Monday, February 14, 2011

Precision Air yatua Bukoba


Ndege ya shirika la ndege la Precision juzi Jumamosi, ilitua rasmi katika uwanja wa ndege wa Bukoba na kulakiwa kwa furaha na watu wa mkoa wa Kagera baada ya kuisha kwa matengenezo ya uwanja wa ndege wa Bukoba.

Akizungumza baada ya kutua Bukoba Mkurugenzi Mtendaji wa Precision Air Alfonse Kioko alisema;

“Hii ni fursa na furaha kubwa kwetu kupata nafasi ya kutoa huduma zetu kwa wakazi na wadau wa mkoa wa Kagera baada ya kutokuwepo kwa muda wa mwaka mmoja sasa”

Uzidnuzi wa safari hizo unafuatia kumalizika kwa ukarabati wa kiwanza cha ndege cha Bukoba uliofanywa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania.

“Huduma ya safari itakuwepo kila siku kutoka Dar es Salaam kupitia Mwanza na kutoka Bukoba kwenda maeneo tofauti katika mtandao wetu,” alisema Kioko.

“Tunaanza na bei ya Tshs. 454,000 kwa safari ya kwenda na kurudi,” aliongeza Kioko.

Katika safari za Bukoba Precision Air itatumia ndege aina ya ATR42-500 iliyobatizwa jina la Bukoba kama ishara ya shukrani kwa watu wa Kagera.

Ndege hii inauwezo wa kubeba abiria 48. Ndege ya aina ya ATR42-500 ni ya kisasa kabisa katika soko la ndege kwa sasa. Ndege hii ni mpya kabisa ambayo imefungwa na vifaa vya kisasa na bora zaidi vya michezo ya kufurahisha abiria. Ndege hii ilinunuliwa mnano mwezi wa Nane mwaka jana kwa hiyo ni moja kati ya ndege mpya kabisa za Precision Air.


Kampuni ya ndege ya Precision imedhamiria kutoa huduma bora kwa wateja wake kwa kutumia vifaa vyake vipya na vya kisasa katika soko la biashara ya ndege. Pia kampuni ina mpango wa kupanua mtandao wake nje ya nchi ikiwemo kuanzisha safari kwenda Johannesburg- Afrika Kusini.

Hivi karibuni watanzania watapata nafasi ya kumiliki sehemu ya Precision Air kwa kunua hisa zake katika soko la hisa la Dar es Salaam.

Mnamo mwaka 2006 Kampuni ya Ndege ya Precision na kampuni ya kutengeneza ndege ya ATR walisaini mkataba wa Dola milioni 129 kwa ajili ya ununuzi wa ndege saba mpya katika mpango wake wa kuboresha ndege zake. Ndege ya mwisho kutoka ATR iliwasili Jijini Dar es Salaam mwezi Septemba mwaka jana.

No comments: