Sunday, August 31, 2008

Mtuhumiwa wa ujambazi akamatwa Dar akiwa amevaa baibui





Na Festo Polea

MTU mmoja ambaye anadaiwa kuwa jambazi maarufu amekamatwa jijini Dar es salaam likiwa amevaa vazi la Baibui ili asijulikane kiraisi akiwa amebeba shoka mgongoni kwa ajili ya kujihami.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, Suleiman Kova, aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa mtuhumiwa huyo wa ujambazi alikamatwa juzi saa 1.30 usiku maeneo ya Kinyerezi Magengeni,jijini Dar es Salaam akiwa ajiandaa kufanya uhalifu.

Kova alisema mtuhumiwa huyo ni mkazi wa Kinyerezi Mwisho na kwamba alianza kufukuzwa baada ya jeshi la polisi kupokea taarifa kutoka kwa wasamaria wema kuwa jambazi linalosakwa na polisi limeonekana katika eneo hilo likiwa limevaa baibui.

Alidai kuwa mtuhumiwa huyo akiwa katika mawindo yake juzi bila kujua kuwa anafuatiliwa, alipoona polisi alianza kukimbia na wananchi wakaanza kumfukuza k na kufanikiwa kumkamata na kuanza kumpa mkong’oto na polisi walifika na kumuokoa.

Kamanda Kova alifafanua kuwa wakati mtuhumiwa anakamatwa alikuwa amevaa baibui na kwamba isingekuwa rahisi kutambua kuwa ni mwanaume.

“Jambazi hilo licha ya kuvaa baibui pia lilikuwa limeficha shoka mgongoni ambayo huitumia kufanikisha mipango yake,” alisema Kova.

Aliongeza kuwa baada ya jambazi hilo kukamatwa ilibainika kuwa amewahi husika katika matukio mbalimbali ya unyang’anyi wa kutumia silaha jijini Dar es Salaam na mikoa ya jirani ya Morogoro na Pwani.

Katika hatua nyingine, wezi wanne ambao wanadaiwa kuiba magari, wamekamatwa jijini wakiwa katika harakati za kubadilisha namba za gari hayo mali.

Kamanda Kova alisema watuhumiwa hao walikamatwa juzi saa 10.30 jioni kwenye baa ya Super Min Wailer, wilayani Temeke ambako waliiba gari hilo siku moja kabla ya kukamatwa.

No comments: