Sunday, December 27, 2009

Yanga bingwa Tusker






Yanyakuwa Mil 40

TIMU ya Yanga imefunga mwaka kwa 2009 kwa kishindo baada ya kutwaa ubingwa wa michuano ya Kombe la Tusker kwa kuichapa Sofapaka kwa mabao 2-1 kwenye mchezo uliochezwa Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Yanga walilazika kusubili hadi dakika tano za mwisho kuanza kusherekea ubingwa wao kwa mabao yaliyofungwa na Mrisho Ngassa (90 dk), na Boniface Ambani (85dk).

Mabingwa hao wa Tanzania wamefanikiwa kujinyakulia shilingi milioni 40, huku ndugu zao Simba wakijinyakulia nafasi ya tatu Mil 10 na Wakenya hao Sofapaka washindi wa pili walijinyakulia Mil 20.

Mshambuliaji Jerryson Tegete alikabidhiwa zawadi yake ya ufungaji bora Mil 2 baada ya kufunga jumla ya mabao 6 kwenye michuano hiyo, huku Mafunzo ya Zanzibar imepata tuzo ya timu yenye nidhamu.

Katika mchezo huo mabingwa wa Kenya, Sofapaka walikuwa wa kwanza kupata bao la kuongoza dakika ya 34 kupitia kwa Wanyama Thomas kwa mpira wa adhabu ukiwa nje kidogo ya 18 baada ya Mohamed Bakari kumwangusha Humphrey Ochieng uliokwenda moja kwa moja wavuni na kumwacha kipa Obren asijue la kufanya.

Katika kipindi cha pili wachezaji wa Sofapaka wakionekana kuanza kuchoka na kutoa nafasi kwa Yanga waliokuwa wakicheza soka safi ya kuona na kupanga mashambulizi wanavyota.

Dakika 82, Ngasa alitumia kasi yake na kuwazidi mbio mabeki kwenye eneo la hatari na kupiga shuti lilomgonga Ambani na kuokolewa na mabeki.

Mkongwe huyo Ambani alijirekebisha na kuifungia Yanga bao la kusawazisha zikiwa zimebaki dakika 85 kwa kumalizia mpira uliomgonga kipa na kurudi uwanjani. Imeandikwa na Sosthenes Nyoni wa Mwananchi.

No comments: