Roma, Italia – Tarehe 19 Juni 2025
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, amewasili leo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Leonardo da Vinci uliopo Jijini Roma, nchini Italia.
Ziara hii ni kwa ajili ya kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa Ubia wa Maendeleo kati ya Afrika na Serikali ya Italia, maarufu kama Mattei Plan, unaotarajiwa kufanyika kesho, tarehe 20 Juni 2025.
Mkutano huu muhimu unalenga kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Italia katika maeneo ya maendeleo ya kiuchumi, uwekezaji wa kimkakati, nishati, kilimo, elimu, na miundombinu. Tanzania inatarajia kutumia fursa hii kuwasilisha vipaumbele vyake vya maendeleo na kuvutia wawekezaji kutoka Italia kushirikiana katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati nchini.
Makamu wa Rais anatarajiwa kushiriki katika majadiliano ya ngazi ya juu pamoja na viongozi wengine wa Afrika na viongozi wa Serikali ya Italia, ambapo atawasilisha msimamo wa Tanzania kuhusu ushirikiano endelevu na wa kijasiri kati ya pande hizo mbili.
Ziara hii ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Tanzania chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuimarisha diplomasia ya uchumi na kuvutia uwekezaji kwa maendeleo ya taifa.
No comments:
Post a Comment