Sunday, April 06, 2025

WAZIRI MKUU AWATAKA MABALOZI KUISHI FALSAFA ZA RAIS DKT. SAMIA




WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amewataka mabalozi kuiishi falsafa ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha mahusiano na kukuza diplomasia ya kiuchumi kati ya Tanzania na mataifa mbalimbali duniani.

Mheshimiwa Majaliwa amesema kufanya hivyo kutaiwezesha Tanzania kuvutia wawekezaji katika sekta mbalimbali zikiwemo za viwanda, kilimo, biashara pamoja na kupata masoko ya bidhaa zinazozalishwa nchini.

Ameyasema hayo leo (Jumapili, Aprili 6, 2025) alipokutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa Balozi Hamad Khamis Hamad Balozi wa Tanzania nchini Msumbuji na Mheshimiwa Balozi Mobhare Matinyi, Balozi wa Tanzania nchini Sweden.

Mheshimiwa Majaliwa amesema Serikali ina mategemeo makubwa na mabalozi hao, hivyo wanapaswa kwenda kuendeleza mahusiano mazuri ya muda mrefu yaliyopo baina ya Tanzania na mataifa hayo.

Waziri Mkuu amesema pamoja na mambo mengine mabalozi hao wanatakiwa wahakikishe wanasimamia vizuri matumizi ya fedha katika ofisi zao pamoja na kuanzisha au kuendeleza madarasa ya kufundisha lugha ya kiswahili.

MRADI WA KUFUA UMEME WA JNHPP WAKAMILIKA RASMI: DKT BITEKO

 









-Asema ni ndoto ya watanzania,awataka wategemee umeme wa uhakika

-Asisitiza kazi iliyobaki ni kuimarisha miundombinu ya kuwafikishia wananchi umeme

-Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Misri kuuzindua rasmi

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mhe. Dkt. Doto Biteko amewataka Watanzania kutegemea kupata umeme wa uhakika baada ya Mradi wa kufua umeme kutoka Bwawa la Julius Nyerere uliokuwa ukisubiriwa kwa shauku kubwa na Watanzania kukamilika rasmi.

Waziri Biteko ameyasema hayo leo April 5, 2025 baada ya kutembelea Mradi huo akiwa ameambatana na Mawaziri ambao ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mha. Hamadi Masauni.

Amesema hivi sasa mitambo yote tisa inafanya kazi ambapo amefafanua kuwa kukamilika kwa Mradi huo kumechangiwa na maono ya Rais wa Awamu ya Sita Mhe. Dokta Samia Suluhu Hassan ambaye aliupokea Mradi ukiwa katika asilimia 33 ya utekelezaji wake na ndani ya kipindi cha miaka minne ya Uongozi wake ameweza kuukamilisha Mradi.

‘’Tumekuja leo tukiwa na furaha kubwa kwamba mitambo yote tisa imekamilika inazalisha umeme na nina furahi kuwajulisha Watanzania kuwa ile ndoto ya kuwa na umeme kutoka kwenye chanzo hiki kikubwa barani Afrika imekamilika, kazi iliyobaki ni kuimarisha miundombinu ya kuwafikishia watanzania umeme’’ Alisisitiza Dkt Biteko.

Dkt. Biteko amesema kutokana na nchi kuwa na uwezo wa kuzalisha umeme kwa kiwango kikubwa sasa Serikali iko katika mchakato wa kukamilisha mazungumzo na nchi ya Zambia kwa ajili ya kuwauzia umeme na tayari njia ya umeme ya kuunganisha nchi hizo mbili inajengwa.

‘’Kile ambacho tumekua tukikiongea miaka mingi kwamba Tanzania itakuwa na uwezo wa kuuza umeme nje ya nchi sasa imetimia katika kipindi hiki cha Serikali ya awamu ya sita baada ya msukumo mkubwa wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan tuna mshukuru sana Mheshimiwa Rais’’

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Mhe.Profesa Kitila Mkumbo amesema kukamilika kwa Mradi huu ni ukombozi wa kiuchumi huku Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Hamadi Masaun amesema Tanzania imeingia katika historia barani Afrika ambapo amesema kazi kubwa iliyobaki ni kutunza vyanzo vya maji ili kuulinda Mradi.

Katika hatua nyingine Mhe Dkt Doto Biiteko amelishukuru Shirika la umeme Tanzania TANESCO kwa utekelezaji wa Mradi kwa kiwango cha kimataifa na kumpongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo Mha. Gissima Nyamo-Hanga kwa usimamizi na jitihada zake katika kusimamia miradi mbalimbali ya umeme.

Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere umegharimu zaidi ya Shilingi Trilioni 6.5 ambapo mpaka sasa serikali imeshalipa zaidi ya asilimia 99.5.

Friday, April 04, 2025

MAKAMU WA RAIS MHE. DKT. PHILIP MPANGO AONGOZA KIKAO CHA 15 CHA KAMATI YA PAMOJA YA MASUALA YA MUUNGANO




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango, ameongoza Kikao cha 15 cha Kamati ya Pamoja kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) cha kushughulikia masuala ya Muungano. Kikao hiki kimefanyika leo, tarehe 04 Aprili 2025, katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete Ikulu, Jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo umejikita katika kujadili na kutafuta suluhisho kwa changamoto mbalimbali zinazohusu Muungano, huku ukilenga kuimarisha mshikamano, ushirikiano, na maendeleo kati ya pande mbili za Muungano. Viongozi wa pande zote mbili wameonyesha dhamira ya dhati ya kuhakikisha masuala yanayohusu Muungano yanashughulikiwa kwa ufanisi na kwa manufaa ya Watanzania wote.

MTAA WA MAKANGIRA DAR ES SALAAM KUPANGWA NA KUENDELEZWA UPYA











Serikali imeanzisha Programu ya kuendeleza miji iliyochakaa kwa kuboresha makazi pasipo kuwahamisha mwananchi hata mmoja kutoka katika eneo analomiliki.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe.  Deogratius Ndejembi Aprili 04, 2025 katika mkutano wa hadhara na wananchi wa mtaa wa Makangira, Kata ya Msasani wilaya ya Kinondoni jijini Dar es salaam wakati akitambulisha program hiyo.

“Katika program hii, hakuna mwananchi hata mmoja atahamishwa, tumedhamiria kuboresha makazi yenu pasipo kuhamishwa kwa mwananchi hata mmoja kutoka katika eneo analoishi isipokuwa kwa wananchi wachache ambao utekelezaji wa mradi utakapoanza, Serikali itawapangishia nyumba wakati mradi ukiendelea kutekelezwa na baada ya kukamilika kwa mradi mtarejea katika maeneo yenu” amesema Waziri Ndejembi. 

Waziri Ndejembi amesema kwa kuzingatia matakwa Sera ya Taifa ya mwaka 1995 Toleo la mwaka 2023 ambayo imezinduliwa hivi karibuni na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Programu hiyo maalum ya uendelezaji upya maeneo chakavu katika miji ili kukabiliana na changamoto za ukosefu wa huduma za msingi, miundombinu, makazi duni au chakavu, ukosefu wa mifumo ya maji taka na uwepo wa changamoto ya taka ngumu zinapelekea uchafuzi wa mazingira. 

Wizara imetambua jumla ya maeneo 111 katika mikoa 24 ambapo kwa kuanzia Programu hiyo itatekelezwa katika majiji ya Arusha, Dar es salaam, Dodoma, Mwanza Mbeya na Tanga.

Waziri Ndejembi amesema program hiyo ina faida lukuki ikiwemo upatikanaji wa ardhi iliyopangwa kwa matumizi mbalimbali ambayo ni kichocheo cha ongezeko la shughuli za kiuchumi na kijamii, upatikanaji wa nyumba hususani za makazi na biashara na kutatua changamoto ya makazi duni katika maeneo ya miji nchini, kuboresha madhari ya miji yetu na kuongeza usalama wa milki za wananchi katika maeneo husika kwa kupatiwa hati za sehemu ya jengo na kuwawezesha wananchi kiuchumi kwa kugeuza ardhi mfu kuwa na thamani.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Bw. Saad Mtambule amesema program hiyo itakuwa suluhisho la changamoto ya mafuriko, magonjwa ya mlipuko, migogoro ya ardhi na itasaidia kuongeza thamani ya ardhi katika eneo hilo kwa kuweka miundombinu ya maji na barabara hatua itakayoboresha makazi ya wananchi wa eneo la Makangira jijini Dar es salaam.

Naye Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Mhe. Songoro Mnyonge amesema ujio wa program hiyo umekuja muda mwafaka ambapo manispaa hiyo mwaka 2013 ilipitisha Mpango wa Kuboresha  Makazi ili kupata nyumba bora za wananchi wa manispaa hiyo.

BALOZI DKT. NCHIMBI AZUNGUMZA NA WANANCHI WA NAMTUMBO










Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi akizungumza na umati mkubwa wa wananchi Namtumbo, kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Namtumbo, leo Alhamis tarehe 3 Aprili 2025.

Katika mkutano huo, viongozi wa vyama vya ACT Wazalendo na Chadema, wakiwaongoza wanachama wao, waliamua kurejesha kadi na vifaa vingine vya vyama hivyo, kisha wakajiunga CCM.

Viongozi hao, akiwemo Ndugu Alifa Jafa, Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Songea, Ndugu Mohamed Said Ndauka, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Ntungwe na Azarius Lucas Ngonyani, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Miembeni, walieleza jinsi ambavyo uongozi wa Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuteuliwa kwa Balozi Nchimbi kuwa mgombea mwenza wa Urais, kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 2025, umewavutia kuhamia CCM.

Thursday, April 03, 2025

SERIKALI ITAENDELEA KUBORESHA MAZINGIRA YA UWEKEZAJI-MAJALIWA




WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kufanya maboresho zaidi ya mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuifanya Tanzania iendelee kuwa sehemu salama zaidi ya uwekezaji.

Mheshimiwa Majaliwa ametoa kauli hiyo leo (Alhamisi, Aprili 3, 2025) wakati wa uzinduzi wa Maandalizi ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji Nchini (MKUMBI II) katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.

Amesema kupitia mpango ambao ameuzindua, maandalizi yake pamoja na kamati zake, Serikali itaweza kushughulikia mabadiliko ya kiuchumi, kijamii, na kiteknolojia na kuweka mazingira bora zaidi kwa wafanyabiashara na wawekezaji.

“Serikali itaendelea kutoa ushirikiano wa dhati kwa wadau wote ili kufanikisha malengo ya kuwa na mazingira mazuri ya uwekezaji na biashara. Ni mategemeo yetu kuwa, mpango huu utaongeza tija kubwa kwa Taifa letu na kusaidia kufikia malengo yetu ya kuwa na uchumi wa kati ulio endelevu.”

Akizungumza kuhusu umuhimu wa MKUMBI II, Waziri Mkuu amesema kuwa ni pamoja na kuvutia wawekezaji wa nje na ndani, kuongeza fursa za ajira, kuboresha miundombinu, upatikanaji wa soko la kimataifa kwa bidhaa za ndani, kukuza ushindani na ubora wa bidhaa.

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa ametumia fursa hiyo kuisisitiza kamati ya maandalizi ya MKUMBI II iharakishe maandalizi ya mpango huo ili utekelezaji wake uweze kuanza mara moja na kurahisisha mazingira bora kwa wafanyabiashara na wawekezaji.

Pia, Waziri Mkuu amezitaka Taasisi na Mamlaka za Udhibiti za Serikali ambazo zitahusishwa katika utafiti na tathmini zitoe ushirikiano wa dhati kwa kamati ili iweze kuja na mapendekezo mahsusi yenye malengo mapana ya nchi ambayo yataendana na Dira ya Taifa 2050.

Kwa upande wake, Waziri Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo amesema lengo la Serikali la kuandaa mpango huo ni pamoja na kuona kuwa Tanzania inakuwa sehemu bora na ya kuvutia ya kufanya biashara na uwekezaji. “Kazi ya kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ni kazi endelevu.”

Amesema ili uchumi uweze kukua ni lazima mazingira ya biashara na uwekezaji yafanyiwe mapitio na maboresho ya mara kwa mara, na ndio maana kamati ya kitaifa ya wataalam iliyoundwa imezingatia matakwa ya sasa ya uhitaji wa biashara na uwekezaji.

KAMATI YA PAC YARIDHISHWA NA UJENZI WA JENGO LA WIZARA YA ARDHI



Na Eleuteri Mangi

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), imeridhishwa na ujenzi wa jengo la Ofisi ya Makao Makuu ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi inayojengwa Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Hayo yamesema na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Mhe. Japhet Hasunga wakati wa ziara yao ya kukagua jengo hilo na kufuatilia matumizi ya fedha za umma kama zilivyoidhinishwa na Bunge na kujionea uhalisia wa fedha zilivyotumika.

“Tumeshuhudia ujenzi wa jengo unaendelea vizuri, lipo asilimia 95 kukamilika na lipo kwenye viwango kizuri sana. Kwa ujumla kamati yetu imeridhishwa sana na maendeleo ya ujenzi wa hili jengo na tunawapongeza Wizara kwa kusimamia vizuri, pamoja na Mkandarasi na Mshauri Elekezi kwa kufanya kazi vizuri, tumeona kazi ni nzuri sana kwa mujibu wa viwango stahiki kama vilivyoainishwa katika mkataba” amesema Makamu Mwenyekiti wa PAC, Mhe. Hasunga.

Mradi wa ujenzi wa jengo la Wizara hiyo una thamani ya takriban Shilingi billion 29.75 ambazo Shilingi billion 27.88 kwa ajili ya Mkandarasi wa ujenzi na Shilingi billion 1.87 kwa ajili ya Mshauri Elekezi.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba na maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga amesema Wizara hiyo imeshirikiana vizuri na Mkandarasi ambaye ni Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) na Mshauri Mwelekezi ambaye ni Wakala wa Majengo nchini (TBA) kwa kufanya kazi kwa ushirikiano mkubwa ambao umesaidia jengo hilo.

Mhandisi Sanga amemshukuru na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za ujenzi wa jengo hilo ambalo ni la kisasa na lina madhari nzuri kwa kazi ya kuwahudumia Watanzania.

Naye Mshauri Elekezi Meneja wa Mradi upande wa Mshauri Elekezi kutoka Wakala wa Majemngo Tanzania (TBA) Mbunifu Majengo Weja Ngolo amesema watatekeleza na kutimiza azma ya Kamati ya Bunge na watakamilisha kazi ndani ya muda wa mkataba.

MTUHUMIWA WA “KUFUTA MADENI” YA MIKOPO AKIRI KOSA, AHUKUMIWA KIGOMA

KIGOMA, Septemba 4, 2026 — Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Kigoma imemhukumu Nicholaus Komba Mahitana maarufu kama Abdallah Mahimbo baad...