Monday, March 20, 2006

Kwa staili hii wapigadebe, wamachinga watastawi

NI lazima niseme kuwa ni mmoja wa watu ambao hawakushangazwa hata kidogo na matokeo ya uchaguzi mkuu uliopita, ingawa bado watu wengi wanabakia na hisia na au maswali mengi kwa nini CCM kinaendelea kutawala siasa za Tanzania pamoja na kushindwa kwao kukidhi matakwa mengi ya wananchi wake na haswa kwa upande wa ukosefu wa ajira.

Katika maelezo ya kitaaluma yapo maainisho ya aina mbili yanayoendana na hali hii. Ya kwanza ni kwamba wapiga kura wanakichagua chama kutokana na ufanisi wake. Hii hasa ni nadharia ya kiuchambuzi.

Ainisho la pili ni kwamba, wapiga kura walikichagua chama hicho ili kujitengenezea uchochoro wa kuweza kufanya 'madudu yao' kama kawaida kutokana na ule usemi na pengine mazoea ya 'zimwi likujualo halikuli likakwisha'

Kuna ukweli ndani ya nadharia hizi mbili kwa kutegemea hasa ni nini lengo lako msomaji ingawa ukweli halisi unabakia kwa mchambuzi.

Sina haja ya kujadili nini kilikuwa nini, lakini kiufupi matokeo ya uchaguzi kiuhakika yanathibitisha ubabe tu wa CCM katika siasa za uchaguzi na kamwe siyo ubora wa uongozi itakaoutoa kwa wavuja jasho na wafyeka nyasi wa nchi hii, kwa sasa na hata baadaye.

Matokeo hayo ya uchaguzi yanatueleza kwamba, mfumo wetu wa siasa unajionesha na kujikita mno katika uwingi wa watu, lakini hazionyeshi uhusiano wa kina uliopo baina ya chama hicho kilichochaguliwa kwa uwingi wa kura kwa upande mmoja na mahakama, bunge, vyombo vya habari, vyuo vikuu na jumuiya za kiraia kwa upande mwingine.

Fikra za kuwa uwingi ndiyo ubora bila ya kuzingatia ubora, ndizo zinazoonyesha kutawala vichwa vyetu hata katika tunavyofikiria kuunda sera zinazoathiri umma.

Kila siku tunatwikwa mizigo ya matarajio ya makuzi. Aidha ya uchumi au kitu kingine chochote kwa kuzingatia uwingi, lakini ni nadra kuwa na mijadala ya kuinua ubora ili kupunguza umasikini, kuongeza ajira na kuondoa pengo lililopo baina ya walio nacho na wasio nacho.

Hata kama tunazungumzia siasa za uchaguzi au sera za kunufaisha umma, kunaweza kukawa hakuna garantii ya demokrasia yetu na hasa katika ubora wa demokrasia hiyo tunayoilenga.

Wiki hii nzima imegubikwa na operesheni mbalimbali lakini kubwa ni tatu, yaani ya kwanza kabisa ikiwa ni ya majambazi, ya pili ikiwa ni bomoa bomoa na kisha ile ya tatu ni ya kufukuza wapiga debe.

Sina tatizo kabisa na operesheni ya kufagia majambazi. Lakini nina matatizo makubwa sana katika fikra zangu na hizi operesheni mbili za bomoa bomoa ya vibanda na kisha wapiga debe.

Hivi wakati hawa wazembe wanaoshinda vituoni kwa kupiga kelele walipokuwa wakianza huu 'usanii' wao katika vituo, mamlaka zilikuwa wapi mpaka wanajikusanya na kuwa na nguvu namna hii.

Upande mmoja wa mawazo unaweza ukatetea kuwa walikuwa sahihi kutokana na hali ngumu, kwamba walijibunia aina yao ya ajira, lakini hapana sijapata kuona katika majiji yoyote makubwa niliyotembelea duniani aina hii ya kazi.

Kwanza hebu tufuatilie kwa kina kabisa ni nini chanzo cha haya matata yote mpaka hawa wamachinga wanatanda mabarabarani, wapiga debe wanazidi vituoni, utagundua kuwa chanzo ni ukosefu wa ajira ambao una milolongo ya masuala ambayo huko nyuma hayakutiliwa mkazo kama elimu, kilimo na elimu ya stadi za maisha kama nilivyoeleza hapo juu.

Ninavyoona mimi hata kama tukibomoa vibanda na kisha tukamwaga sumu katika maeneo hayo au hata mitego ili watakaogusa wanaswe, bado vibanda vitajengwa, wapiga debe watabakia sababu suala la msingi halijaguswa. Yameguswa matawi badala ya mashina.

Mashina ni matatizo ya msingi yanayosababisha matata yote haya na matawi ndiyo hii bomoa bomoa. Tutawapiga risasi bure wafanya biashara ndogo ndogo, tutawajeruhi na tutafanya kila kitu lakini bila kuweka sawa masuala ya msingi ni bure.

Sikatai kuwa zipo jitihada za kukabiliana na umasikini za serikali zilizoibuka na mkakati wa MKUKUTA na MKURABITA, lakini zinasubiri nini. Maisha yanaendelea hivyo na wananchi ndiyo maana wanafanya vituko mabarabarani njaa haichagui. Hivyo cha msingi ni bora tukashughulikia masuala ya msingi.

No comments: