Monday, January 12, 2009

Wauza mafuta waanza mgomo


HALI ya upatikanaji wa mafuta jijini, hasa petroli, inazidi kuwa mbaya kutokana na vituo vingi kutouza bidhaa hiyo kwa kile kinachoonekana kuwa, ni njama za waziwazi za wafanyabiashara ya mafuta kuikwamisha serikali kudhibiti upandaji holela wa bei ya nishati hiyo.

Lakini Wizara ya Madini na Nishati imesema inasubiri kupata taarifa kutoka kwa watendaji leo asubuhi, kabla ya kuanza kuchukua hatua kwa wote waliokiuka sheria iliyotangazwa kwenye Gazeti la Serikali kuhusu bei elekezi za mafuta, kwa mujibu wa naibu waziri kwenye wizara hiyo, Adam Malima.

Mafuta ya dizeli ndiyo yanayopatikana bila ya shida kwenye vituo vingi na inauzwa kwa bei iliyotangazwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura). Katika kile kinachoonyesha kutii agizo la Ewura, vituo hivyo vilivyokuwa vikiuza dizeli pekee, vimeweka mabango yanayoonyesha kuwa petroli inauzwa kwa bei ya Sh1,233 ikikaribiana na ya Ewura, ingawa inakuwa haiuzwi.

Hayo yametokea wakati Ewura imetangaza bei mpya ya nishati hizo kwa mikoa 21 ya bara, ikiwa imeongeza senti kadhaa kwenye bei ya awali.

Mgomo huo baridi ulisababisha vituo vichache vilivyokuwa vikiuza petroli kwa bei ya Ewura kufurika magari mengi na watu wenye madumu kwa ajili ya kununua petroli ya ziada, katika wiki ambayo bei ya mafuta katika soko la dunia imezidi kuporomoka na kufikia chini ya dola 39 kwa pipa.

Ewura imewataka wauzaji wa bidhaa hiyo kuuza petroli kwa Sh1,166 kwa lita, ingawa vituo vinavyouza bidhaa hiyo vimekuwa vikiuza kwa Sh1,233 kwa lita, tofauti na bei ambayo ilikuwa ikitumiwa awali na wafanyabiashara hao ambayo ilikuwa kati ya Sh1,450 na Sh1,600 kwa lita ya petroli.

No comments: