📍 Dar es Salaam, Juni 2, 2025
Ofisi ya Msajili wa Hazina imefanikiwa kuongeza makusanyo ya mapato yasiyo ya kodi kwa asilimia 40 ndani ya miezi 11 iliyopita, ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliopita. Mpaka sasa, kiasi cha takribani shilingi bilioni 900 kimekusanywa kutoka taasisi na mashirika ya umma, pamoja na kampuni ambazo Serikali inamiliki hisa.
Akizungumza katika kikao na wahariri wa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam leo, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alisema lengo la mwaka huu wa fedha ni kufikisha shilingi trilioni 1 – jambo ambalo likitimia litakuwa ni mafanikio makubwa na ongezeko la asilimia 30.4 ikilinganishwa na mwaka uliopita ambapo zilikusanywa shilingi bilioni 767.
“Tuna matumaini makubwa ya kufikia trilioni 1. Tunaendelea kufuatilia kwa karibu na tumeweka mifumo bora ya kuhakikisha uwazi na uwajibikaji,” alisema Bw. Mchechu.
Taasisi Zatakiwa Kuwasilisha Gawio Wiki Hii
Bw. Mchechu alitoa wito kwa taasisi zote za umma ambazo bado hazijawasilisha gawio kwa Serikali kuhakikisha zinafanya hivyo kabla ya tarehe 10 Juni 2025, ambayo ni Siku Rasmi ya Gawio kwa Serikali.
“Hakutakuwa na nafasi kwa taasisi ambayo haitatekeleza wajibu wake. Tunahitaji mapato haya kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo,” aliongeza.
Siri ya Mafanikio: TEHAMA na Ufuatiliaji wa Karibu
Ofisi ya Msajili wa Hazina imefanikiwa kuongeza mapato haya kutokana na kuimarisha mifumo ya TEHAMA na ufuatiliaji wa karibu wa michango ya mashirika ya umma.
Miongoni mwa mifumo iliyoboreshwa ni pamoja na:
-
Mfumo wa Mpango na Bajeti (PlanRep),
-
Mfumo wa ERMS,
-
Mfumo wa e-Watumishi,
-
Mfumo wa MUSE – unaosaidia kupata taarifa sahihi za matumizi ya fedha katika taasisi za umma.
Kwa mujibu wa Bw. Mchechu, maboresho haya ni sehemu ya utekelezaji wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan, aliyeagiza mifumo yote ya serikali "isomeane" ili kuongeza uwazi na kupunguza mianya ya upotevu wa fedha.
No comments:
Post a Comment