Tuesday, May 16, 2006

Huruma zetu Wabongo tumezificha wapi

Bibi Kikongwe Asha Msawila wa Kijiji cha Mkamba, Morogoro akitoka nje ya kasri lake, hebu fikiria haya ndo maisha. Picha hii imepigwa na Kaanaeli Kaale.

KWETU Tanzania, kidesturi unapoamka hakuna siku utaamka ukamsalimu jirani au ndugu yako wa karibu akakujibu kuwa mambo ni safi sana, ikitokea hivyo huwa ni nadra mno.

Unapotoa salamu, moja kwa moja tegemea majibu kama: Habari mbaya, Tunaumwa umwa, Alhamdulillahi, Tunaendelea hivyo hivyo na mengine mengi. Ndugu zangu kina Makene, Ndesanjo, Mwaipopo,Jeff, na Tungaraza nadhani bado wanaikumbuka hii hali.

Inawezekana tukajibu hivyo kwa vile huwa tunakabiliwa na matatizo. Wala sina maana kwamba tunapokuwa na matatizo, basi tusiseme hivyo, lakini sijui ni asili yetu kujisikia wanyonge au ni hali ya maisha ndiyoinayotupeleka hivyo, au ni walalamishi!

Wenzetu wa ughaibuni hapa niseme kabisa weupe ni wawazi wanapokuwa na unafuu wa maisha husema kabisa mambo ni safi, mambo ni barabara , murua na kila kitu cha namna hiyo, ni safi sana. Pengine ni kwa sababu walishatunyonya katika mfumo usio wa haki.

Lakini, hili la unyonge si la kulipuuzia hata kidogo, hebu tujiulize unyonge wetu huu unatokana na nini je ni uvivu wetu tu, na au ni uzembe?

Kama wanaojituma wanafanya kazi kwa bidii, damu au hata jasho, kwa machozi na mabavu wanafanya hivyo, lakini kila kukicha wanabakia pale pale hawasongi mbele, tujiulize, hivi tatizo ni nini hasa.

Zipo taarifa kwamba wananchi wengi sasa wamefuta baadhi ya milo ya siku, utakuta au wanakula chakula cha mchana pekee, halafu ndiyo basi tena.

Au wanakula chakula cha usiku pekee halafu ndiyo siku inakwisha au chakula kinasogezwa mpaka jioni halafu siku imekwenda hivyo.

Watafanyaje wakati bei ya mchele imepanda mara dufu hivi sasa inakimbilia Sh1,300 au zaidi wakati muda mfupi uliopita ilikuwa Sh600, mkaa ambao ndiyo kimbilio la wengi umefikia Sh22,000 kwa gunia wakati ulikuwa chini ya 10,000, maharage ya soya nayo hayashikiki wakati kipato kimebakia pale pale au kushuka.

Kwa mahesabu ya kawaida tu uchukulie mwananchi anayeishi mjini na kisha anafanya pengine kazi na mara nyingi ni kibarua analipwa Sh 60,000, kwa maisha ya sasa atafanya nini ili aweze kujimudu wakati kila kitu kimepaa.

Nauli ya daladala inazidi kupaa ilikuwa sh. 150 sasa inakimbilia 250 hadi 400, hii ina maana kwamba ikiwa ni kwa kwenda na kurudi ni kati ya Sh 500 na 1,000 hiyo kama mhusika ana usafiri wa moja kwa moja.

Hii ikijumlishwa kwa mwezi inamaanisha kuwa nusu ya kipato itaondoka kwa usafiri tu, bado chakula, bado watoto hawajaenda shule, bado hawajaugua na bado mlolongo mrefu wa vitu vinavyohitajika kwa maisha ya kila siku.

Yote hii inafanyika kwa kivuli kwamba bei ya mafuta imepanda, ukosefu wa mvua na umeme, ingawa sasa tatizo la ukosefu wa mvua limeondoka na limeingia jingine la maafa ya mafuriko.

Haya yote yanatoa kitu kinachoitwa,Mshtuko wa moyo kwa wakazi siyo wa mijini tu bali hata wale wa vijijini sasa, ule wakati wa kuishi bila senti kwa muda hata wa miezi sita unakwisha na sasa kila kitu pesa tena pesa nyingi.

Mfumuko huu wa bei umefanya watu wengi wawe na mawazo kama ya rafiki yangu mmoja aliyeibuka na aina yake ya kaulimbiu, yeye ameigeuza kauli mbiu akisema : Ari Mpya, Kasi mpya, maisha magumu kwa kila Mtanzania.

Kwa ufupi, maisha ya Mtanzania halisi maisha yake yamekuwa taabu tupu wakati hakuna dalili zozote za kuleta matumaini kesho itakuwa vipi! Yaani, inakuwa afadhali jana kuliko leo.

Kuna watu miongoni mwetu wameshakata tamaa ya kaulimbiu au maneno matamu matamu, kwa kuwa wanaona kila mtu amepotea, kila mtu anajali maisha yake binafsi na hakuna anayewatetea.

Watu kama hawa ni wengi siyo wa kuhesabu wanalalamika chini chini kwani hawana pa kusemea wanaishia kunong’ona na siku zinatokomea bila huruma.

Wakati kuna wajanja wanabugia au kula raha kwa fujo, wanawanyonya damu hawa hawa wenye kipato cha chini, wanaopata kipato kwa kutukanwa na kunyanyaswa.

Hata kama ni wachache, hao hawana budi wadhibitiwe ili wapunguze unyonyaji huo, wanatumaliza wenzao taratibu, kwa mfano kuna haja gani ya kupanga njama kuuza vitu kwa bei ya juu wakati mnaouza mnanunua shambani kwa bei ya chini.

Mbona mahindi yapo mengi. Mbona mchele upo mwingi. Mbona mafuta mnanunua kwa bei ya chini kwanini muuze kwa bei ya juu. Hata kama ni soko huria hii itakuwa ni soko hulia. Lile la kihuni, ambalo halina huruma.

7 comments:

Jeff Msangi said...

Charahani,
Umechambua matatizo ya watanzania barabara kabisa.Hiyo ndio hali halisi ya mtanzania wa kawaida ambayo haiihitaji research yoyote ili UN,IMF,WB na wengineo kuyaelewa.
Hili la kulalama ni tatizo la kisaikolojia na baya sana.You are who you think you are,you are in the condition that you think you are nk.Huo ndio ukweli.Hebu fanya zoezi hili Charahani,kesho kila mtu utakayesalimiana naye mwambie mambo safi sana mpaka mwenyewe unashangaa.Kisha baada ya hapo sikiliza ari mpya inayoibuka moyoni mwako.Pia usiache kuangalia jinsi watu wanavyokushangaa.

boniphace said...

charahani, wanyinyaji hawako mbali kabisa, inawezekanje serikali ikagawa milioni 20 kwa kila mbunge bure kabisa tena kipindi hiki cha njaa. Tumezibwa midomo hatuoni kabisa wakati vijana wale wanaotafuta elimu kule vyuo vya juu wanmapewa mikopo ya vimilioni vitatu, sasa vipi hawa wanaopewa pesa zote hizo bure? Nilipita kuongeza hoja hiyo kaka, tuendelee kujadili.

mwandani said...

Hii hali ngumu mbona iko tangu mwaka 79? Tena sasa nasikia ndio mapato ya taifa yanapanda kwa asilimia tano tano kila mwaka,
Tatizo nadhani tangu wakati huo limekuwa ni vipaumbele. Msisitizo ungewekwa panapotakiwa kila mwaka, kila siku - tangu 79 mpaka leo mambo yangeshaanza kuwa bora kwa kiasi kadhaa.
Tumeridhika na mambo - hata katika dhiki tunaafiki tu.
Na viongozi pia wanajua fika nini cha kufanya, tena hata hawezi kuwaza mara mbili, kwa sababu siku zote mambo yamekuwa kama yalivyo.
Inabidi kutia fikra mpya.

Hauwezi kuwa huru mpaka uwe na uhuru.

Ukiwa umefungwa na mawazo na mazingira ya 'kizamani' basi tutabaki nyuma nyuma tu.

mzee wa mshitu said...

Jeff unachosema ni kweli lakini ukisema mambo safi jiandae kuwa na msururu wa watu kukupinga mizinga, au hata kukuandama, bado tuna matata ndani ya fikra zetu.
Makene hiki umenikimbusha hivi inakuwaje eti wanasema sisi ni masikini wakati kuna 'majitu' yanakopeshwa kiaina aina pesa za kodi za baba na mama zetu na hata sisi wenyewe huku wenyewe tukishangaa.
Tungaraza hii kuridhika unakokusema ndiko kunakotuponza tunaishia kila mmoja kuwa aidha na biashara za aina moja, mawazo mgando na ujanja wa kuandika proposal kuomba hela kwa wafadhili, hii haina tofauti na ombaomba wa pale Ubungo.

Reggy's said...

Nimemwangalia sana huyo bibi. Nilidhani utamjadili kama yeye lakini hukumgusa kabisa, bali ukajadili hali kwa ujumla. kwa jinsi alivyo huyu bibi kwa kulinganisha na wengine wengi ninaowajua wa vijijini, ana unafuu mkubwa sana. Kwanza ana vitenge vizuri amejisetiri sawasawa, pili ana kandambili mguuni; na tatu, nyumba yake ya udongo inaonekana ni imara. Wapo watu wanaishi katika nyumba zilizowekewa egemeo ili zisianguke, wapo wanaishi katika tembe hapa Dodoma na mvua ikinyesha kubwa ndio kiama chao. wapo wanaolala kwa kuzungushia magunia/ visalphate. Angalia hata watumishi wa umma, mfano polisi na askari magereza ambao wanaishi katika nyumba za full suti (kuta zote badi), nimeona za Askari Magereza Ukonga katika gazeti moja ziko kama mabanda ya kuku. Shangaa! Wapo Watz ambao tangu wazaliwe hawajawahi kuvaa kandambili, achilia mbali kiatu. wapo ambao kuvaa kwao ni taabu, wapo ambao kula yao ni shida miaka yote, si tu katika kipindi cha njaa ya jumla kama ya mwaka huu. Kwa ujumla kwa sasa ni maisha magumu kwa kila Mtanzania. lakini salmu yetu vijana inabaki kuwa: MAMBO na jibu la POA/SAFI
siku njema

mzee wa mshitu said...

Regnald hapo umenena ni kweli huyu ana unafuu sana wengine hata nguo na hata nyumba hawana wanalala kwenye maboksi, hiyo ni kweli nilioverlook ahsante musee

mloyi said...

Nimeiona hiyo hali ipo na inazidi kuongezeka, kizuri huyu bibi yetu ananguvu za asili ndiyo maana tunamuona hivyo. pengine angekuwa hoi kutokana na chakula anachokula, sijui lama ananieli alikumbuka kumuuliza lini alikula chakula cha mwisho na anakula mara ngapi kwa siku na nini? na anatoa wapi? Nadhani mlioko huko ughaibuni mngepigia simu wazazi wenu kuwauliza hali zao.
Sisi tuliobahatika kufika mlimani mishahara yetu inatufikisha tarehe 13-18 ya mwezi. je? wale waliokuwa wanatumwa kuangalia pombe kama zimeiva na wazazi wao wanaishiji? Tatizo ni kubwa.