Pemba, Zanzibar | Januari 4, 2026
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, amewasili kisiwani Pemba kwa ajili ya Sherehe ya Uzinduzi wa Jengo la Ofisi ya Uhamiaji pamoja na Makazi ya Askari, tukio muhimu linalofanyika Wilaya ya Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Mara baada ya kuwasili, Dkt. Kikwete amepokelewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Anna Makakala, pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba, Mgeni Hassan Yahaya.
Uzinduzi wa jengo hilo unafanyika leo tarehe 4 Januari, 2026, na ni sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 62 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar, yanayoendelea kuenzi historia, mshikamano na maendeleo ya wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.
Jengo hilo jipya la Ofisi ya Uhamiaji na Makazi ya Askari linatarajiwa kuimarisha utoaji wa huduma za uhamiaji, kuongeza ufanisi wa kiutendaji pamoja na kuboresha mazingira ya kazi na makazi kwa askari, hatua inayochochea usalama, utulivu na maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Ushiriki wa Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete katika uzinduzi huu unaendelea kuakisi mshikamano wa kitaifa, kuthamini mchango wa viongozi waliotangulia na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuimarisha miundombinu na huduma muhimu kwa wananchi, hususan katika kipindi hiki cha maadhimisho ya kihistoria ya Mapinduzi ya Zanzibar.




No comments:
Post a Comment