Tuesday, April 29, 2025

WAZIRI MKUU ATOA WITO KWA WAANDISHI WA HABARI NCHINI


▪️Awataka watumie akili mnemba kama nyenzo na si kikwazo cha uhuru wao▪️

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa ametoa wito kwa Waandishi wa Habari nchini kutumia Akili Mnemba (Artificial Inteligence) kama nyenzo ya kuwawezesha kutekeleza majukumu yao ipasavyo na sio kikwazo cha uhuru wao.

Amesema kuwa katika dunia ya sasa, vyombo vya habari vinakutana na changamoto mpya zinazotokana na maendeleo ya teknolojia, ambapo akili mnemba inachukua nafasi kubwa katika uzalishaji na usambazaji wa habari.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumanne, Aprili 29, 2025) katika Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani, ambayo kitaifa inafanyika Jijini Arusha kwenye Hoteli ya Gran Melia.

Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kuandaa sera maalum ya Akili Mnemba, ambayo itatoa mwongozo wa matumizi yake katika vyombo vya habari ili kuhakikisha kuwa teknolojia hiyo inaendana na misingi ya uhuru wa vyombo vya habari, uwazi, na uadilifu wa uandishi wa habari.  

“Ni ukweli usiopingika kwamba, Akili Mnemba inaweza kuwa msaada mkubwa kwa wanahabari, lakini pia inaweza kuwa chanzo cha changamoto kubwa ikiwa haitatumika kwa busara. Hili linahitaji mjadala wa wazi, sera madhubuti, na ushirikiano wa karibu kati ya sekta zote.”

Amesema Serikali ya Tanzania inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa vyombo vya habari katika maendeleo ya Taifa, kwa kupitia vyombo vya habari, imeweza kuwahabarisha wananchi kuhusu shughuli na mipango ya Serikali, kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika shughuli za kimaendeleo.

Amesema viongozi wanatambua na kuthamini mchango mkubwa wa waandishi wa habari na vyombo vya habari katika kuhabarisha jamii, kuhimiza uwajibikaji na kuimarisha demokrasia nchini. Aidha, wanawahimiza kuendelea kufanya kazi kwa weledi, maadili na uzalendo kwa ajili ya mustakabali wa wananchi na dunia kwa ujumla.

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amesema vyombo vya habari vimekuwa sehemu muhimu katika kutoa elimu kwa wananchi kuhusu masuala mbalimbali, ikiwa ni pamoja na elimu ya uzalishaji, ujasiriamali, na maendeleo ya kijamii.

Waziri Mkuu ameongeza kwa kusema kuwa vyombo vya habari vimekuwa na nafasi kubwa katika kulinda na kudumisha amani, umoja, na mshikamano wa kitaifa na kuchangia kwa kiasi kikubwa katika kuijenga taswira chanya ya Tanzania kimataifa.

Naye, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Profesa Palamagamba Kabudi amesema kuwa Akili Mnemba isiwafanye waandishi wa habari nchini wakafubaa na badala yake wahakikishe wanaitumia vizuri katika utekelezaji wa majukumu yao.

Awali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Gerson Msigwa ametumia fursa hiyo kuwapongeza waandishi wa habari kwa kuendelea kupambania matumaini ya wananchi.

Kauli mbiu ya Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani kwa mwaka 2025 inasema: “Uhabarishaji kwenye Dunia Mpya: Mchango wa Akili Mnemba (AI) katika Uhuru wa Vyombo vya Habari.”


WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA MGENI RASMI KATIKA MAADHIMISHO YA SIKU YA UHURU WA VYOMBO VYA HABARI


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa, leo Aprili 29, 2025, ni mgeni rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari, yanayofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Gran Melia, jijini Arusha.

Maadhimisho haya yamewaleta pamoja wadau mbalimbali wa sekta ya habari kwa lengo la kubadilishana mawazo na kufanya majadiliano ya kina kuhusu fursa na changamoto zinazoikabili sekta ya habari nchini.

Aidha, maadhimisho haya yanatoa fursa ya kuangazia nafasi ya vyombo vya habari katika kuimarisha demokrasia, uwazi, uwajibikaji na haki ya kupata taarifa, sambamba na kuhimiza matumizi ya maadili, weledi na teknolojia ya kisasa katika uandishi wa habari.

Waziri Mkuu anatarajiwa kutoa hotuba muhimu itakayogusa masuala ya sera, mazingira ya kazi kwa wanahabari, usalama wao, na hatua za serikali katika kuhakikisha uhuru na ustawi wa sekta ya habari unalindwa na kuendelezwa.

Serikali inatoa wito kwa wadau wote wa habari na wananchi kwa ujumla kuitumia siku hii kutafakari na kuunga mkono juhudi za kujenga tasnia ya habari iliyo huru, makini na yenye kuzingatia maadili ya taaluma.

Monday, April 28, 2025

WAZIRI WA ARDHI AZINDUA MKUTANO WA WADAU KWA AJILI YA MAREJEO YA MPANGO WA UENDELEZAJI UPYA WA OYSTERBAY NA MASAKI JIJINI DAR ES SALAAM

 







Dar es Salaam, 28 Aprili 2025
Leo, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Deogratius Ndejembi, amezindua rasmi mkutano wa kwanza wa wadau kwa ajili ya marejeo ya mpango wa uendelezaji upya wa eneo la Oysterbay na Masaki jijini Dar es Salaam. Mkutano huu ni sehemu ya mchakato wa utekelezaji wa mpango kabambe wa kuboresha maeneo ya fukwe na mandhari ya asili ya maeneo hayo, na pia kuweka mazingira bora kwa maendeleo ya jiji la Dar es Salaam.

Katika uzinduzi wa mkutano huo, Mhe. Ndejembi alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha wadau wote wanahusishwa kikamilifu katika kutoa maoni yao kwa uwazi na uhuru. Alisema kuwa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, inapaswa kuhakikisha kuwa kila mdau anapata fursa ya kutoa maoni kuhusu utekelezaji wa mpango huo, huku akizingatia maslahi mapana ya jamii, hasa kwa kutambua mabadiliko ya kijamii na kiuchumi yanayotokana na kuhamia kwa makao makuu ya nchi Dodoma.

Nisisitize pia kuhakikisha uendelezaji wa fukwe na mandhari ya asili ya eneo la mpango uzingatie kanuni za uendelevu, uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi,” alisisitiza Mhe. Ndejembi.

Aidha, Mhe. Ndejembi alifafanua kuwa mpango mpya unapaswa kufungamanishwa na mpango kabambe wa maendeleo ya miji uliopo na kuzingatia miongozo ya maendeleo ya miji. Alisema kuwa sekta binafsi inapaswa kupata nafasi stahiki katika utekelezaji wa mpango huu, lakini kwa kufuata miongozo inayohusiana na kulinda haiba ya maeneo haya ya hadhi ya juu.

Waziri Ndejembi alieleza kuwa mpango huu shirikishi umetayarishwa kwa kushirikiana na Halmashauri zote na umejengwa katika Dira ya kuwa na Jiji endelevu lenye ushindani kiuchumi linalotumia rasilimali zake kiufanisi na kuhifadhi mazingira. Aliongeza kuwa mpango huo ni muhimu katika kuboresha miundombinu ya jiji na kukuza ustawi wa wananchi, huku kuhifadhi vyanzo vya maji na mazingira ya maeneo hayo.


UMUHIMU WA MPANGO HUU:

Mpango wa uendelezaji wa Oysterbay na Masaki ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Tanzania kuhakikisha kuwa maeneo ya miji yanaboreshwa kwa kufuata miongozo ya kimataifa ya maendeleo endelevu. Eneo la Oysterbay na Masaki ni miongoni mwa maeneo yenye hadhi ya juu jijini Dar es Salaam, na kuboresha miundombinu yake kutaleta manufaa makubwa kwa wakazi na taifa kwa ujumla.

Kwa kuzingatia mabadiliko ya tabianchi na uhifadhi wa mazingira, mpango huu utajikita katika kuendeleza maeneo haya kwa njia inayozingatia maendeleo endelevu, ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa huduma bora za jamii, uboreshaji wa usafiri, na maendeleo ya kiuchumi.

RAIS MSTAAFU DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE ASHIRIKI KUTOA MAFUNZO KWA MAWAZIRI WA NCHI ZINAZOENDELEA CHUO KIKUU CHA HARVARD, BOSTON, MAREKANI





Boston, Marekani – 28 Aprili 2025

Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, yuko mjini Boston, Marekani, ambako anashiriki katika kutoa mafunzo kwa Mawaziri wa Fedha na Mawaziri wa Mipango kutoka nchi mbalimbali zinazoendelea.

Mafunzo hayo yanafanyika chini ya mpango maalum wa Chuo Kikuu cha Harvard ujulikanao kama Harvard Ministerial Leadership Program, mpango unaolenga kuwawezesha viongozi waandamizi wa serikali kutoka nchi zinazoendelea kuimarisha uongozi, upangaji wa sera, na utekelezaji wa mipango ya maendeleo katika nchi zao.

Katika programu hiyo, Mheshimiwa Dkt. Kikwete amealikwa kama mmoja wa Viongozi Wakuu wa Kitaifa Wastaafu kushiriki kama mkufunzi na mshauri, akitumia tajiriba yake pana katika uongozi wa taifa na ushiriki wa kimataifa kuhamasisha na kuwajengea uwezo viongozi wa kizazi kipya.

Mafunzo haya yanahusisha Mawaziri kutoka sekta muhimu za serikali wakiwemo Mawaziri wa Fedha, Uchumi na Mipango kutoka mataifa ya Afrika, Asia, na Amerika Kusini. Washiriki wanapewa mbinu bora za uongozi, usimamizi wa rasilimali, uboreshaji wa sera, pamoja na kushirikiana kwa karibu na wataalamu wa kimataifa wa uchumi, maendeleo na utawala bora.

Mbali na Rais Mstaafu Dkt. Kikwete, mpango huu pia unashirikisha:

  • Wakuu wa Taasisi za Kimataifa za maendeleo,

  • Wawakilishi wa sekta binafsi,

  • Mabingwa wa masuala ya sera za uchumi na maendeleo kutoka maeneo mbalimbali duniani.

Kupitia ushiriki wake, Mheshimiwa Dkt. Kikwete anaendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kuchangia maendeleo ya uongozi bora duniani, kwa kuhamasisha maadili ya utumishi wa umma, uwajibikaji na uwazi miongoni mwa viongozi wa nchi zinazoendelea.

Programu ya Harvard Ministerial Leadership imekuwa ikihusisha viongozi wa ngazi ya juu kutoka serikalini, ikiwa na lengo la kujenga msingi thabiti wa mageuzi katika sekta za afya, elimu, fedha na uchumi, kwa kutumia uzoefu halisi wa viongozi waliowahi kuongoza mataifa yao kwa mafanikio

RAIS DKT. SAMIA SULUHU HASSAN AZINDUA JENGO LA MAKAO MAKUU YA BENKI YA USHIRIKA TANZANIA JIJINI DODOMA















Dodoma, 28 Aprili 2025 —
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 28 Aprili 2025, amezindua rasmi Jengo la Makao Makuu ya Benki ya Ushirika Tanzania, lililopo katika Jiji la Dodoma.

Akizungumza katika hafla hiyo muhimu iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, sekta ya fedha na vyama vya ushirika, Rais Dkt. Samia amepongeza maendeleo ya sekta ya ushirika nchini na kusisitiza umuhimu wa benki hiyo katika kuwezesha wakulima na wajasiriamali kufikia maendeleo endelevu.

Mara baada ya uzinduzi, Mhe. Rais alitembelea na kukagua mabanda ya maonesho ya masuala ya kilimo yaliyopangwa nje ya Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, ambapo aliweza kujionea bunifu mbalimbali za wakulima na wajasiriamali zinazochangia katika kuimarisha uchumi wa taifa kupitia sekta ya kilimo.

Tukio hili linahitimisha hatua muhimu katika kukuza maendeleo ya kifedha na kiuchumi kwa wanachama wa vyama vya ushirika na jamii kwa ujumla, sambamba na jitihada za Serikali katika kuimarisha sekta ya kilimo na biashara nchini.

Thursday, April 24, 2025

HELIUM ONE YAKAMILISHA MALIPO YA FIDIA KWA WANANCHI WA ITUMBULA

 











● Yalipa fidia ya shilingi zaidi ya milioni 100 kwa wananchi

● Wananchi wafurahishwa na maendeleo ya mradi

● Mradi kutekelezwa kwa kipindi cha zaidi ya miaka 10

Momba, Songwe

Kampuni ya Helium One, inayojihusisha na utafiti na uchimbaji wa gesi ya helium nchini Tanzania, imekamilisha zoezi la ulipaji fidia ya zaidi ya milioni 100 kwa wananchi wa Vijiji vya Itumbula, Lwatwe, Masanyinta, Mkonko na Muungano Wilaya ya Momba mkoani Songwe, waliopisha shughuli za maendeleo ya mradi huo.

Akizungumza leo Aprili 24, 2025 wakati wa ziara ya wataalam kutoka Wizara ya Madini pamoja na waandishi wa habari, Msimamizi katika maeneo ya utafiti na Uendelezaji wa Mradi huo, Emmanuel Ghachocha, alisema kuwa fidia hiyo imelipwa kwa mujibu wa sheria za nchi na imelenga kuwawezesha wananchi waliotoa maeneo yao kwa ajili ya shughuli za utafiti na uchimbaji.

Kwa mujibu wa Ghachocha, mradi huo ulianza rasmi mwaka 2015 kampuni ya Helium One ilipoanzishwa  nakufanikiwa kufanya shughuli zake za kitafiti ikiwamo utafiti kwa njia ya mitetemo na uchimbaji wa visima vya utafiti. Kuanzia mwaka 2021 mpaka 2025 Kampuni ya Helium One  imekwisha chimba visima vinne, ambapo mafanikio makubwa yalionekana kwenye visima vya Itumbula West 1 na Tai 3 vilivyogundulika kuwa na mkusanyiko mkubwa wa gesi ya helium.

Baada ya kufanyika majaribio (Extended Well Testing) Kisima cha Itambula 1 ilionesha kuwa na mkusanyiko wa gesi hiyo ya helium yenye kiwango cha asilimia 7.9%. Utafiti wa kina uliofuata pia ulionesha uwepo wa mkusanyiko wa gesi hiyo ya helium kwa kiwango cha asilimia 5.5 juu ya ardhi ikitokea kisimani.

“Mradi huu unatarajiwa kudumu kwa takribani kipindi cha zaidi ya miaka 10 ya uendelezaji na uzalishaji wa gesi hiyo,” alisema Ghachocha.

Kwa upande wake, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Songwe, Mjiolojia Chone Malembo, alisema kuwa Songwe ina nafasi kubwa ya kuwa kinara wa uzalishaji wa gesi ya helium nchini, jambo ambalo litaongeza mchango wa mkoa huo katika Pato la Taifa kupitia sekta ya madini. 

Sambamba na hapo, Malembo alibainisha kuwa, katika mwaka 2023/2024, mkoa ulikusanya zaidi ya shilingi bilioni 37 kutokana na shughuli za madini na kwa robo ya tatu ya mwaka 2024/2025 ukikusanya zaidi ya bilioni 36, na matarajio ni kufikia bilioni 40 ifikapo mwisho wa mwaka huu wa fedha.

Naye, Mjiolojia kutoka Wizara ya Madini, Venosa Ngowi, ameeleza kuwa,  Tanzania imebarikiwa kuwa Gesi ya helium katika maeneo mbali mbali ikiwemo katika Bonde la Ziwa Rukwa na Bonde la Eyasi Wembere.

Ngowi amefafanua kuwa, gesi hiyo ina matumizi muhimu katika sekta mbalimbali ikiwemo afya (hasa kwenye MRI Scanner), teknolojia ya anga, utafiti wa sayansi ya angahewa, pamoja na usafiri wa anga kama vile roketi na vifaa vya ndege.

Aidha, Wananchi wa eneo husika wameishukuru Serikali na Kampuni ya Helium one kwa kukamilisha kulipa fidia kwa wananchi waliopisha meadi.

“Tulikuwa na wasiwasi mwanzoni kama tutalipwa stahiki zetu, lakini sasa tunashukuru. Tumepata fidia zetu na tunaona namna mradi huu utakavyosaidia maendeleo ya kijiji chetu.”

Mzee Suleiman Mwashiuya, mkazi wa kijiji hicho, amesema: “Huu ni mradi wa kihistoria kwa eneo letu. Mbali na fidia, tunatarajia vijana wetu kupata ajira, na huduma za kijamii kama barabara na maji kuimarika kutokana na uwepo wa mradi.”

Kwa sasa, nchi zinazoongoza kwa uzalishaji wa gesi ya helium duniani ni Marekani, Urusi, Qatar, Saudi Arabia na Algeria

MAKAMU WA RAIS DKT. PHILIP MPANGO AWEKA JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA VIWANJA VYA MICHEZO KILIMANI – ZANZIBAR











Unguja – Zanzibar

Aprili 24, 2025

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango, amesema Serikali zote mbili za Muungano chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi zimejipanga kwa dhati kufanya mageuzi makubwa katika Sekta ya Michezo kwa kuimarisha miundombinu ya kisasa ya michezo na kuwajengea uwezo wataalamu wa michezo ili kukuza vipaji na kuongeza ushindani wa michezo katika ngazi ya kitaifa na kimataifa.

Mhe. Mpango ameyasema hayo leo Aprili 24, 2025 wakati wa Hafla ya Uwekaji Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Viwanja vya Michezo vya Priz katika eneo la Kilimani, Unguja – Zanzibar, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 61 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

"Ujenzi wa viwanja hivi vya michezo ni mwendelezo wa juhudi za Serikali katika kuwekeza kwenye sekta ya michezo ambayo ni sekta ya kimkakati inayokua kwa kasi, na yenye uwezo wa kutoa ajira, kujenga afya ya jamii, na kutoa hamasa kwa mashindano ya kimataifa," alisema Makamu wa Rais.

Aidha, Mhe. Dkt. Mpango alibainisha kuwa Serikali kupitia Wizara husika itaendelea kuhamasisha ushiriki wa jamii katika michezo mbalimbali ikiwemo michezo ya mpira wa miguu, mpira wa pete, riadha, bao, drafti, karata, mieleka, mbio za baskeli, pamoja na michezo ya jadi kama mbio za ngalawa na mchezo wa ng'ombe.

"Serikali inalenga kutoa fursa kwa watoto, vijana, wanafunzi, wanawake na watu wenye ulemavu kushiriki kwenye michezo katika mazingira salama, rafiki na jumuishi," alisisitiza Mhe. Mpango.

Makamu wa Rais pia alieleza kuwa ujenzi wa viwanja hivyo umezingatia mahitaji ya makundi maalum, ikiwa ni pamoja na kupunguza changamoto za udhalilishaji, miundombinu isiyofikika kwa wachezaji wenye mahitaji maalum, na umbali wa kufuata huduma za michezo.

Katika kuadhimisha miaka 61 ya Muungano, Mhe. Mpango alihimiza shughuli za kuhifadhi mazingira kama vile upandaji miti kwenye maeneo ya viwanja vya michezo na matumizi ya nishati safi ya kupikia, sambamba na usafi wa mazingira.

Pia, ametoa wito kwa sekta binafsi kushirikiana na Serikali katika kukuza sekta ya michezo kupitia uanzishaji wa "Green Parks", timu na klabu za michezo, shule maalum za michezo, na programu za ushirikishwaji wa watu wenye mahitaji maalum.

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wa Zanzibar, Mhe. Tabia Maulid Mwita amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imevuka malengo ya Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020 kwa kuwekeza kikamilifu katika miundombinu ya michezo katika visiwa vya Unguja na Pemba. Amesema viwanja hivyo ni fursa muhimu kwa vijana kujenga maisha bora na kuepuka tabia hatarishi kama matumizi ya dawa za kulevya.

PPAA yatoa rai wazabuni kutumia moduli kuwasilisha rufaa

  Na Mwandishi wetu, Dar Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imetoa rai kwa wazabuni kutumia Moduli ya kupokea na kushughulikia malal...