Tuesday, December 01, 2009

Rufaa ya babu seya yaahirishwa



Rufaa ya mwanamuziki maarufu, Nguza Viking (pichani kulia) maarufu kwa jina la Babu Seya na wanawe watatu, imehairishwa hadi Desemba 3 mwaka huu, ili upande wa Jamhuri uweze kupitia nyaraka mbalimbali zilizowasilishwa na mawakili wa upande wa utetezi.

Katika rufani hiyo pia wamo watoto wake ambao ni Papii Nguza, Nguza Mbangu na Francis Nguza ambao wanapinga hukumu waliyohukumiwa kutumikia jela maisha iliyotolewa mwaka 2004 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam.

Rufani hiyo iliahirishwa jana mbele ya jopo la majaji watatu lililokuwa likiongozwa na Nathalia Kimaro pamoja na wenzake ambao ni jaji Mbarouk Salim Mbarouk na Salum Massati.

Awali upande wa utetezi uliokuwa ukiongozwa na wakili wa kujitegemea Mabere Malando aliiomba Mahakama hiyo ya Rufaa kupokea maombi yake yakurekebisha maombi ya rufani iliyowasilishwa Mahakamani hapo na iweze kusomeka kesi namba 56/2005 ya makosa ya jinai badala ya kesi namba 56/2009.

Mbali na ombi hilo pia aliiomba Mahakama kuongeza sababu nne za kufungua rufani hiyo na hivyo kuwa na sababu 19, alidai kuwa ameamua kuongeza sababu hizo kutokana na kuona baadhi ya vitu vilisahaurika katika rufaa iliyowasilishwa awali na wakili Nyange.

“Licha ya kuongeza hizi nne baadhi ya sababu nitaziacha wakati tukiendelea kusikiliza rufaa hii,” alidai Marando.

Upande wa Jamuhuri uliokuwa ukiongozwa na Justuce Mlokozi, ulikubaliana na maombi hayo na kudai kuwa maombi hayo waliyapokea wiki iliyopita.

Mlokozi alidai kuwa baadhi ya vielelezo vya ushahidi vilichelewesha kufikishwa katika ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka Nchini (DPP) ambapo alidai nyaraka hizo alizipata Novemba 27 wakati muda wa kazi ukiwa umeisha.
Alidai kuw akutokana na hali hiyo hajaweza kuzipitia kwa haraka kutokana na kuwa nyingi ambapo alidai kuwa nyaraka hizo ni zaidi ya 20 ambako alidai kuwa atakuwa akisoma taratibu.

Pia alidai kuwa kabla ya kesi hiyo kuanza jana Mahakamani hapo Malando alimpatia nyaraka nyingine ambazo bado hajajua zinasema nini ambapo alidai kuwa kutokana na uwingi huo aliiomba Mahakama kuhairisha shauri hilo ili kuweza kupata muda wa kusoma.

Mbali na hayo Mlokozi alidai kutoelewa sababu ya 14 na 15 ambapo alidai kuwa sababu ya 14 inashambulia Mahakama ya Mkoa kwakutoweka kumbukumbu vizuri wakati sababu namba 15 nayo pia inashambulia Mahakama Kuu kwa kutokuweza kumbukumbu vizuri.

1 comment: