Luanda, Angola – Aprili 8, 2025
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya Angola, Mhe. João Manuel Gonçalves Lourenço, leo wamekutana na kuzungumza na waandishi wa habari katika mkutano rasmi uliofanyika katika Ikulu ya Luanda, ikiwa ni sehemu ya ziara ya kiserikali ya Dkt. Samia nchini humo.
Katika mkutano huo, viongozi hao wawili walielezea dhamira ya kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na Angola katika nyanja mbalimbali zikiwemo biashara, nishati, miundombinu, elimu, utalii na ulinzi. Wameahidi kuweka mazingira wezeshi kwa sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika kukuza uchumi wa mataifa yote mawili.
“Ziara hii inalenga kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano wa kimkakati kati ya Tanzania na Angola. Tunathamini historia yetu ya pamoja na tunajipanga kushirikiana zaidi kwa maendeleo ya watu wetu,” alisema Rais Dkt. Samia.
Kwa upande wake, Rais Lourenço alimpongeza Rais Samia kwa uongozi wake makini na mchango wake katika kukuza diplomasia ya Afrika. Alieleza kuwa Angola iko tayari kushirikiana na Tanzania katika miradi mikubwa ya maendeleo na biashara ya kikanda.
Mkutano huu umeakisi uhusiano mzuri uliopo kati ya mataifa haya na kuonesha dira ya matumaini kwa mustakabali wa Afrika yenye mshikamano na maendeleo jumuishi.
No comments:
Post a Comment