Friday, May 11, 2018

WAFANYABIASHARA SOKO LA MAGOMENI WASINYANYASWE-JAFO

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Selemani Jafo akiwa ameshika orodha ya wafanyabiashara wa soko la Magomeni akisisitiza wapewe kipaumbele baada ya soko kukamilika.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Selemani Jafo akiwa na viongozi wa wilaya ya Kinondoni.
Wananchi wa Magomeni wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Selemani Jafo(hayupo pichani).
Muonekano wa soko la Kisasa linalojengwa Magomeni


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Selemani Jafo amemuagiza Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni kukamilisha ndani ya muda ujenzi wa soko Jipya la Kinondoni na kuwapa kipaumbele wafanyabiashara 693 waliopo hivi sasa.
Jafo ametaka wafanyabiashara hao wawe wa kwanza kumpatia maeneo ya Biashara bila kunyanyaswa baada ya ujenzi wa soko hilo jipya la kisasa kukamilika.Akizungumza alipotembelea soko hilo leo, Waziri Jafo amesema kuna kasumba imejengeka ambapo masoko yanapojengwa wale waliokutwa sokoni kabla ya ujenzi huwa watatupwa nje na badala yake watu wengine wapya wenye fedha ndio hupatiwa.
"Nataka hawa wananchi waliopo sasa hapa sokoni ndio wawe watu wa kwanza kukabidhiwa maeneo ya biashara baada ya ujenzi kukamilika," amesisitiza Jafo.Waziri Jafo amemwagia sifa Mbunge wa Jimbo la Kinondoni Maulid Mtulia kwa kuwa ndiye aliyewasilisha kilio cha wanafanyabishara wa Magomeni na serikali imekisikia na kuamua kupeleka fedha.
Pia amewapongeza viongozi wa wilaya ya Kinondoni kwa mshikamano mkubwa chini ya Mkuu wa wilaya yao Ally Hapi na kwamba chini ya Mkuu huyo wilaya hiyo imetulia sana  na inasonga mbele na hakuna migogoro ya viongozi inayoweza kurudisha nyuma maendeleo.
Aidha, Waziri Jafo amempongeza pia kwa kuanza utekelezaji wa utoaji wa mikopo kwa Vijana na wanawake bila Riba.Halmashauri ya wilaya ya Kinondoni imepata Kiasi cha Sh.Bilioni 9 kwa ajili ya ujenzi wa soko hilo kutoka serikali kuu katika mpango wa utekelezaji wa miradi ya kimkakati.

No comments: