Wednesday, October 06, 2010

RAIS JAKAYA AMTEUA PROFESA WANGWE KUWA MWENYEKITI WA BODI



Benjamin Sawe

Maelezo

Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mheshimiwa Dk.Jakaya Mrisho Kikwete amemteua Profesa Samwel Wangwe kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Elimu Kibaha.
Taarifa iliyotumwa Kwa vyombo vya habari kutoka kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu na Serikali za Mitaa Bibi Maimuna Tarishi imesema Profesa Wangwe ameteuliwa kutokana na Sheria aliyopewa Rais Kikwete katika Sheria ya Mashirika ya umma namba 17 ya mwaka 1969.
Sambamba na uteuzi wa Profesa Wangwe,Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mizengo Pinda pia amewateua Wakurugenzi wa Bodi ya Shirika la Elimu Kibaha.
Kutokana na Mamlaka aliyopewa Waziri Mkuu katika Sheria ya Umma namba 17 ya mwaka 1969 wakurugenzi wa bodi walioteuliwa ni pamoja na Bibi Fatma Kiongosya ambaye ni Mwakilishi wa Wizara ya Afya na Uchumi,Dr Magreth Mhando,Mwakilishi wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.
Wengine ni Bibi Salock Musese kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,Bwana Apenda William Mrinji,kutoka Wizara ya Kilimo,Chakula na Ushirika na Bibi Halima Kihemba ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Kibaha.
Uteuzi wa Mwenyekiti wa Bodi pamoja na Wakurugenzi hao umeanza rasmi tarehe 1/9/2010 na itamaliza muda wake tarehe 31/08/2013

1 comment:

emu-three said...

Tunamtakia kazi njema!