Monday, October 26, 2009

Visa 2 dance







TAMASHA ngoma za ubunifu linalofahamika kama Visa2 dance limemalizika, huku likiacha simulizi kwa watu wa mataifa mbalimbali hususani waliohudhuria.

vikundi tofautitofauti kutoka mataifa mbalimbali vimeshiriki tamasha hilo na kuonyesha mshikamano wa kipekee miongoni mwa wasanii na mashabiki wa ngoma hizo.

Mratibu wa tamasha hilo Aloyce Makonde amevitaja vikundi hivyo kuwa ni Kunja Dance Theatre na Jokajoka Dance (Kenya), FLUSSO dance Project na I'mperfect dancers (Italia),Dansgroep Amsterdam (Nertherland) Zufit Simon (Ujerumani) FACT (Afrika Kusini).

Vingine ni Jus De la vie (Sweeden) Aduga Community dance and Theatre Company ( Ethiopia) na Mionzi Dance Theatre, LumumbaTheatre Group na THT vya Tanzania.

Tamasha hilo limetanguliwa na warsha na mihadhara iliyoanza Jumatatu kwa wataalamu mbalimbali kuendesha mafunzo ya sanaa ya dansi ya ubunifu.
Warsha hizo zililenga utengenezaji wa jukwaa na matumizi ya taa, mavazi, historia ya dansi ya ubunifu, uhamasishaji na utawala wa sanaa dansi ya ubunifu.

Pia matumizi ya teknolojia kwenye dansi ya ubunifu ambazo zilitolewa na wataalamu wa humu nchini na nje ya nchi.

Makonde alisema: “ Visa 2 Dance ni tukio kubwa ambalo litatoa fursa kwa washiriki toka nchi mbalimbali kuonyesha umahiri wao kwa pamoja katika sanaa ya dansi.

“ Kupitia tukio hili wasanii wa Tanzania watapata nafasi ya kuonyesha vipaji vyao kwenye uwanja wa sanaa wa kimataifa na watapata nafasi ya kujifunza na kubadilishana uzoefu.”

Makonde alisema kuwa tamasha la Visa 2 Dance linalenga kukuza vipaji miongoni mwa wasanii wa Tanzania na kuwapa uwezo wa kufikia malengo yao ya kisanii.

Baadhi ya malengo hayo ni pamoja na kuanzisha utaratibu wa kubadilishana uzoefu kupitia muziki, dansi na maigizo, kufungua mipaka ya kiutamaduni, kukuza mahusiano ya kimataifa na kuendeleza sanaa na utamaduni katika jamii ya Watanzania.

“ Mara ya kwanza tamasha hili lilifanyika mwaka jana na kushirikisha washiriki wa humu nchini. Mara ya pili lilifanyika mwaka jana ambapo idadi ya washiriki iliongezeka kufikia nchi 6 ambapo mwaka huu wan nchi 9 zilifanikiwa kushiriki tamasha hilo.
Imeandaliwa na Maimuna Kubegeya.

No comments: