Wednesday, June 30, 2010

Usajili wa line za simu mwisho leo


WATU wakiwa katika kibanda cha usajili wa namba za simu za mkononi. Zoezi hilo bado linaendelea Jijini Dar es Salaam. Picha na Amran Mnjagila.

*********************************************

Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imesema haitaongeza muda wa kusajili laini za simu za mkononi na kwamba namba yoyote ambayo itakuwa haijasajiliwa itafungiwa kupiga, kupokea simu pamoja na ujumbe wa maandishi (SMS).

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Profesa John Nkoma alisema baada ya saa sita usiku ya Juni 30 namba yoyote ambayo itakuwa haijasajiliwa itafungwa kupiga, kupokea simu pamoja na ujumbe wa maandishi kwa siku 90 hadi Septemba 30 mwaka huu.

“Katika kipindi hiki cha siku 90 endapo mtumiaji atasajili namba yake itafungwa na kwa namba ambazo hazitakuwa zimesajiliwa ifikapo Septemba 30 zitafutwa na kuondolewa kwenye mitandao kabisa,” alisema Nkoma

Alisema Mamlaka hiyo imekubaliana na makampuni ya simu kufanya uhakiki wa usajiliwa laini za simu za wateja kwa kutumia namba 106 kupitia simu za mkononi na kwa wateja wa mitandao iliyoko katika mifumo ya GSM, wateja wanatakiwa kuingiza *106# , wateja wa mfumo wa CDMA watatakiwa kupiga namba hiyo na watapokea taarifa za usajili.

“Hivi karibuni muswada wa sheria ya mawasiliano ya kielektroniki na posta ulipitishwa na Bunge kwa sheria , sheria hiyo inafanya usajili wa namba za simu za mkononi kuwa ni wa lazima kwa mujibu wa sheria hiyo, kuanzia sasa na kutofanya hivyo ni kosa la jinai. Adhabu ni faini na kifungo au vyote kwa pamoja,” alisema Nkoma.

Mwanzoni mwa mwezi Julai mwaka jana mamlaka hiyo ilitoa agizo kuwa namba zote za simu za mkononi zisajiliwe kwa sababu mbalimbali zikiwemo za kuwalinda watumiaji dhidi ya matumizi mabaya ya huduma ya mawasiliano, kuwezesha na kurahisisha utambuzi wa wateja watumiao huduma mbalimbali, kuimarisha usalama wan chi na nk.

Wakizungumza mara baada ya tamko hilo la mkurugenzi wa TCRA, viongozi wa kampuni za simu za mikononi za TTCL, Zain, Tigo, Vodacom, Sasatel, BOL, kwa nyakati tofauti waliilalamikia hatua hiyo ya serikali wakisema kwamba iatawasababishia usumbufu wateja wao na kuwapa hasara kubwa.

Mkurugenzi Mkuu wa Zain Tanzania, Khaled Mehtadi alisema wanakubaliana na mpango huo wa serikali, lakini wanaomba uongezwe muda kwa kuwa kazi ya kukusanya data kutoka maeneo mbalimbali ya nchi ni kubwa na haiwezi kumalizika haraka kutokana na wateja wengi kujitokeza dakika za mwisho.

"Pia alisema kuwa iwapo serikali itaendelea kung'ang'ania uamuzi wake wa kufungia laini basi kampuni hiyo itapata hasara ya kadri ya asilimia 25 kwa kuwa wamewekeza fedha nyingi kulipa mawakala zaidi ya 50,000 nchi nzima na bado kazi haijamalizika,"alisema.

Kaimu Mkuu wa Masoko na Mauzo wa Kampuni ya simu za mikononi ya TTCL, Ernest Nangi alisema kuwa kama walivyo waendeshaji wa kampuni zingine za simu wanaona kuwa bado wanahitaji muda kuweza kukabili changamoto hiyo.

Kwa upande wa kampuni za Tigo kupitia Meneja wa Huduma kwa Wateja, Harieth Rwakatare na Vodacom kupitia Mkurugenzi wake Francois Swart walisema kuwa zoezi hilo ni gumu na kwa maana hiyo wakaitaka serikali na wateja wao kuwa wavumilivu ili waweze kulikamilisha kama inavyopaswa. SOURCE: TCRA

No comments: