Wednesday, April 23, 2008

Kwaheri Ditopile





Kikwete aongoza mazishi ya Ditopile

RAIS Jakaya Kikwete jana aliongoza mamia ya waombolezaji katika mazishi ya aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Marehemu Ukiwaona Ditopile Mzuzuri (60) yaliyofanyika kwenye makaburi ya familia yao huko Kinyerezi, jijini Dar es Salaam.

Marehemu Ditopile alifariki dunia ghafla Aprili 20 katika Hoteli ya Hilux, iliyopo mkoani Morogoro mwishoni mwa wiki iliyopita.

Akimwelezea marehemu, msemaji wa famili ambaye ni mdogo wa marehemu, Abdallah Ramadhani Ditopile alisema kaka alikuwa ni nguzo ya familia yao kwa kipindi chote cha uhai wake hivyo kifo chake kimeacha pengo kubwa lisiloweza kuzibwa.

Akitoa salamu za Chama Cha Mapinduzi (CCM), Katibu wa chama hicho ambaye pia ni Waziri wa Michezo na Utamaduni, Kapteni George Mkuchika alisema mbali na kumfahamu marehemu wakiwa shuleni, alimfahamu zaidi kutokana na uadilifu wake kazini katika nyadhifa mbalimbali alizoshika.

Katika uhai wake, Ditopile aliwahi kuwa mbunge wa Ilala kwa miaka 10, Katibu Mwenezi wa CCM, Mkuu wa Mkoa Dar es salaam, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mkuu wa Mkoa Pwani, Naibu wa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mkuu wa Mkoa wa Lindi na Mkuu wa Mkoa wa Tabora.

Wakati wa dua ya kumuombea marehemu inasomwa nyumbani kwake, viongozi mbalimbali wa serikali walihudhuria wakiongozwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda pamoja na Mke wa Rais, Mama Salma Kikwete.

Hata hivyo, msiba huo ulitawaliwa na utani wa hapa na pale kati ya kabila la Wandengereko ambalo ni kabila la marehemu na kabila la Wanyamwezi na wasukuma ambao ni watani wa kabila hilo.

Katika hali hiyo ya utani, Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya na aliyekuwa Waziri wa Miundombinu Andrew Chenge waliombwa kwenda kula chakula cha watani ulioandaliwa kwa niaba yao msibani.

Baada ya hapo mwili wa marehemu ulipeleka katika Msikiti wa Tambaza kwa ajili ya kumuombea kuswaliwa na ilipomalizika swala hilo, ulipelekwa hadi katika makaburi Kinyerezi kwa kupitia barabara ya Umoja wa Mataifa, Morogoro, Mandela na Tabata Segerea.

Wakiwa katika makaburi hayo, mamia ya waombolezaji waliongozwa na Rais Kikwete waliweka mchanga katika kaburi la marehemu. Pichani Rais Jikwete, Bilionea Chenge na waombelezaji wengine wakijumuika.

No comments: