Monday, October 16, 2006

Tusipokuwa makini, ipo siku tutaitwa 'Jamhuri ya Mwekezaji'

NASHANGAA kwanini Watanzania sisi, tunaosifika kwa uelewa, wema na uadilifu katika sehemu karibu zote ulimwenguni tunaanza kujidanganya na kisha kujibomoa, tena kwa kasi ya kutisha.
Sisemi kwamba huko nyuma tulikuwa hatujidanyanyi na wala hatudanganywi, la hasha! Nafahamu wazi kwamba yameshawahi kutokea matukio ya kudanganywa na au kudanganya.
Lakini, kama yapo yaliyotokea, yalitokea kwa bahati mbaya sana na yalikuwa yakichukuliwa hatua kali na thabiti sana ili kuyarekebisha na kurudisha mambo katika mstari ulionyooka, na hata sasa naamini hili ntakalolieleza baadaye, haliwezi kuvumiliwa likapita hivi hivi.
Wananchi, wavuja jasho na hata viongozi wao walikuwa na uchungu wa kina na nchi yao hawakupenda kudhulumu, kudhulumiwa, kuiba na au kupora kidogo kilichokuwapo na kisha kujilimbikizia hataka hawakihitaji kwa matumizi ya wakati ule.
Sijui kwa sababu walijengewa misingi ya kuheshimiana, kuthaminiana na kujaliana ambayo kwa sasa imeporomoka kwa kasi hivi karibuni au kwa sababu nyingine pia.
Ninasema hivi kwa uchungu kwa sababu ya matukio kadhaa yaliyowahi kutokea huko nyuma, lakini kubwa likiwa ni hili lililotokea hivi karibuni la kuwapo kampuni ‘hewa’ iliyokaribishwa ili kutukodisha majenereta ya kusaidia kuboresha hali ya uzalishaji umeme.
Taarifa tulizozipata majuzi katika gazeti dada ya hili, The Citizen likinukuu vyanzo mbalimbali vya ndani na nje ya nchi, inastusha na inaonyesha kuwa kampuni hiyo, tena kutoka nchi maarufu kama Marekani, haipo katika orodha ya makampuni yanayofanya kazi zake katika Jimbo la Texas.
Na kwamba maelezo ya kampuni hiyo, yanayoonyesha ina makao yake makuu katika Jiji la Houston, jimboni Texas, si ya kweli. Wakati habari hizo zikieleza hivyo, huku kwetu inaonyesha kuwa kampuni hiyo ya Richmond inaonyeshwa kuwa iliingia mkataba na Serikali ya Tanzania Juni 23, mwaka tulio nao, kwa ajili ya kuikodishia mitambo ya kuzalisha umeme wa gesi wa megawati 100 ili kuongeza kiasi hicho kwenye gridi ya taifa.
Katika ziara yake katika makao makuu ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na Kampuni ya uzalishaji wa gesi (Songas), Ubungo Dar es Salaam, Rais Jakaya Kikwete alielezwa kuwa kampuni ya Richmond Development ingeanza kufunga mitambo na kukamilisha baada ya wiki tatu na kwamba umeme wa mitambo hiyo ungeanza kuzalishwa Oktoba 20.
Mradi huo ulikuwa uanze kuzalisha megawati 20 katikati ya mwezi huu na ifikapo Novemba 19, ilitarajiwa kuwa kiasi cha megawati nyingine 80 zingeanza kuzalishwa na kufanya kampuni hiyo izalishe umeme wa dharura wa megawati 100. Kuna maswali mengi ya kujiuliza hapa.
Je, Watanzania, hivi inakuwaje watu tuliowaamini tukawapa madaraka kupitia ofisi za umma ili waweze kutuongoza na kutufanyia masuala yanayohusu maslahi yetu, wakakosa uzalendo namna hii, wakamdanganya hata rais.
Inakuwaje, watu hao wakaweza kula njama na kampuni hewa ambayo tunaambiwa haijasajiliwa wala kutambuliwa si Tanzania tu bali hata Marekani kwenyewe?
Tushukuru Mungu kwamba hawakuwa wamegawiwa kiasi cha mamilioni ya shilingi ya fedha za walipa kodi wanaovuja jasho kutwa kucha katika jamhuri hii ya Watanzania, vinginevyo tungelia na kusaga meno.
Tunafikiri kwamba itakuwa ni jambo la busara kama zitachukuliwa hatua za haraka za kuwawajibisha waliohusika na uzembe huu na kubatilisha mara moja mkataba uliopelekea kampuni hiyo kujipenyeza kijanja nchini mwetu.
Kutokana na mlolongo wa vitendo vinavyofanana na hivi hatuna budi kuwa makini kwa kila tunalolifanya ili kusudi tusije kuangamia na kutumbukia katika matatizo huko mbele ya safari. Nina wasiwasi kweli.
Tusipoangalia na wala kuzingatia na au kuchukulia hatua kali vitendo kama hivi nina hakika kabisa ipo siku tutakuja wananchi wote kuuzwa kwa mwekezaji halafu tutashangaa mikataba iliingiwa nani na kwa maana hiyo hatutakuwa tena na uhuru tutakuwa tukiishi katika nchi ya watu!

3 comments:

Jeff Msangi said...

Charahani,
Habari hii imenishtua sana au zaidi niseme imenitia hasira.Kama kuna kitu ambacho Tanzania bado inakifanyia masihara basi ni cha uwajibikaji.Utamaduni wa uwajibikaji inaelekea kuwa dhana mpya kabisa miongoni mwa viongozi wetu.Inakuwaje mikataba ya namna hii inapitishwa,inagundulika kuwa hewa lakini hakuna anayewajibijika au kuwajibishwa? Nguvu ya wananchi nayo inakuwa wapi?Nguvu ya maandamano ya kupinga mambo inakuwa wapi?Viongozi wa upinzani nao wako wapi?

mzee wa mshitu said...

Hapa bwana Msangi kuna tatizo kubwa, kwanza kwasababu waliopewa mamlaka ya kulinda mali yetu huko maofisini wanatafuna rushwa kama hawana akili njema, ndiyo hawa mahodari wa kutafuna 10%.
Na kwasababu wanapongia mikataba wanakuwa mafichoni hiyo inakuwa mbaya zaidi, wananchi tunakuja kujua wakati mambo yashaharibika, na njia pekee tunayobakiwa nayo ni hii ya kuandamana kama unavyosema.
Huyu bosi wa Nishati na Madini kachefua huko kahamishiwa Afrika Mashariki hivi Rais hajui kwamba huyo ataenda kufanya hivyo hivyo huko na hatimaye tukawa na shirikisho bovu.

NDABULI said...

Haya mambo ya Karl Peters na chifu Mangungo. Sasa hivi sijui tutajitetea nani Hii historia ikija kusomwa na vizazi vijavyo.