Saturday, January 31, 2026

TANAPA YASHIRIKI TUZO ZA THE SERENGETI AWARDS JIJINI ARUSHA









Bodi ya Wadhamini ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) inayoongozwa na Mkuu wa Majeshi Mstaafu Jenerali George Waitara, pamoja na Menejimenti ya TANAPA, leo Januari 31, 2025, inashiriki hafla ya utoaji wa Tuzo za The Serengeti Awards inayofanyika katika Hoteli ya Mount Meru, jijini Arusha.

Tuzo hizo zinalenga kutambua na kuthamini mchango wa wadau wa uhifadhi na utalii katika kukuza sekta ya uhifadhi na utalii pamoja na kuitangaza Tanzania kupitia vivutio vyake mbalimbali vya utalii.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, huku tukio hilo likihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, pamoja na wadau wa sekta ya utalii.

DKT. MWIGULU KUMUWAKILISHA RAIS DKT. SAMIA KWENYE HAFLA YA UTOAJI TUZO ZA UHIFADHI NA UTALII

 







WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Januari 31, 2026 amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) ambapo anatarajiwa kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika hafla ya Utoaji wa Tuzo za kitaifa za Uhifadhi na Utalii (The Serengeti Awards).

Pia, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu atatembelea Hifadhi ya Taifa ya Arusha ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Mhe. Rais Dkt. Samia katika kukuza Utalii nchini.

Friday, January 30, 2026

 



‎
Bodi ya Kitaaluma ya Ununuzi na Ugavi (PSPTB), inayofanya kazi chini ya Wizara ya Fedha, imetoa onyo kali kwa watahiniwa wote wa fani ya Ununuzi na Ugavi kujiepusha na vitendo vya ukiukwaji wa kanuni na taratibu za mitihani, ikisisitiza kuwa haitasita kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya watakaobainika kufanya udanganyifu.

‎Onyo hilo limetolewa Januari 30, 2026 jijini Dodoma na Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB, Bw. Godfred Mbanyi, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu udahili na matokeo ya mitihani ya 32 ya bodi hiyo.

‎Bw. Mbanyi amesema adhabu kwa mujibu wa kanuni ni pamoja na kufutiwa matokeo ya mitihani yote, kusimamishwa kushiriki mitihani kwa mikao mitatu mfululizo, kutozwa faini au hata kifungo cha jela kulingana na uzito wa kosa.

‎Katika mitihani hiyo, jumla ya watahiniwa 1,291 walidahiliwa, ambapo watahiniwa 1,223 walifanya mitihani huku watahiniwa 68 wakikosa kushiriki kwa sababu mbalimbali. 

‎Kati ya waliofanya mitihani, watahiniwa 595 sawa na asilimia 48.7 walifaulu, watahiniwa 589 (asilimia 48.2) wanarudia masomo yao, huku watahiniwa 39 sawa na asilimia 3.2 wakifeli na kuanza upya masomo yao katika ngazi husika.

‎Aidha, Bw. Mbanyi ameeleza kuwa watahiniwa wawili wa ngazi ya CPSP walikamatwa wakijihusisha na ukiukwaji wa taratibu za mitihani baada ya kubainika kuingia ndani ya vyumba vya mitihani wakiwa na karatasi zinazodhaniwa kuwa na majibu ya mitihani.

‎Amesema Bodi ya Wakurugenzi imeielekeza Kamati ya Usajili na Nidhamu kushughulikia suala hilo, na endapo wahusika watapatikana na hatia, watachukuliwa hatua kali kwa mujibu wa kanuni zilizopo. 

‎Kwa sasa, matokeo ya watahiniwa hao yamezuiliwa na wahusika watapewa haki ya kusikilizwa mbele ya kamati husika.

‎Kwa upande mwingine, PSPTB imewahimiza watahiniwa waliokosa alama za kutosha kujisajili upya na kurudia masomo yao katika mitihani inayotarajiwa kufanyika Mei 2026.

‎Bw. Mbanyi pia amewakaribisha wahitimu wa vyuo vikuu vya ndani na nje ya nchi kujisajili kufanya mitihani ya kitaaluma ya PSPTB ili kupata sifa stahiki katika fani ya Ununuzi na Ugavi.

‎Kadhalika, wazazi, wadhamini na waajiri wametakiwa kuwasaidia watahiniwa kwa kuwalipia ada za maandalizi na mitihani, hatua itakayochochea ukuaji wa wataalamu wenye maarifa na ujuzi katika sekta hiyo muhimu.

‎PSPTB imetoa pongezi kwa watahiniwa wote waliofaulu katika ngazi mbalimbali, wakiwemo waliopata sifa za kutunukiwa Vyeti vya Professional Diploma, Graduate Professional na CPSP, pamoja na wahadhiri na wakufunzi kutoka vyuo na vituo vya mafunzo kwa mchango wao katika kuwajengea watahiniwa uwezo wa kufanya vyema

CHONGOLO AELEKEZA MAKAMISHNA WA TCDC MAMBO SITA YA KUZINGATIA KUIMARISHA USHIRIKA

 

Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb) ameelekeza mambo sita muhimu kuzingatia ili ushirika kuimarika zaidi na kuleta tija kwa wanaushirika.

Akizungumza tarehe 30 Januari 2026 jijini Dodoma wakati akizindua Bodi ya Makamishna wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Waziri Chongolo amesema Kamisheni ihakikishe inaleta mageuzi ya kidigitali ili takwimu sahihi zipatikane kwenye mizani ya kidigitali na kupunguza udanganyifu kwa wanachama na wakulima. 

Jambo la pili ameielekeza Kamisheni kuhakikisha ukaguzi unafanyika kwa vyama vyote vya ushirika nchini kila mwaka na hatua stahiki kuchukuliwa kwa wahusika wote wanaokiuka taratibu na kurudisha nyuma jitihada za maendeleo ya ushirika. Pia, masoko ya nje yatafutwe ili bidhaa zinazozalishwa na Vyama vya Ushirika ziuzwe na kuleta tija ya mitaji.

Kuhusu suala la nne, Kamisheni imetakiwa kuhakikisha mali za vyama vya ushirika zinawekezwa ipasavyo ili ziweze kuzalisha na kusaidia kuleta maendeleo yanayotarajiwa na wanaushirika. Sambamba na hilo, uadilifu, weledi na ubunifu vimetiliwa mkazo kuwa ni chachu ya kuimarisha ushirika. 

Aidha, jambo la mwisho ni kuhakikisha kunakuwa na ujenzi wa viwanda, upatikanaji wa huduma za bima ya mazao, huduma za matibabu na mafao ya uzeeni kwa wakulima. 

“Ni matumaini yangu kuwa Kamisheni hii itaweza kutekeleza haya kwa weledi na niwapongeze tena Wajumbe wote kwa kuteuliwa kwani tunahitaji kuleta matokeo kwa wakulima,” amesema Mhe. Chongolo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania, Bw. Abdulmajid Nsekela amemuhakikishia Mhe. Waziri Chongolo kuwa Bodi na pia kwa kushirikiana na Mrajis na Mtendaji Mkuu wa lTCDC, Dkt Benson Ndiege watatekeleza maelekezo yake katika kuhakikisha ushirika unakuwa nguzo ya uchumi shirikishi utakaochochea ajira na maendeleo ya Taifa.







RAIS SAMIA AMEJIPANGA KUFIKISHA UMEME VITONGOJI VYOTE




📌Bilioni 24.9 kupeleka umeme vitongoji 218 Njomb

📍Njombe

Imeelezwa kuwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameelekeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kufikisha umeme kwenye vitongoji vyote vilivyobakia nchini ambavyo bado havina huduma ya umeme ifikapo mwaka 2030.

Hayo yamebainishwa leo Januari 30, 2026 na Bw. Frank Mugogo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mha. Hassan Saidy wakati wa hafla fupi ya kumtambulisha mkandarasi kutoka kampuni ya Central Electricals International Ltd katika Mradi wa HEP 2B ambaye anaenda kutekeleza kwenye vitongoji 218 mkoani Njombe.

"Jumla ya vitongoji vyote mkoa wa Njombe ni 1,833 na vitongoji vyenye umeme ni 1,276. Vilevile vitongoji ambavyo havina umeme ni 557. Hivyo mradi huu unakwenda kupeleka umeme kwenye vitongoji 218 katika mkoa huu na vitabakia vitongoji 339 ambavyo havina umeme navyo vitakamilika, " Amesema Bw. Mugogo.

Ameongeza kuwa, gharama za kuunganisha umeme huo ni shilingi 27,000 tu na kuwataka wananchi wa mkoa huo kutumia fursa ya kuunganisha umeme kwa gharama nafuu iliyowezeshwa na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe.Rais Samia.

Akizungumza mara baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa miradi hiyo mkoani Njombe, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa Bw. Lewisi Mnyambwa amemshukuru Rais Samia kwa kuleta fedha nyingi zaidi ya bilioni 24 ili kupeleka umeme kwenye vitongoji vya mkoa wa Njombe.

"Serikali kupitia REA imefanya kazi kubwa. Tunasisitiza miradi hii ikamilike kwa muda uliopangwa na tutaendelea kuusimamia ipasavyo ili mkandarasi aweze kutekeleza majukumu yake pasipo changamoto yeyote katika kipindi chote cha utekelezaji wa mradi," Amesema Mnyambwa. 

Aidha, ametoa rai kwa wananchi wanaozunguka eneo la mradi kumpatia ushirikiano mkandarasi huyo na ametakiwa kutoa kipaumbele cha ajira kwa wazawa ili kufanya shughuli mbalimbali katika mradi huo ili uchumi wa wananchi uongezeke na wanufaike na uwepo wa miradi hiyo katika mazingira yao.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Miradi kutoka kampuni ya Central Electricals International Ltd, Bw. Zameer Meghji ameishukuru Serikali kupitia REA kwa kupewa fursa ya kutekeleza mradi huo mkubwa. Amesema watahakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati, watashirikiana na wananchi na kutoa kipaumbele cha ajira kwa wazawa ili miradi hiyo ilete tija kwa wananchi na nchi kwa ujumla.

WITO KWA WAFANYABIASHARA NDOGONDOGO KUCHANGAMKIA FURSA YA MIKOPO YA SERIKALI YENYE RIBA NAFUU



 

NGORONGORO SAKO KWA BAKO NA TAASISI ZA ELIMU KUTANGAZA VIVUTIO VYA UTALII NA KUIMARISHA ELIMU YA UHIFADHI

 





Monduli, Arusha – Januari 30, 2026

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) imeendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuwa mstari wa mbele katika kulinda rasilimali za asili na kuandaa kizazi kijacho chenye uelewa wa kina kuhusu uhifadhi endelevu, kupitia kampeni maalum ya utoaji elimu ya vivutio vya utalii na masuala ya uhifadhi kwa taasisi za elimu zilizopo Wilaya ya Monduli, mkoani Arusha.

Katika kampeni hiyo iliyofanyika leo, NCAA ilikutana na wanafunzi pamoja na walimu kutoka Shule za Sekondari Manyara, Lowasa, Rift Valley pamoja na Chuo cha Maendeleo ya Wananchi (FDC) Mto wa Mbu, ambapo washiriki walipata fursa ya kujifunza kwa kina kuhusu thamani ya kipekee ya Hifadhi ya Ngorongoro, mchango wake kwa uchumi wa taifa, na wajibu wa jamii katika kuilinda kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo, mwakilishi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro alisema kuwa lengo kuu la kampeni hiyo ni kujenga uelewa, uzalendo na hisia za umiliki miongoni mwa vijana kuhusu rasilimali za asili, hususan vivutio vya utalii vilivyopo ndani ya Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, ambalo ni miongoni mwa maajabu ya dunia yanayotambuliwa kimataifa.

“Ngorongoro si urithi wa Tanzania pekee, bali ni urithi wa dunia. Ili uendelee kudumu, ni lazima vijana waelewe thamani yake mapema na washiriki kikamilifu katika juhudi za uhifadhi,” alisema.

Kupitia mawasilisho, majadiliano na maswali ya wazi, wanafunzi walielimishwa kuhusu aina mbalimbali za vivutio vya utalii, ikiwemo Crater ya Ngorongoro, wanyamapori adimu, urithi wa kihistoria na kiutamaduni, pamoja na mchango wa utalii katika kuongeza mapato ya taifa na kuboresha huduma za kijamii.

Aidha, elimu ya uhifadhi iligusia masuala ya matumizi endelevu ya rasilimali, athari za uharibifu wa mazingira, mabadiliko ya tabianchi, na umuhimu wa jamii kushirikiana na taasisi za uhifadhi katika kulinda mazingira yao.

Walimu na wanafunzi walipongeza hatua hiyo ya NCAA, wakieleza kuwa elimu waliyoipata itaongeza motisha kwa vijana kuzingatia masomo yanayohusiana na mazingira, utalii na uhifadhi, sambamba na kuwa mabalozi wazuri wa kutunza mazingira katika jamii zao.

Mwalimu mmoja kutoka Shule ya Sekondari Lowasa alisema kampeni hiyo imewawezesha wanafunzi kuona uhifadhi si dhana ya darasani pekee, bali ni jukumu la kila mwananchi.

“Hii ni elimu inayogusa maisha ya kila siku. Wanafunzi wetu sasa wanaelewa kuwa kulinda mazingira ni kulinda maisha yao ya baadaye,” alisema.

Kupitia kampeni hii, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro inaendelea kuimarisha uhusiano wake na taasisi za elimu, ikilenga kuandaa kizazi chenye maarifa, maadili na uwajibikaji katika kulinda na kutangaza vivutio vya utalii na rasilimali za asili za Tanzania.

Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa NCAA wa kuwekeza katika elimu, uhamasishaji wa jamii na ushirikishwaji wa vijana kama nguzo muhimu ya uhifadhi endelevu na maendeleo ya sekta ya utalii nchini.

FURSA MPYA KWA VIJANA: BILIONI 2 KWA WATENGENEZAJI WA MAUDHUI



Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Paul Makonda, amesema Wizara imepatiwa kiasi cha TZS bilioni 2 itakayowawezesha watengenezaji wa maudhui mbalimbali mitandaoni kuimarisha kazi zao na kuwaongezea kipato kupitia majukwaa ya kidijitali.

Amesema hayo Januari 29, 2026 jijini Dodoma na kubainisha kuwa, fedha hizo zimetolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kuyawezesha makundi yote ya watengeneza maudhui ikiwemo katika Sekta ya Utalii, Michezo, Habari, Jamii, Muziki, Filamu na sanaa nyinginezo. 

Amebainisha kuwa, zoezi la uandikishaji wa walengwa linaanza rasmi Januari 30 hadi Februari 15, 2026, ambapo watengenezaji wa maudhui wanatakiwa kufika katika ofisi za Halmashauri za Wilaya, Manispaa za Miji na Majiji kupitia vitengo vya habari, ili kuchukua na kujaza fomu za maombi, zikiainisha taarifa binafsi pamoja na shughuli wanazozifanya.

Thursday, January 29, 2026

MSAJILI WA HAZINA AZINDUA MPANGO MKAKATI WA NMB 2026-2030

Mwandishi wa OMH

Dar es Salaam. Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amezindua Mpango Mkakati wa Muda wa Kati wa Benki ya NMB wa mwaka 2026 hadi 2030 (Agenda 2030).

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo unaolenga kuboresha utendaji kazi wa benki hiyo, Bw. Mchechu aliupongeza uongozi wa NMB na Bodi ya Wakurugenzi kwa kuifanya benki hiyo kuwa miongoni mwa benki bora zinazochangia kwa kasi ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

Alisema kuwa katika kipindi cha miaka mitano, Serikali, inayomiliki asilimia 31.8 ya hisa za NMB, imepata Sh670 bilioni kutokana na uwekezaji wake katika benki hiyo, ambapo kati ya kiasi hicho, Sh224 bilioni ni gawio.

Sanjari na hilo, aliipongeza Benki ya NMB kwa kuoanisha vipaumbele vyake na maono ya Mhe. Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, hususan katika maeneo ya afya, elimu, ujasiriamali na mazingira.

Katika kusisitiza umuhimu wa mwelekeo huo wa maendeleo, Bw. Mchechu alisema anatamani kuona taasisi zote nchini, ikiwemo za sekta binafsi, zikioanisha mikakati yao na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. 

Alitaja Benki ya NMB kuwa mfano wa taasisi inayotekeleza mwelekeo huo kupitia utendaji wake wa kifedha na usimamizi makini wa mikopo.

“Benki ambayo imekuwa ikitoa wastani wa mikopo ya Sh5.6 trilioni kwa mwaka halafu inakuwa na wastani wa mikopo chechefu wa asilimia 2.5 ni kitu cha ajabu sana, hongereni sana NMB,” alisema.

Aidha, aliwataka wateja na wawekezaji kuendelea kuiamini na kupata huduma kutoka Benki ya NMB, akisisitiza kuwa ni sehemu salama kwa kuwekeza fedha zao.





WAFANYABIASHARA MSIWAUMIZE WANANCHI-DKT. MWIGULU





WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka wafanyabiashara nchini kutowaumiza Watanzania kwa kupandisha bei za bidhaa hususani kipindi hiki cha kuelekea Mwezi Mtukufu wa Ramadhani pamoja na mfungo wa Kwaresma kwa kuwa nchi kwa sasa haina upungufu wa chakula.

Amesema licha ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) nchini kutangaza kuwepo kwa upungufu wa mvua katika maeneo mengi nchini lakini nchi inautoshelevu wa chakula hivyo hakuna sababu ya kupandisha bei za vyakula.

Ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Januari 29, wakati akijibu swali la Nancy Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum katika kipindi cha Maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu. Mbunge huyo alitaka kujua Serikali imejipangaje kuhakikisha nchi inakuwa na utoshelevu wa chakula na kuzuia mfumuko wa bei kuelekea kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na Kwaresma.

“…Kwa sasa tunachakula cha kutosha, mahitaji ya chakula cha akiba kwa nchi ni takribani tani 150,000 na sasa nchi ina zaidi ya tani 400,000 za akiba ya chakula rai ambayo niliitoa hata nilipokutana na wakuu wa mikoa ni kuendelea kuwahamasisha wananchi  kuzingatia ushauri wa aina ya mazao ya kupanda.”

Pia, Waziri Mkuu amewaelekeza Wakuu wa Mikoa yote nchini wawaelimishe wananchi kuendelea kutumia vizuri chakula walichonacho kutokana na tahadhari ya upungufu wa mvua iliyotolewa na TMA. “Wananchi watunze chakula na kuwa na matumizi ya lazima tu, ili kuweza kuwa na akiba.”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameielekeza Wizara ya Afya kuzingatia viwango rasmi vya gharama za huduma na kuharakisha mpango wa kutunga sheria itakayoweka viwango vinavyofanana nchini kote, ili kuondoa hali ya baadhi ya maeneo kuwa na viwango tofauti.

Ametoa maelekezo hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Ushetu, Emmanuel Cherehani ambaye alitaka kupata kauli ya Serikali kuhusu viwango wanavyotozwa wananchi kama gharama ya kumuona daktari ambaye ni mwajiriwa na analipwa mshahara na Serikali.

Waziri Mkuu amesema kwa mujibu wa utaratibu wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, wananchi wanahimizwa kujiunga na mifumo ya bima ili kupunguza changamoto ya kuchangia gharama wanapohitaji huduma hospitalini.

Waziri Mkuu amefafanua kuwa makundi yaliyoainishwa kisheria kama watoto chini ya miaka mitano, wajawazito, wazee na wenye magonjwa ya mlipuko yanaendelea kupata msamaha wa kuchangia gharama hizo.

Kuhusu changamoto ya mifumo hospitalini, Waziri Mkuu amesema Serikali itafuatilia kwa karibu ili kuondoa uzembe na visingizio vinavyochelewesha wagonjwa, huku taasisi husika zikielekezwa kurekebisha mapungufu ya kimfumo kwa kuwa huduma za afya hazipaswi kusubiri.

RAIS SAMIA AZINDUA MPANGO MKAKATI WA KISAYANSI WA KUJENGA UMAHIRI WA KUSOMA, KUANDIKA NA KUHESABU





Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amezindua Mpango Mkakati wa Kisayansi wa Kujenga Umahiri wa Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK), unaolenga kuboresha msingi wa elimu kwa watoto nchini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Rais Samia amesema mpango huo umeandaliwa kwa kutumia ushahidi wa kisayansi na uzoefu wa kitaalamu, ukiweka mkazo katika mbinu bora za ufundishaji, ufuatiliaji wa maendeleo ya wanafunzi, pamoja na kuwajengea walimu uwezo wa kitaalamu unaoendana na mahitaji ya sasa ya elimu.

Ameeleza kuwa umahiri wa kusoma, kuandika na kuhesabu ni nguzo muhimu ya maendeleo ya elimu na taifa kwa ujumla, akisisitiza kuwa watoto wanaopata msingi imara wa KKK hujifunza kwa ufanisi zaidi katika ngazi za juu za elimu na kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Mpango huo pia unatarajiwa kuongeza usawa wa fursa za elimu, kupunguza ufaulu duni wa wanafunzi wa elimu ya awali na msingi, na kuchochea maendeleo endelevu kupitia elimu jumuishi na yenye ubora.

Mhe. Dkt. Samia, ameshiriki kucheza pamoja na kikundi cha ngoma za asili cha wanafunzi wa Shule ya Msingi Kisutu mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), jijini Dar es Salaam, tarehe 29 Januari, 2026.

Uzinduzi wa mpango huo unaakisi dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuwekeza katika elimu kwa vitendo, kwa misingi ya Kazi na Utu, ili kujenga rasilimali watu yenye maarifa, ujuzi na maadili kwa maendeleo ya Taifa.

#KaziNaUtuTunasongaMbele
#ElimuBoraKwaWote
#MaendeleoEndelevu
#Siku100ZaSamia

Rais Dkt. Samia Awasili Addis Ababa Kushiriki Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi wa AU

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewasili katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Bole, Jij...