Monday, August 24, 2009

Wanafunzi walioteketea na moto kuzikwa



SERIKALI imefunga Shule ya Sekondari ya Idodi kwa muda wa siku 21 kufuatia vifo vya wanafunzi wa kike 12 na kujeruhi wengine 23 baada ya bweni la wasichana la Shule hiyo kuteketea kwa moto.
Akizungumza ana wanafunzi wa shule hiyo wakiwemo walionusurika na ajali hiyo pamoja na wazazi wao jana, Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi stadi, ProfesaJumannne Maghembe aliyefuatana na Naibu wake, Mwantumu Mahiza alisema wamefikia hatua hiyo ili kuweza kupata nafasi nzuri ya kuisitiri miili ya wanafunzi waliokufa na kujipanga.
Alisema ajali hiyo ni kubwa na inatia huzuni kwa wanafunzi,wazazi na majirani wanaoishi katika eneo na endapo shule haitafungwa itakuwa ni hatari kubwa kwa wanafunzi walionusurika.
Alisema wanafunzi 326 walinusurika hawana mahali pa kulala baada ya bweni hilo kuteketea na moto ambalo linachukua watoto 461 lenye vyumba 25 kuteketea kabisa na moto huo uliozuka usiku wa manane Agosti 23 mwaka huu.
Maghembe alisema kuwa kuwa shule hiyo imefungwa rasmi Agosti 23 na itafunguliwa Septemba 13 mwaka huu ili kutoa nafasi kwa serikali kufanya ukarabati wa bweni hilo lenye vyumba 25 yalioharibiwa kwa kuteketezwa na moto uliosababishwa na mshumaa uliokuwa ukitumiwa na mmoja wa wanafunzi, Naomi Nyange aliyekuwa akijisomea.
Alisema pia serikali inaangalia uwezekano wa kuweka umeme na muundo wa ujenzi wa mabweni iwe na milango mingi ili inapotokea janaga kama hilo iwe rahisi kuokoka.
Naye Kaimu Mkuu wa mkoa wa Iringa Aseri Msangi akizungumzia kuhusu mazishi alisema kuwa wanafunzi wote 12 waliofariki dunia watazikwa kwa pamoja katika eneo la shule kesho, Agosti 25 mwaka huu. Imeandikwa na Hakimu Mwafongo.

No comments: