Afisa Sheria Mwandamizi wa NHC, Scholastica Kilagane, alitoa elimu ya kina kuhusu dhana ya hati pacha (Unit title)
Uongozi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) umefanya kikao pamoja na wateja wake wa nyumba za makazi za Samia Housing Scheme jana, tarehe 2/5/2026, katika eneo la Kawe jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kuwajengea uelewa wa kina kuhusu umiliki wa nyumba za kisasa, hususan mfumo wa hati pacha pamoja na kuimarisha misingi ya usimamizi wa pamoja wa makazi hayo.
Akizungumza katika kikao hicho, kilichohudhuriwa na wamiliki wa nyumba hizo 560 zilizopo Kawe Tanganyika Packers Dar es Salaam, Afisa Sheria Mwandamizi wa NHC, Scholastica Kilagane, alitoa elimu ya kina kuhusu dhana ya hati pacha (Unit title), akieleza kuwa mfumo huo unampa mmiliki haki ya kumiliki sehemu yake binafsi ya nyumba huku akishiriki umiliki wa maeneo ya pamoja kama vile lifti, korido, ngazi, maeneo ya wazi na miundombinu mingine ya huduma.
Alisisitiza kuwa uelewa sahihi wa mfumo huo ni muhimu ili kuepusha migogoro ya kisheria na kuhakikisha matumizi bora ya mali hizo.
“Hati pacha inalenga kuweka uwazi katika umiliki wa mali na kugawanya wazi haki na wajibu wa kila mmiliki. Ni muhimu kwa kila mmiliki kuelewa kuwa pamoja na kumiliki nyumba yake, ana wajibu wa kushiriki kikamilifu katika kusimamia maeneo ya pamoja kwa mujibu wa sheria,” alieleza Kalagane.
Aidha, Kilagane alieleza umuhimu wa kuanzishwa kwa umoja wa wamiliki wa nyumba (Owners Association), akibainisha kuwa huo ndio chombo rasmi cha kisheria kitakachosimamia masuala yote ya pamoja ndani ya eneo hilo.
Alifafanua kuwa umoja huo utakuwa na viongozi watakaochaguliwa kwa mujibu wa taratibu za kisheria, ikiwemo Mwenyekiti, Katibu na Mweka Hazina, huku kila mmoja akiwa na majukumu mahsusi ya kuhakikisha uendeshaji mzuri na uwajibikaji.
Naye Injinia Grace Msita, Meneja Miradi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), akizungumza na wamiliki hao aliwahakikishia kuwa miundombinu yote ya Samia Housing Scheme imekamilika kwa viwango vya juu vya ubora na usalama, huku akisisitiza kuwa usimamizi madhubuti wa miradi hiyo wakati wa utekelezaji ni sehemu ya dhamira ya NHC ya kutoa makazi endelevu na yenye thamani kwa wananchi.
Alieleza kuwa NHC itaendelea kushirikiana na umoja wa wamiliki katika hatua zote za wakati huu wa kipindi cha uangalizi yaani DLP wa mradi huo ili kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi wa haraka na kwa weledi, na hivyo kulinda uwekezaji wa kila mmiliki pamoja na kuhakikisha mazingira ya kuishi yanabaki kuwa bora na ya kisasa.
Kwa upande wake, Meneja wa Milki wa NHC, France Bahangarwa, alisisitiza wajibu wa wamiliki katika kuhakikisha uendelevu wa huduma ndani ya Samia Housing Scheme. Alieleza kuwa ulipaji wa service charge ni sharti la kisheria lisiloweza kuepukika kwani ndilo linalowezesha uendeshaji wa huduma muhimu za pamoja.
“Huduma kama lifti, usafi wa mazingira, ulinzi, taa za maeneo ya pamoja na matengenezo ya miundombinu haviwezi kuendelea bila michango ya wamiliki. Hivyo, kila mmiliki ana wajibu wa kulipa service charge kwa wakati ili kuhakikisha mazingira haya yanaendelea kuwa salama na yenye hadhi,” alisema Bahangarwa.
Aliongeza kuwa pamoja na hilo, wamiliki wanapaswa kutekeleza majukumu yao mengine ya kisheria ikiwemo kulipa kodi ya ardhi na kushiriki katika maamuzi ya pamoja kupitia umoja wao. Pia alisisitiza umuhimu wa kuajiri kampuni ya usimamizi wa milki au mtaalamu binafsi ili kuhakikisha shughuli za kila siku za uendeshaji zinafanyika kwa weledi na kwa kuzingatia viwango vya kitaalamu.
“Usimamizi wa kitaalamu ni nguzo muhimu katika mafanikio ya miradi ya makazi ya aina hii. Ni vyema wamiliki wakachagua njia bora ya usimamizi itakayolinda thamani ya mali zao na kuboresha maisha yao kwa ujumla,” aliongeza Bahangarwa.
Kwa upande wao, wamiliki wa nyumba katika Samia Housing Scheme walieleza kuridhishwa na kikao hicho, wakitoa shukurani kwa Shirika la Nyumba la Taifa kwa kuwapatia elimu hiyo muhimu.
Mmoja wa wamiliki alieleza kuwa, “Tunashukuru sana NHC kwa kutuletea elimu hii. Imetusaidia kuelewa kwa undani haki na wajibu wetu kama wamiliki wa nyumba za mfumo huu wa kisasa. Sasa tunaona umuhimu wa kushirikiana na kuunda umoja imara kwa ajili ya maendeleo ya makazi yetu.”
Kwa ujumla, kikao hiki kimekuwa jukwaa muhimu la kuwawezesha wamiliki kwa maarifa sahihi ya kisheria na kiutendaji, hatua inayotarajiwa kuimarisha usimamizi wa pamoja, kuongeza thamani ya mali na kuhakikisha Samia Housing Scheme inakuwa mfano bora wa makazi ya kisasa yanayosimamiwa kwa ufanisi nchini.
Naye Meneja Mauzo na Masoko wa NHC, Deogratius Batakanwa alieleza kuwa Samia Housing Scheme ni zaidi ya makazi; ni uwekezaji wenye thamani unaohitaji uelewa sahihi wa kisheria na usimamizi wa pamoja ili kulinda na kukuza thamani yake kwa muda mrefu.
“Kupitia mfumo wa hati pacha, kila mmiliki anapata umiliki halali wa sehemu yake binafsi huku akishiriki umiliki wa maeneo ya pamoja. Huu ni mfumo wa kisasa unaolenga kuongeza uwazi, kulinda uwekezaji na kuhakikisha mazingira bora ya kuishi kwa wakazi wote,” alisema Batakanwa.
Alisisitiza kuwa uelewa wa mfumo huo unawawezesha wamiliki kufanya maamuzi sahihi kuhusu mali zao na kushiriki kikamilifu katika uendeshaji wa makazi yao kwa tija.
Katika kuimarisha usimamizi wa pamoja, Batakanwa alibainisha umuhimu wa kuunda umoja wa wamiliki wa nyumba (Owners Association) utakaosimamia masuala ya pamoja kwa weledi na uwazi. Alieleza kuwa uongozi wa umoja huo utachaguliwa kwa kufuata taratibu rasmi na utakuwa na jukumu la kuhakikisha huduma zote zinaendeshwa kwa ufanisi.
Katika hatua ya kuimarisha usimamizi wa pamoja, wamiliki wa Samia Housing Scheme wamechagua uongozi wa umoja wao ukiongozwa na Mwenyekiti Catherine Mrosso akisaidiwa na Makamu Mwenyekiti Eng. Juma Kiboko, huku nafasi ya Katibu ikishikiliwa na Grace Lemunge akisaidiwa na Katibu Msaidizi George Laurian, na Mweka Hazina akiwa Veronica Rukeha.
Wajumbe wa kamati hiyo ni Rehema Chonda, Ramadhani Mshana, Dkt. Petronila Ngiloi, Bi. Hadija Mwema, Isack Ngovi, Faith Kayombo, Robert Matapu, Jesca Macharia, Salma Juma, Dkt. Oreste Munishi na Grace Mwaihojo.
Kwa upande wao, wamiliki wa nyumba walitoa shukurani kwa NHC kwa kuandaa kikao hicho, wakieleza kuwa elimu waliyoipata imewasaidia kuelewa thamani halisi ya uwekezaji wao na namna bora ya kuilinda.
“Tunathamini jitihada za NHC kutuelimisha. Sasa tunaelewa kuwa mafanikio ya makazi haya yanategemea ushirikiano wetu na utekelezaji wa majukumu yetu ipasavyo,” walieleza baadhi ya wamiliki.
Kwa ujumla, kikao hiki kimeweka msingi thabiti wa kuifanya Samia Housing Scheme kuwa mfano wa makazi ya kisasa yanayosimamiwa kwa ufanisi, huku yakitoa thamani ya juu kwa wamiliki wake—ikiwa ni sehemu ya dhamira ya NHC ya kuendeleza makazi bora na uwekezaji salama kwa Watanzania.
No comments:
Post a Comment