Tuesday, June 21, 2011

Madawati ya Saruji darasani


HIVI karibuni asasi ya kiraia ya Twaweza kupitia programu yake ya Uwazi,ilifanya utafiti katika jiji la Dar es Salaam na kubaini upungufu mkubwa wa madawati katika shule za serikali.

Kwa mujibu wa matokeo ya utafiti huo uliohusisha sampuli ya shule za msingi 40 katika manispaa za Temeke, Ilala na Kinondoni, karibu nusu ya shule hizo hazina madawati ya kutosha, hali inayowalazimu wanafunzi kukaa sakafuni.

Na hata katika shule zilizo na madawati, wanafunzi wanalazimika kukaa watano katika dawati moja ambalo kimsingi linapaswa kukaliwa na wanafunzi wasiozidi watatu.

“Katika takribani nusu ya shule(18 kati ya 40), hapakuwa na madawati ya kutosha kwa wanafunzi wote, wengi wanalazimika kukaa chini…..,” inasema sehemu ya ripoti ya utafiti.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, ukosefu wa madawati ni tatizo kubwa katika Shule ya Msingi Kunduchi ambapo, robo tatu ya wanafunzi 1,931 katika shule hiyo hawana madawati. Pichani unaweza kuona ubunifu wa aina yake wa madawati ya saruji yaliyojengewa ndani ya darasa kama suluhisho la tatizo hilo.

No comments: