Monday, April 24, 2017

MEYA WA JIJI ISAYA MWITA ARIDHISHWA NA KASI YA UJENZI WA MRADI OCEAN ROAD

 Mstahiki Meya wa jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita akipata maelekezo kutoka kwa Mhandisi Mzawa baada ya kutembelea mradi huo.
 Mstahiki Meya wa jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita wa kwanza kushoto akiwa kwenye picha ya pamoja na wajumbe wa kamati ya mipango miji na kamati ya huduma ya jamii pamoja na watendaji wa Halmshauri ya jiji wakati alipofanya ziara ya kutembelea mradi wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabia ya nchi pamoja na maboresho ya maeneo ya umma katika fukwe ya Ocean Road.
 Wakandarasi wakiwa kwenye ujenzi
 Mstahiki Meya wa jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita akikagua mradi.
Mhandisi Mzawa akimuelekeza jambo Mstahiki Meya wa jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita wakipolikuwa kwenye eneo la mradi.

NA CHRISTINA MWAGALA,(OMJ) , Dar es Salaam.
MEYA wa jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabia nchi pamoja na maboresho ya maeneo ya umma katika fukwe  ya Ocean Road.
Mradi huo ambao unatarajiwa kumalizika Oktoba mwaka huu, utakuwa ni mahususi kwa wakazi wa jiji la Dar es Salaam kwa ajili kutunza mazingira na kuepukana na mafuriko.
Alifafanua kwamba, mradi huo utahusisha ujenzi wa vyoo na mabenchi ya kupumzikia, utakuwa na jumla ya urefu wa mita 860 kuanzia Hospitali ya Agha-Khani kupitia viwanja vya Ikulu.
“Ukiangalia kwenye fukwe zetu hazina vyoo, hivyo kuwafanya watu wanaokuja kupumzika kukosa sehemu za kwenda kujihifadhi, jambo ambalo sio zuri, ukizingatia jiji letu linapokea wageni kutoka sehemu mbalimbali, ndio maana tumeamua kuleta mradi huu ili kuondoa aibu hii” alifafanua.
Katika ziara hiyo iliyofanyika hivi karibuni, Meya alisema kwamba maeneo ya kupumzikia katika jiji la Dar es Salaam sio rafiki kutokana na ukosefu wa miundombinu hivyo kukamilika kwa mradi huu kutaondoa baadhi ya changamoto zilizopo kwenye maeneo ya hayo.
“Jiji letu ukiangalia kimiundombinu haliko vizuri, mpangilio wake pia hauko vizuri, sasa inapotokea mabadiliko yoyote, wananchi hujikuta kwenye athari kubwa sana, hivyo kupitia mradi huu, utaondoa changamoto hizi” alisema Meya.
“ Ukienda kwenye majiji mengine, utakuta sehemu za fukwe kama hizi , watu wanapumzika, lakini pia ni chanzo cha mapato kwa jiji kwa sababu wanalipia, ila kwetu hapa, imekuwa ni jambo la kawaida, watu wakuja kupumzika kiholela, huu ndio muda wetu wa kulibadilisha jiji letu la Dar es Salaam” aliongeza.
Akizungumzia vikundi mbalimbali ambavyo vilipewa mikopo kwa ajili ya kujiendeleza, Meya Isaya alisisitiza kwamba, bado nafasi zipo kwa vikundi vingine vinavyohitaji mikopo kwa masharti ya uaminifu.
Alifafanua kwamba vikundi vyote ambavyo vitakidhi vigezo, vitapewa mikopo na kwamba lengo kubwa ni kuwakwamua wananchi kiuchumi kupitia vikundi ambavyo vimeamua kujitoa kwa ajili ya kupambana na umasikini.


No comments: