Saturday, September 09, 2006

Ipo siku tutakuja kununua mchele gengeni kwa dola

Benki Kuu chimbuko na mdhibiti mkuu wa pesa.

MAJUZI gazeti la Mwananchi liliripoti kuporomoka kwa kasi kwa sarafu ya Tanzania, hali ambayo lilielezwa kuwa unazusha hofu kama mkakati wa kuwapatia Watanzania maisha yenye neema zaidi.

Habari za kuporomoka kwa shilingi na kupanda kwa dola ya Marekani zimeleta si tu hofu, bali balaa kwa wananchi wa kawaida.

Kwanza kwa kuwa wajanja wachache wanaojua kucheza na mahesabu wameanza kuutumia mwanya huu kujipatia mamilioni ya shilingi kutokana na ujinga wa wengi.

Wanauza bidhaa walizonunua mwaka au miezi mingi iliyopita nje ya nchi kwa thamani ya sasa ya dola badala ya kutumia bei ya chini ya wakati walipopata bidhaa hizo.

Mtindo huu wa kuthaminisha bidhaa ulizonunua zamani kwa bei ya sasa ni dhahiri kwamba ni wizi usiofaa na unawanyonya wengine kinyume kabisa cha utaratibu

Vyovyote iwavyo, lakini kwa mantiki ndogo tu ni dhahiri kwamba iwapo utanunua bidhaa kwa fedha za kigeni kuna hatari kubwa sana ya kupata hasara, hasa kama pesa haina nguvu kama hii yetu.

Kwa hapa kwetu kwa kuwa wananchi wengi wanapata pesa baada ya kufanya kazi, ambapo hulipwa au kwa lugha nyingine hufidiwa nguvu zao iwe zaidi au kidogo, lakini mara nyingi hupunjwa na huzitumia kwaajili ya matumizi ya kila siku maishani mwao.

Inakuwa vipi kwa vijisenti hivyo eti uende kuvibadilisha hivi utapasa senti ngapi, ili uweze kununua bidhaa unayotaka? Tuachane na mtindo huu unatufanya kujitia uzungu zaidi huku tunajibomoa!

Ndiyo nakubali kwamba wapo wenye vijiakiba, lakini ni wachache sana ambao hawatumii fedha zao kabisa, ambao huziwekeza ili ziweze kuongezeka.

Hivi kwanini huduma na bidhaa ziuzwe kwa dola? Kwanini printers zilizonunuliwa mwaka juzi ziuzwe kwa thamani ya sasa ya dola? Kwa mtindo huu ipo siku wafanyabiashara wa mchele na viazi watauza bidhaa hiyo kwa dola na watatoa visingizio vingi tu. Hatutakubali!

Nafikiri kinatakiwa kifanyike kitu ili kuweza kunusuru balaa hili, sababu kama kunakuwa na uchezeaji akili za watu na kisha kuwapunja kwa staili hii inakuwa siyo sawa.

Fedha hasa noti ni utambulisho muhimu sana wa taifa na ni kitu kikubwa kinachowaunganisha wananchi wa taifa husika na hivyo kuondoa mianya ya kufanyika kwa biashara isiyo halali.

Muda si mrefu uliopita, tulikuwa tukinunua muda wa maongezi katika simu kwa kutumia fedha zetu lakini tulikuwa tukiuthaminisha kwa dola. Hivi nini dola, mbona Wapakistan, Wahindi, Wachina wanajivunia vya kwao kwanini isiwe sisi?

Alinifurahisha Waziri mmoja wa Pakistan kipindi hicho nikiwa New York, Marekani hotelini, Waziri yule alifika katika jiji lile kuhudhuria kikao kimojawapo cha Umoja wa Mataifa.

Alipotakiwa alipie gharama za chumba akatoa bulungutu la rupia za kwao. Mhudumu alimshangaa sana, lakini naye waziri yule alimshangaa sana yule mhudumu.

Kila mmoja kati yao alikuwa akijifanya kuwa yeye zaidi. Yule Waziri akamuona yule mhudumu mpuuzi, lakini naye mhudumu akamuona waziri mshamba, lakini ukweli wa mambo waziri alionyesha uzalendo na utaifa wa hali ya juu.

Hata hivvyo hatimaye waziri alizunguka akaenda kubadilisha bulungutu la rupia zake, lakini bado alikuwa akilalamika kwanini rupia za kwao hazitumiki Marekani!

Hadithi hii ingepaswa nasi tukawa angalau tunaifikiria hivi kwa mfano hawa wanaojifanya biashara ni huria kwanini tunalazimika tukiwa kwao kutumia pesa zao na kwanini siyo zetu.

Hata hivyo kikubwa kinachotakiwa ni kama serikali yetu inavyofanya sasa kuwawezesha wananchi mmoja mmoja wawe na uwezo wa kujimudu kujiendesha kimaisha vinginevyo aina hii ya unyonyaji itatumaliza!

2 comments:

mwandani said...

Mzee wa mshitu, unaniambia kuwa watanzania wanatumia dola za kimarekani mitaani bongo? - au tu wana mtindo wa kutafsiri sarafu zetu katika dola kama njia ya kujikweza kwamba wana maarifa ya kujua thamani kimtindo?

Halafu pia unaniambia: Ndio nakubali kuna wenye vijiakiba, lakini ni wachache sana.

serikali yetu inadai kuwa masikini chini ya kiwango cha umasikini kilichowekwa na taifa ni asilimia 41 tu ya watanzania(kwa mujibu wa takwimu za benki ya Afrika 2006)

Nikipata wakati nitapenda kupeleleza umasikini kama inavyosema serikali maana yake nini. ninavyofahamu miye mtu asiye maskini anaweza kujimudu tena na kutunza akiba ikibidi.

halafu umeandika kuwa serikali iko kwenye njia sawa hivi sasa inapotumia:
"Staili ya kuwawezesha mwananchi mmoja mmoja wawe na uwezo wa kujimudu kujienshea maisha…"

Tafadhali nihabarishe ni staili gani hiyo?

mzee wa mshitu said...

aahhh kweli ndugu yangu Tungaraza hapo umeninyooshea sentesi ni kwamba wanatumia dola za kimarekani kujikweza thanx very much.
Kuanzia hapo sasa naweza kuendelea ni kwamba uzungu unatuzungusha hapa kila anayejifanya kujua mengi kiulaya ulaya ndo anayejifanya mjuzi na anajiona mjanja ndiyo hii essence ya matumizi ya dola inapokuja.
Yess maana ya umasikini kwa serikali sijui imelenga nini lakini nachoweza kufahamu ni kwamba mambo yanakwenda kiupogo upogo tunajitahidi lakini ndiyo hivyo inabidi kukomaa nao. EEEEEHHHH hiii staili ya kumuwezesha 'mtanzania' mmoja mmoja ina utata lakini naamini ipo siku tutakuwa katika njia sahihi tartiibu tutafika tu!