Wednesday, May 10, 2017

BALOZI SYLEVESTER MABUMBA, BALOZI WA TANZANIA VISIWANI KOMORO AWASILISHA NAKALA YA HATI ZAKE ZA UWAKILISHI KWA WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA KOMORO, MHE, MOHAMED BACCAR DOSSAR

Mhe. Sylvester Mabumba Balaozi wa Tanzania ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Visiwa vya Komoro jana tarehe 09 Mei aliwasilisha nakala za hati zake za uwakilishi kwa Mhe. Mohambed Baccar Dossar, Waziri wa Mambo ya Nje wa Komoro. Hafla hiyo ilifanyika siku hiyo hiyo ambayo Mhe. Balozi aliwasili Visiwani Komoro jambo ambalo linaonesha jinsi gani nchi hizi mbili zimedhamiria katika kuboresha na kukuza mahusiano yaliopo baina yao. 

Katika hafla hiyo Mhe. Dossar alichukua fursa hiyo kumkaribisha Mhe. Balozi Mabumba Visiwani Komoro na kumtakia kila la kheri katika kipindi chake ambacho atakuwa Balozi Visiwani hapa. Aidha Mhe. Waziri alimuahidi Mhe. Balozi Mabumba kuwa nchi yake itampatia ushirikiano maradufu na kwamba milango yake ipo wazi muda wowote ambapo Mhe. Balozi atakuwa na shida ya kuonana nae na kufanya mazungumzo. 
 
Kwa upande wake Mhe. Balozi Mabumba alionyesha furaha yake kwa kumuelezea Mhe. Waziri kuwa amejiskia faraja sana kwa kuchaguliwa kuwa Balozi wa Pili kuiwakilisha Tanzania Visiwani Komoro na kwamba anaimani kuwa Serikali ya Komoro itampatia ushirikiano wa kutosha katika kutekeleza majukumu yake. 
 
Aidha Mhe. Balozi Mabumba alieleza kuwa uhusiano uliopo baina ya Tanzania na Komoro ni wa Kihistoria na unapaswa kudumishwa. Mhe Balozi alimueleza Mhe. Waziri kuwa moja ya agenda zake za mwanzo ambazo anataka kutekeleza ni ile ya utiaji saini wa Mkataba wa Kudumu wa Ushirikiano baina ya Tanzania na Comoro (Joint Permanent Commission).

No comments: