

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imemtangaza mgombea wa Ubunge kupitia (CCM) Dk Dalaly Kafumu kuwa mshindi wa kiti cha Ubunge wa Jimbo la Igunga, kufuatia uchaguzi mdogo uliofanyika juzi Jumapili.
Kafumu ameshinda kiti hicho kwa kupata kura 26,484 kati ya kura 52,487 halali zilizopigwa, sawa na asilimia 50.4 ya kura hizo, akiwashinda wenzake saba wa vyama vingine ambao pia walishiriki uchaguzi huo.
Msimamizi wa uchaguzi huo, Protase Magayane alimtaja mshindi wa pili katia kinyang’anyiro hicho kuwa ni Joseph Kashindye wa Chadema aleyapata kura 23,260 sawa na asilimia 44.3 akifuatiwa na mgombea wa CUF, Leopold Mahona aliyepata kura 2,104 sawa na asilimia 4.
Wagombea wengine walioshiriki uchaguzi huo na vyama vyao kwenye mabano ni Steven Mahuyi (AFP) aliyepata kura 235, Hassan Rutegama (Chausta) aliyepata kura 182, Said Cheni DP kura 76 na Hemed Ramadhani (SAU) kura 63.
Hata hivyo, CCM kimefanya vibaya katika jimbo la Igunga ikilinganishwa na uchaguzi wa mwaka jana wakati mgombea wake aliyeshinda, Rostam Aziz alipopata ushindi wa kura 35,674 sawa na asilimia 72.7 ya kura halali zilizopigwa.
Rostam aliyejiuzulu nafasi ya ubunge na kutoa nafasi ya kufanyika kwa uchaguzi wa juzi, alimshinda aliyekuwa mgombea wa CUF, Mahona ambaye alipata kura 11, 321 sawa na asilimia 23.1 ya kura halali. Mahona mwaka huu kura zake zimeshuka kwa asilimia 19 ikilinganishwa na matokeo hayo ya mwaka jana.
No comments:
Post a Comment