Thursday, December 31, 2009

Mzee Kawawa Amefariki!



Waziri Mkuu wa Tanganyika na mpigania huru wa Tanganyika na Muasisi wa Muungano mzee Rashid Mfaume Kawawa amefariki dunia. Mzee Kawawa alikuwa ni swahiba wa karibu zaidi wa baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere.

Mzee Kawawa alizaliwa Mei 27 , 1926 huko Songea kijiji cha Matepwende mkoani Ruvuma. Alianza elimu ya msingi huko Liwale Lindi. Aliendelea na elimu ya kati (middle school) hapo Dar-es-Salaam school ambapo mmojawapo wa wanafunzi wengine ni marehemu mzee Kanyama Chiume mpigania uhuru toka Malawi aliyeishi uhamishoni nchini Tanzania kwa muda mrefu. Wengine katika shule hiyo wakati huo ni pamoja na kina Abdul Sykes, Ali Sykes, Hamza Aziz na Faraji Kilumanga.

Aliendelea na masomo yake huko Tabora Boys kati ya 1951-1956. Alikuwa ni Waziri Mkuu wa Tanganyika mwaka 1962 wakati Mwalimu Nyerere alipoamua kwenda mikoani kujenga chama na kufanya shughuli za kisiasa. Baadaye aliteuliwa tena kuwa Waziri Mkuu mwaka 1972-1977 na akawa miongoni mwa wahamasishaji wakubwa wakati wa vita ya kumng'oa nduli Idi Amin ambapo alitembelea wapiganaji wetu waliokuwa mstari wa mbele kule Uganda. Hii ilimpatia jina la "Simba wa Vita" jina ambalo lilimkaa vyema kwa muda mrefu.

Kabla ya kuingia katika harakati za kupigania Uhuru Mzee Kawawa alikuwa ni miongoni mwa waanzilishi wa Shirikisho la Wafanyakazi mwaka 1955 ambapo alichaguliwa kuwa Katibu wake Mkuu wa kwanza. Ni katika nafasi hii ndiyo aliweza kuanza kushiriki kwa nguvu zaidi katika harakati za kupigania uhuru wa Tanganyika akihamasisha wafanyakazi. Kabla ya hapo alikuwa ni Katibu Mkuu wa Shirikisho la Wafanyakazi wa Serikali.

Februari 1956 Mzee Kawawa aliacha kazi yake ya Shirikisho la Wafanyakazi kutokana na kuwa mwajiriwa wa serikali kitu ambacho kilimkataza kuhusisha na siasa na kuamua kuingia katika harakati za kudai uhuru kupitia TANU. Alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya TANU mwaka 1957, Makamu mwenyekiti wa TANU mwaka 1960.

Mwaka 1964 baada ya Muungano Mzee Kawawa alikuwa ni Makamu wa Pili wa Rais akiwa ni msaidizi wa Rais wa Muungano kwa upande wa mambo ya Bara.

Katika siasa amewahi kushika nafasi mbalimbali ikiwemo ile ya Ukatibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi na Makamu Mwenyekiti wa CCM na amekuwa mjumbe wa kudumu wa Kamati Kuu ya CCM.

Mzee Kawawa alikuwa ni mtoto wa kwanza kati ya watoto nane na mojawapo ya kazi zake za awali ilikuwa ni uchezaji wa filamu za uhamasishaji na akawa ndiye mcheza filamu wa kwanza kiongozi mweusi (lead actor).

Mzee Kawawa alikimbizwa hospitali hapo jana kutokana na hali yake kuwa mbaya na kulazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi; ambapo mapema leo asubuhi alifariki dunia. Mipango ya mazishi inaandaliwa.

Mungu ailaze roho ya Marehemu Pema Peponi, Amina.

Imeandikwa na: Mwanakijiji

2 comments:

Anonymous said...

MBONA MIAKA YA KUSOMA TABORA NA KUFANYA KAZI IKO PAMOJA? ALIKUWA MWANAFUNZI MFANYA KAZI? TUAMBIENI UKWELI AU TUNGENI UPYA. KAWAWA ALIKUWA MMOJA WA WACHEZA FILAMU NA WALIKUWEPO WENGINE KAMA ANDREW CHANZI ALIYECHEZA DAWA YA MAPENZI.

Unknown said...

I 'm so glad you could come across this site ,
and we hope to establish good relations with you.
greetings from me ( Seo Milanisti )
peninggi badan | obat peninggi badan super cepat | obat peninggi badan

pelangsing badan | obat pelangsing badan | obat pelangsing badan super cepat