Thursday, September 15, 2011

Meli zingine mbili zazima injini zikitokea bara na Zanzibar

Boti zazimika baharini
Boti ya Sea Star iliyokuwa imebeba abiria 134 na kuanza safari ya kutoka Unguja kuelekea Pemba, ilitumia dakika 20 tu baharini kabla injini yake moja kuzimika muda mfupi kabla ya kufika eneo la Chumbe.

Mkuu wa gati ya abiria ya Malindi Zanzibar, Basha Haji Salehe alisema baada ya kutokea kwa hitilafu hiyo, nahodha wa boti hiyo alipiga simu bandarini na akamriwa akatishe safari.

Afisa wa usafirishaji wa boti hiyo, Mussa Salum Ali alisema hitilafu ilitokana na mafuta yaliyotumika siku hiyo ambayo baadaye walibaini kuwa yalikuwa yamechanganywa na maji.

Alisema tayari wametoa taarifa katika kituo ambacho wamechukua mafuta hayo na uchunguzi unaendelea na kwamba ikithibitika watarejeshewa gharama zao.

Kwa upande wake, Boti ya Sea Bus II iliyokuwa inatoka kisiwani Pemba kuelekea Unguja, ililazimika kukatisha safari kutokana na injini yake moja pia kuzimika.

Boti hiyo iliyokuwa na abiria 138, ilikatisha safari katika kisiwa cha Matumbini na kulazimika kurudi Mkoani ambako iliagizwa boti nyingine ya kampuni hiyo ya Sea Bus III kwa ajili ya kuwasafirisha abiria waliokwama.

No comments: