Friday, October 10, 2025

ABSA WAJIONEA MAAJABU YA MIRADI YA NHC DAR ES SALAAM

Mkurugenzi Mtendaji wa ABSA Tanzania, Bw. Obedi Laiser akikaribishwa na Bw. Deogratious BatakanwaMeneja wa Mauzo na Masoko wa NHC kwenye mradi wa Kawe 711 jijini Dar es Salaam.

Injinia Grace Musita, Meneja Miradi wa NHC, akitoa maelezo kuhusu maendeleo ya mradi wa Samia Housing Scheme – Kijichi kwa maafisa wa Benki ya Absa Tanzania.


Timu ya wataalamu kutoka Benki ya ABSA Tanzania ikiwa katika ziara maalum katika mradi wa Samia Housing Scheme – Kijichi jijini Dar es Salaam.


Timu ya Benki ya ABSA Tanzania ikiwa katika picha ya pamoja kwenye mradi wa Kawe 711 jijini Dar es Salaam.





Mkurugenzi Mtendaji wa ABSA Tanzania, Bw. Obedi Laiser akiongozana na Bw. Deogratious BatakanwaMeneja wa Mauzo na Masoko wa NHC kwenye mradi wa Kawe 711 jijini Dar es Salaam.

Afisa Mkuu wa Mauzo na Masoko wa NHC, Emmanuel Lyimo akiwaeleza jambo Wataalamu wa Benki ya ABSA walipokuwa kwenye majengo ya Samia Housing Scheme Kawe.

Tarehe 10 Oktoba 2025, timu ya wataalamu kutoka Benki ya ABSA Tanzania imefanya ziara maalum katika miradi mikubwa ya makazi inayotekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) jijini Dar es Salaam — ikiwemo Samia Housing Scheme – Kijichi na Kawe 711 Housing Project.

Lengo la ziara hiyo lilikuwa ni kuwajengea uelewa maafisa wa ABSA kuhusu utekelezaji wa miradi ya NHC, kuonyesha fursa za ununuzi wa nyumba, na kuimarisha ushirikiano katika kusaidia Watanzania kumiliki makazi bora kupitia mikopo ya nyumba.

Ziara hiyo iliongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa ABSA Tanzania, Bw. Obedi Laiser, ambaye hakuficha furaha yake baada ya kujionea kazi kubwa inayofanywa na NHC katika kubadilisha sura ya makazi nchini.

“Tumepata fursa nzuri ya kujifunza na kujionea kazi kubwa inayofanywa na NHC. Nyumba hizi ni za kisasa, zenye ubora wa juu na zitachangia kwa kiasi kikubwa kupunguza changamoto ya uhaba wa makazi nchini. Tunawapongeza NHC kwa ubunifu na ufanisi mkubwa katika utekelezaji wa miradi hii,” alisema Bw. Laiser.

Aidha, alisisitiza kuwa ubora wa miradi ya NHC unaendana kikamilifu na falsafa ya chapa ya ABSA inayosema “Hadithi yako ina thamani”, akifafanua kuwa nyumba hizo zinaakisi maisha halisi ya Watanzania na ndoto zao za kumiliki makazi bora.

Kwa upande wa NHC, Meneja Miradi, Injinia Grace Musita, aliyeongoza maelezo kwa niaba ya Shirika, alieleza kuwa miradi ya Samia Housing na Kawe 711 ni sehemu ya utekelezaji wa dira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“NHC imejipanga kuhakikisha kila Mtanzania anapata makazi bora, salama na ya kisasa. Miradi hii inajengwa kwa kutumia teknolojia za kisasa, ubora wa hali ya juu na kwa kuzingatia mazingira rafiki,” alisema Injinia Musita.

Naye Bw. Deogratious Batakanwa, Meneja wa Mauzo na Masoko wa NHC, aliishukuru Benki ya ABSA kwa ushirikiano wa muda mrefu katika kusaidia ujenzi na mauzo ya nyumba za Shirika.

“Tunathamini ushirikiano wa ABSA kwa kutuwezesha kifedha katika ujenzi wa miradi yetu, na pia kwa kuwasaidia wateja wetu kupata mikopo ya nyumba. Ushirikiano huu ni mfano bora wa taasisi za kifedha na sekta ya makazi kufanya kazi kwa pamoja kwa manufaa ya Watanzania,” alisema Bw. Batakanwa.

Ziara hiyo imetajwa kuwa ni mwanzo wa hatua mpya ya ushirikiano wa kimkakati kati ya NHC na ABSA Tanzania, ikilenga kuendeleza jitihada za kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata makazi bora, yenye hadhi na ya gharama nafuu.

Kupitia miradi kama Samia Housing Scheme – Kijichi na Kawe 711, NHC inaendelea kuthibitisha uwezo wake wa kubadilisha mandhari ya miji ya Tanzania na kuwa nguzo muhimu katika ujenzi wa Taifa lenye ustawi wa makazi bora kwa wote.

🏠 NHC – Tunajenga Taifa, Tunakuza Ndoto.
#NHC #ABSA #Kawe711 #SamiaHousing #MakaziBora #UshirikianoWaMaendeleo #TunajengaTaifa #DarEsSalaam

 

No comments:

ABSA WAJIONEA MAAJABU YA MIRADI YA NHC DAR ES SALAAM

Mkurugenzi Mtendaji wa ABSA Tanzania, Bw. Obedi Laiser akikaribishwa na  Bw. Deogratious Batakanwa ,  Meneja wa Mauzo na Masoko wa NHC kweny...