Tuesday, January 10, 2017

RAIS MAGUFULI KUFANYA ZIARA MKOANI SIMIYU

 Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na waandishi wa habari(hawapo pichani) katika mkutano aliotisha kwa lengo la kuwajulisha ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli mkoani Simiyu.
Baadhi ya waandishi wa habari wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtakakatika Mkutano aliotisha kwa lengo la kuwajulisha ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli mkoani Simiyu.

Na Stella Kalinga, Simiyu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli anatarajia kufanya ziara ya siku mbili Mkoani  Simiyu, kuanzia tarehe 11/01/2017 hadi tarehe 12/01/2017.

Akizungumza na Waandishi wa Habari ofisini kwake leo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka amesema, Tarehe 11/01/2017 Rais Magufuli ataweka jiwe la Msingi katika Hospitali ya Mkoa wa Simiyu katika Mtaa wa Nyaumata Halmashauri ya Mji wa Bariadi na kufungua barabara ya Lamadi-Bariadi.

Mtaka amesema baada ya kuweka jiwe la msingi la Hospitali ya Mkoa na kufungua barabara ya Lamadi–Bariadi Mhe. Rais atazungumza na  wananchi wa Bariadi katika Uwanja wa Shule ya Msingi Somanda, mahali lilipo jiwe la ufunguzi wa barabara hiyo.

Aidha, Mtaka ameongeza kuwa Siku ya tarehe 12/01/2017 Mhe.Rais atatembelea kiwanda cha kutengeneza Chaki kilichopo Wilayani Maswa na baadaye ataweka jiwe la msingi katika barabara ya Mwigumbi-Maswa ambapo pia atazungumza na wananchi wa Wilaya ya Maswa.

“Kwa niaba ya Viongozi wa Mkoa wa Simiyu,napenda kuwaalika wananchi wote wa mkoa wetu kujitokeza kwa wingi kumlaki na kumsikiliza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli katika maeneo yote atakayopita”  amesema Mtaka.

No comments: