelo aliyetamba na kundi la Kaole na John Maganga aliyetamba na filamu ya 'Mrembo Kikojozi' aliyocheza na Aunt Ezekiel. 

Vifo hivyo vinakumbushia msiba wa Steven Kanumba, ambaye pia alifariki ghafla. 

Sharo atakumbukwa kwa ubunifu wake katika uigizaji akitoka kama mchekeshaji msafi tofauti na wachekeshaji wengi waliomtangulia ambao waliamini vichekesho ni lazima kuvaa kama katuni, kujaza nguo tumboni ili kuonekana na matumbo makubwa ama kujipaka masizi.

Akipendeza kwa mavazi nadhifu, Sharo Milionea alipata umaarufu kwa msemo wake wa "kamata mwizi meeen" na "Ooooh mamma!" huku akijipangusa mabega katika pozi za kibrazameni.

Katika siku za karibuni amekuwa akitawala vioo vya televisheni kutokana na kushiriki tangazo la kampuni ya huduma za simu ya Airtel akiwa na mchekeshaji mkongwe King Majuto, ambapo msemo wake mwingine wa "umebugi meen!" umetawala hasa midomoni mwa watoto.

No comments: