Monday, December 13, 2010

Kifo hakina huruma kimemchukua Dk Remmy




Mwanamuziki mkongwe na kipenzi cha watu wengi nchini, Ramazani Mtoro Ongala au maarufu kama Dokta Remmy amefariki dunia usiku wa kuamkia leo nyumbani kwake Mbezi.

Habari zilizopatikana katika eneo la msiba leo asubuhi zinasema msiba wa mwanamuziki huyo utakuwapo nyumbani kwake Sinza kwa Remmy jijini Dar es Salaam. Taarifa zaidi za mipango za mazishi tutawaleteeni baadaye.

Dk Remmy Ongala ni mmoja wa wanamuziki waliojipatia umaarufu nchini Tanzana tangu miaka ya 1980 kutokana na umahiri wake katika masuala ya muziki.

Ongala, mwanamuziki mwenye asili ya Kikongo, alizaliwa mwaka 1947 Kisangani huko Jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo (DRC), wakati huo ikijulikana kama Zaire, na ndiko alikoanza kujihusisha na muziki wa dansi.

Alisema kwamba alianza kuupenda muziki tangu akiwa mtoto kwa sababu ni moja ya fani iliyokuwa damuni, pia anaamini Mungu ndiye aliyempatia kipaji mpaka kufikia kupendwa na wapenzi wengi wa muziki.

Mnamo mwaka 1964 ndio alianza rasmi masuala ya muziki akiwa DRC na bendi ya Grandmike.

Mwaka 1967 alijiunga na kundi lingine lililojulikana kama Sakses Bantu ambalo pia lipo hukohuko DRC.

Ongala alikuja nchini katika miaka ya 1970 na kufanikiwa kuendelea na muziki ambapo alianzisha bendi yake ya Super Matimila na kutoa albamu kadhaa kama "Kilio cha Samaki" na nyinginezo.

Mkongwe huyu anakumbukwa na nyimbo zake zilizotikisa ulimwengu wa muziki wa dansi kama 'Mambo kwa Soksi', 'Kifo Hakina huruma', 'Mambo Mbele kwa mbele' na nyinginezo nyingi zilizomfanya ajipatie umaarufu nchini na nje ya nchi.

2 comments:

emu-three said...

Oh, kwake tumetoka na kwake ndio marejeo...mungu amlaze mahala pema peponi!

Anonymous said...

One of the greatest musicians to ever graced the once respectable country Tanzania. Walioziona hizi enzi wakiwa na umri mkubwa wanasema “that was early 80s when economy was still sound, everyone was looking forward to weekend in Dar. Good old days” How I wish I were there! Rest in peace MAESTRO DR ONGALA. By the way this man is more deserving to be honoured with a PhD than Jk, Makongoro, Nagu, Nchimbi and other crooks in the current government.