Wednesday, April 17, 2013

WAGONJWA 316 WAPATA HUDUMA ZA MADAKTARI BINGWA MKOANI KIGOMA

1 
Dk. Vence (Katikati) akiwa katika chumba cha upasuaji kutoa huduma kwa mmoja wa watoto ambao walifanyiwa upasuaji mapema leo (jana)
Wagonjwa wakisubiri kuonana na madaktari bingwa wa magonjwa ya kawaida6 (2) 
Wagonjwa wakisubiri kuonana na madaktari bingwa wa upasuaji2
Daktari Bingwa wa akina Mama Dk. Mrema (wapili kutoka kulia) akimsikiliza kwa makini mmoja wa wagonjwa waliolazwa hospitalini hapo kwa lengo la kutoa ushauri wa tiba sahihi.
Na Grace Michael, Kigoma
JUMLA ya wagonjwa 316 ndani ya siku mbili katika Hospitali ya Rufaa ya Maweni mkoani Kigoma wamefanikiwa kuonana na madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili ambao wapo mkoani humo kwa mpango unaoendeshwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF).
Mbali na wagonjwa hao kuonana na madaktari hao, jumla ya wagonjwa 11 ndani ya muda huo nao wamefanikiwa kufanyiwa upasuaji na madaktari hao hali inayoonesha kuwepo uhitaji mkubwa wa madaktari katika mikoa ya pembezoni ambayo miundombinu yake bado haijaimarika.
Hayo yanafanyika katika Mkoa wa Kigoma ndani ya mpango wa NHIF ambao ulizinduliwa mapema Aprili mwaka huu mkoani Lindi ambako nako timu ya madaktari bingwa watatu waliweka kambi katika Hospitali ya Mkoa na kufanikiwa kutoa huduma kwa mamia ya wananchi.
Katika Hospitali ya Maweni, timu ya madaktari wanne kutoka Muhimbili ilianza kazi rasmi jana (Jumatatu) na itakaa hospitalini hapo kwa muda wa siku saba lengo ni kutumia wataalam hao kitaifa.
Wagonjwa wanaonufaika na mpango huu ni wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na wananchi kwa ujumla ambao wanapata huduma kupitia utaratibu wa kawaida.
Wagonjwa waliofanikiwa kujiandikisha kwa lengo la kupata huduma kutoka kwa wataalam hao ni kutoka katika wilaya zote za mkoa wa Kigoma ambapo wanaeleza kuwa ni fursa ya kipekee kuipata.
Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi wagonjwa ambao wamepata huduma ambao walifikishwa hospitalini hapo wakiwa na hali mbaya waliushukuru Mfuko kwa kuanzisha mpango huo ambao moja kwa moja unawagusa wananchi hasa wa kipato cha chini.
Kwa upande wa watumishi hospitalini hapo, wanasema kuwa wataitumia fursa hii vyema hasa katika kujifunza mambo mbalimbali kutoka kwa madaktari hao bingwa ili waweze kuboresha huduma zao kwa wagonjwa hata watakapobaki wenyewe.
Idadi ya wagonjwa inazidi kuongezeka kila kukicha hatua inayowalazimu madaktari hao kufanya kazi kwa zaidi ya saa 15 bila ya kupumzika.
Akizungumzia mwitikio huo, Naibu Mkurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Hamis Mdee, alisema kuwa mwitikio huo ni faraja kwa Mfuko ambao lengo lake ni kutoa huduma kwa Watanzania na kuhakikisha afya zao zinaimarika.
“Sisi kama Mfuko tunaona faraja sana tunapoona wagonjwa wamefika hapa na kupata huduma hizi ambazo pengine wasingeweza kuzipata hivyo tutaendelea na mpango huu kwa kuwa unagusa moja kwa moja uhai wa wanachama wetu na wananchi kwa ujumla,” alisema Mdee.
NHIF imeanzisha mpango huu na utatekelezwa katika mikoa mbalimbali ya pembezoni ikiwemo Rukwa, Katavi, Pwani, Lindi na Kigoma.

No comments: