Thursday, July 01, 2010

JK awatisha wagombea urais CCM




CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimeandaa maandamano maalum kwa ajili ya kumsindikiza mgombea wake pekee wa urais kupitia chama hicho Jakaya Kikwete anayetarajia kurudisha fomu zake leo katika ofisi kuu chama hicho mjini hapa.

Katibu Mkuu wa Yusuf Makamba alisema jana kuwa anaamini Rais Kikwete atakuwa mgombea pekee wa urais katika chama hicho kwani hadi jana mchana hakukuwa na mtu mwingine aliyejitokeza.

“Niko ofisini kwa muda wote huo na sijamwona mtu mwingine, labda aje kesho (leo) asubuhi. Lakini hadi sasa Kikwete yuko pekee yake,” alisema Makamba.

Ikitokea amejitokeza mtu mwingine atatakiwa kuchukua, kuzijaza na kuzirudisha fomu hizo hapo hapo kwa kuwa muda utakuwa umekwisha, jambo ambalo ni gumu kwa sababu atakuwa hana muda wa kupata wadhamini 250 kutoka kila mkoa wa Tanzania.

Lakini Makamba alipotakia kueleza endapo CCM imeandaa sherehe zozote kwa ajili ya kusindikiza Kikwete alijibu “haya mengine mwulize Naibu Katibu Mkuu. Mimi siwezi kusema kwa kuwa ni mkurugenzi wa uchaguzi na bado nasubiri kama kuna wagombea wengine”.

Katibu wa Itikati na Uenezi wa CCM Kapteni John Chiligati aliweka bayana kuwa wanaCCM wameandaa sherehe na maandamano kwa ajili ya kumsindikiza Kikwete wakati anarudisha fomu hizo.

“Hawezi kurudisha fomu kimya kimya huyo ni mgombea wetu pekee. Shughuli zitaanza saa 4:00 na atasindikizwa hadi ofisini kwa katibu mkuu wa CCM ambako atarejesha fomu hizo,” alisema

Juni 21 mwaka huo Rais Jakaya Kikwete alichukua fomu za kuwania tena urais na kueleza kuwa serikali yake mpya itaongozwa na vipaumbele kadhaa vitavyosukumwa na misingi kumi.

Alitaja moja ya misingi hiyo kuwa ni kuongeza kasi ya mapambano ya rushwa na matumizi mabaya ya madaraka itakayoenda sambamba na kuimarisha utawala bora, utawala wa sheria, demokrasia na mapambano ya ubadhirifu wa mali za umma.

“Nitatumia bidii yangu yote kufanya kampeni ya kukipigania chama chetu kipate ushindi mkubwa na mara tutakapofanikiwa, vipaumbele vya serikali ijayo vitasukumwa na misingi kumi ifuatayo,” alisema Rais Kikwete.

“Kuhakikisha kwamba nchi inaendelea kuwa na umoja, amani na usalama, Kujenga msingi wa uchumi wa kisasa wa Taifa linalojitegemea kwa kuchukua hatua madhubuti za kuharakisha zaidi mapinduzi ya kilimo, ufugaji, uvuvi na viwanda.” SOURCE: MWANANCHI

1 comment:

Anonymous said...

jamani wengine tumechoka na huyu raisi ma-staili, jamani hembu kwa nini ccm isife!!!! maendeleo ya inchi yataanza baada ya arobaini ya ccm.